Isaya 17 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu ataazibu Asuria na Israeli

1Ujumbe wa Mungu juu ya muji wa Damasiki.

Damasiki utakoma kuwa muji;

utakuwa lundo la mabomoko.

2Miji inayokuwa chini yake imeachwa matongo milele.

Itakuwa makao ya makundi ya nyama,

wala hakuna mutu atakayewatisha.

3Pango za Efuraimu zitatoweka,

na utawala wa Damasiki utakwisha.

Waaramu ambao watabaki wazima,

hawatakuwa na utukufu zaidi kama wazao wa Israeli.

–Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.

Watakaobaki katika Israeli

4Siku hiyo, utukufu wa Yakobo utaporomoshwa,

na unono wake utapotea.

5Itakuwa kama wakati wa mavuno,

wakati wamekwisha kuokota ngano,

na kukusanya masuke katika mukono.

Hakika, itakuwa kama bonde la Refaimu

wakati wamekwisha kuvuna ngano.

6Watabaki wachache kama vile kisha kuangusha matunda ya mizeituni:

matunda mawili au matatu katika tawi la juu;

mane, matano katika matawi yanayozaa sana.

–Ni ujumbe wa Yawe, Mungu wa Israeli.

Mwisho wa kuabudu sanamu

7Siku hiyo, watu watamwangalia Muumba wao, na kuelekeza macho yao kwa huyo Mutakatifu wa Israeli.

8Hawataelekea tena mazabahu ambazo ni kazi za vidole vyao wenyewe, wala kuzitazamia tena kazi za mikono yao wenyewe, ni kusema sanamu za mungu Ashera na mazabahu za kufukizia ubani.

9Siku hiyo miji yao imara itaachwa matongo, kama miji ambayo Wahivi na Waamori waliihama walipokuwa wakiwakimbia wazao wa Israeli. Kila kitu kitakuwa uharibifu.

10Maana wewe Israeli umemusahau Mungu aliyekuokoa,

haukukumbuka Jiwe lako la kufichamia.

Kwa hiyo, hata mukipanda mimea ya Bali,

na kuitakasa kwa mungu wa kigeni;

11hata mukiifanya ikomae siku hiyohiyo muliyoipanda

na kuifanya ichanue asubui hiyohiyo,

mavuno yenu yatatoweka

siku hiyo ya hasara na maumivu yasiyoweza kuponyeshwa.

Mataifa adui yanashindwa

12Aha! Ngurumo ya watu wengi!

Wananguruma kama bahari.

Aha! Mulio wa watu wa mataifa!

Yanatoa mulio kama wa maji mengi.

13Mataifa yananguruma kama ngurumo ya maji mengi,

lakini Mungu atayakaripia, nayo yatakimbilia mbali.

Yatafukuzwa kama maganda juu ya mulima mbele ya upepo;

kama mavumbi yanayonyanyuliwa na upepo mukali.

14Wakati wa magaribi yanaleta hofu kubwa,

lakini mbele ya asubui yametoweka!

Ndilo litakalowapata wale wanaotukamata

na kutunyanganya mali yetu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help