1Kwa hasira yake,
Yawe amewaweka watu wa Sayuni katika giza.
Ametupa toka mbinguni mpaka katika dunia utukufu wa Israeli.
Kwa siku ya hasira yake,
alilitupilia mbali hata hekalu lake.
2Yawe ameharibu bila huruma
makao yote ya wazao wa Yakobo.
Kwa kasirani yake amevibomoa vikingio vya watu wa Yuda.
Ametupa chini na kuchafua
ufalme wao na watawala wake.
3Ameivunja kwa hasira nguvu yote ya Israeli.
Hakunyoosha mukono kwa kuwasaidia
walipokutana na adui;
amewawakia watu wa Yakobo kama moto,
akateketeza kila kitu.
4Amevuta upinde wake kama adui,
na kuuweka mukono wake wa kuume tayari,
amewaua wote waliopendeza macho.
Amemwanga hasira yake kama moto
katika hema yetu watu wa Sayuni.
5Yawe amekuwa kama adui,
ameangamiza watu wa Israeli;
ameharibu nyumba zake kubwa zote,
amevibomoa vikingio vyake.
Amewazidishia watu wa Yuda
kilio na maombolezo.
6Amelibomoa hekalu lake kama kibanda katika bustani,
ameharibu pahali pake pa kusanyiko.
Amefanya sikukuu na siku ya Sabato visahauliwe kule Sayuni,
kwa hasira yake kubwa amewakataa mufalme na makuhani.
7Yawe amechukia mazabahu yake
na hekalu lake amelikataa.
Amewaachilia waadui wazibomoe kuta za nyumba zake katika muji.
Wakapiga kelele ndani ya nyumba ya Yawe
kama kelele za wakati wa sikukuu.
8Yawe alikusudia kuubomoa ukuta wa Sayuni;
aliupima na kuhakikisha kila kitu kwamba kimeharibika;
minara na kuta za inje ya muji akazifanya ukiwa,
zote kwa pamoja zikaangamia.
9Milango yake imezama ndani ya udongo,
ameharibu na kuvunjavunja vifungio vyake.
Mufalme na wakubwa wake wako katika uhamisho kati ya mataifa.
Hakuna sheria tena,
manabii wake hawapati tena maono
kutoka kwa Yawe.
10Wazee wa Sayuni wameikaa chini kimya,
wamejitia mavumbi juu ya vichwa
na kuvaa gunia.
Wabinti wa Yerusalema wameinamisha vichwa chini.
11Macho yangu yamevimba kwa kulia,
roho yangu imechafuka,
moyo wangu una huzuni nyingi,
kwa sababu ya kuangamizwa kwa watu wangu,
kwa sababu watoto wachanga na wale wanaonyonya wanazimia
katika barabara za muji.
12Wanawalilia wamama zao:
Chakula kiko wapi, kinywaji kiko wapi?
Wanazimia kama wale walioumizwa
katika barabara za muji,
na kukata roho katika mikono ya wamama zao.
13Nikuambie nini, ee Yerusalema?
Nikulinganishe na nini?
Nikufananishe na kitu gani
kusudi niweze kukufariji,
ee Sayuni uliyekuwa muzuri?
Maangamizi yako ni mengi kama bahari,
ni nani atakayekuponyesha?
14Manabii wako wamekuonea maono madanganyifu.
Hawakufichua wazi uovu wako
kusudi wapate kukurudishia hali yako ya mbele.
Lakini walikuonea maono ya uongo na ya kupotosha.
15Wapita njia wote wanakuchekelea;
wanakupigia muunzi, ee Yerusalema,
wakitikisa vichwa vyao kwa mazarau na kusema:
Huu ndio ule muji uliofikia ukamilifu wa uzuri,
muji uliokuwa furaha ya dunia nzima?
16Waadui zako wote wanakuzomea,
wanakupigia muunzi na kukusagia meno,
nao wanasema: Tumemwangamiza!
Kweli, siku ile tuliyoingojea kwa hamu
sasa imefika na tumeiona!
17Yawe amefanya yale aliyokusudia,
ametimiza yale aliyoagiza.
Kama alivyopanga tangu kale,
ameangamiza bila huruma yoyote.
Amewafanya waadui wafurahie azabu yako,
amewatukuza mashujaa wa waadui zako.
18Ee Sayuni, umulilie Yawe!
Machozi yatiririke kama muto muchana na usiku!
Lia na kuomboleza bila kupumzika!
19Usiku kucha uamukeamuke na kulia.
Umufungulie Yawe yanayokuwa ndani ya moyo wako.
Umwinulie mikono yako kwa kuwaombea watoto wako,
watoto wanazimia na njaa popote katika barabara.
20Angalia, ee Yawe, uone!
Kuna yeyote uliyemutendea kama ulivyotutendea sisi,
hata wamama wawakule watoto wao
nao makuhani wauawe ndani ya hekalu lako?
21Maiti za vijana na wazee
zimelala ndani ya mavumbi katika barabara,
wabinti na vijana wangu wameuawa kwa upanga;
umewaua bila huruma siku ya hasira yako.
22Umewaalika kama kwenye sikukuu
waadui zangu walionitisha kila upande.
Katika siku ya hasira yako, ee Yawe,
hakuna aliyetoroka au kubakia.
Wale niliowazaa na kuwalea,
waadui zangu wamewaangamiza.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.