Ezekieli 4 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Muji Yerusalema utashambuliwa

1Yawe akaniambia tena: Wewe mwanadamu, twaa tofali, uliweke mbele yako na uchape juu yake muji, kama wa Yerusalema.

2Onyesha kwamba muji ule umeshambuliwa. Utaujengea nafasi za kupandia juu ya kuta zake. Kandokando yake uweke makambi ya waaskari, na gongo ya kubomoa kuta.

3Nawe utwae bamba la chuma. Ulisimamishe likuwe kama ukuta wa chuma kati yako na muji. Kisha utaelekezea muji huo uso wako nao utashambuliwa na utaushambulia. Hiki kitakuwa kitambulisho kwa taifa la Waisraeli.

4Kisha, uende ulalie mbavu kwa upande wako wa kushoto. Muda wote utakapokaa katika hali hiyo utabeba uovu wa Waisraeli kama muzigo muzito.

5Nimekupangia muda wa siku mia tatu na makumi kenda. Muda huu ni sawa na miaka ya azabu yao: siku moja ni sawa na mwaka mumoja. Utabeba azabu ya Waisraeli kwa muda huu.

6Utakapotimiza siku hizo, utalalia kwa upande wa kuume, na hapo utabeba azabu ya watu wa ufalme wa Yuda kwa muda wa siku makumi ine; nimekupangia siku moja kuwa sawa na mwaka mumoja.

7Kisha, utauelekea Yerusalema ulioshambuliwa kwa vita na kuunyooshea mukono mutupu na kutabiri juu yake.

8Nitakufunga kamba kusudi usiweze kugeuka toka upande mumoja mpaka upande mwingine, mpaka wakati kushambuliwa kwa Yerusalema kutakapomalizika.

9Wewe utwae ngano, shayiri, mahalagi, manjegere, mutama na ulezi, uvitie vyote katika chombo kimoja, ujitengenezee mukate. Mukate huo ndio utakaokuwa chakula chako wakati unapolala kwa upande mumoja, siku zote mia tatu na makumi kenda.

10Chakula utakachokula kitapimwa, nacho kitakuwa grama mia mbili makumi tatu kwa siku; nawe utakula mara moja tu kwa siku.

11Maji nayo utayakunywa kwa kipimo: vikombe viwili, mara moja kwa siku.

12Utatwaa mavi ya mutu, uwashe nayo moto, upike mukate juu yake na kuukula mbele ya watu.

13Yawe aliniambia: Vile ndivyo Waisraeli watakavyokula mukate wao muchafu wakiwa kati ya mataifa ninakowapeleka.

14Halafu nikamwambia hivi: Ee, Bwana wangu Yawe, sijajichafua hata kidogo kwa kula nyamafu wala nyama aliyeuawa na nyama wa pori, wala sijapata kuonja nyama anayehesabiwa kuwa muchafu tangu ujana wangu.

15Kisha akaniambia: Basi, ninakuruhusu utumie mavi ya ngombe pahali pa mavi ya mutu kwa kupika mukate wako.

16Tena akaniambia hivi: Wewe mwanadamu, mimi nitaharibu akiba ya chakula katika Yerusalema; wakaaji wake watakula chakula watakachopimiwa kwa hofu. Watakunywa maji watakayopimiwa kwa kufazaika.

17Nitafanya hivyo kusudi wakose chakula na maji, na kila mumoja atamwangalia mwenzake kwa kufazaika; nao watakuwa zaifu kwa ajili ya azabu yao.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help