1Mordekayi alipojua yote yaliyotukia, akapasua nguo zake, akavaa nguo ya gunia, na kujitia majivu. Kisha, akapita katikati ya muji akilia kwa sauti ya uchungu.
2Akakwenda mpaka kwenye mulango wa nyumba ya mufalme, lakini hakuweza kuingia kwa sababu hakuna mutu aliyeruhusiwa kuingia katika nyumba ya kifalme akiwa amevaa nguo ya gunia.
3Katika kila jimbo, mara tu amri ya mufalme ilipotangazwa, kilio kikubwa kiliwapata Wayuda. Wakafunga, wakalia na kuomboleza; na wengi wao wakalala katika majivu wakiwa wamevaa magunia.
4Malkia Esteri alipoarifiwa na matowashi na wajakazi wake habari za Mordekayi akahuzunika sana. Akamupelekea Mordekayi nguo za kuvaa kwa pahali pa nguo ya gunia, lakini Mordekayi akazikataa.
5Basi, akamwita Hataki, mumoja wa matowashi wa mufalme aliyechaguliwa na mufalme amutumikie Esteri, akamutuma kwa Mordekayi kuuliza maneno na maana ya tukio hilo.
6Hataki akamwendea Mordekayi katika uwanja, mbele ya mulango wa nyumba ya kifalme.
7Mordekayi akamwelezea Hataki yote yaliyokuwa yamemupata, na kiasi kamili cha feza ambayo Hamani alikuwa ameahidi kulipa katika hazina ya mufalme kama Wayuda wote wangeangamizwa.
8Akamupa na barua moja ya tangazo lililokuwa limetolewa katika muji wa Susani juu ya kuangamizwa kwa Wayuda, akamwomba amupelekee Esteri na kumwelezea jinsi hali inavyokuwa, na kumwambia aende kumusihi mufalme na kumwomba awahurumie Wayuda, watu wa Esteri.
9Hataki akaenda akamwelezea Esteri maneno yote Mordekayi aliyosema.
10Naye Esteri akamwambia Hataki arudie amwambie Mordekayi:
11“Watumishi wote wa mufalme na watu wote wa majimbo yote wanajua kwamba mutu yeyote yule akiingia katika kiwanja cha ndani na kumwona mufalme bila kuitwa, huyo anapaswa kuuawa. Anayeweza kuponyoka ni yule tu ambaye mufalme atamunyooshea fimbo yake ya zahabu kwa kumuponyesha. Na mimi sijaitwa na mufalme, yapata mwezi muzima sasa.”
12Mordekayi alipopata ujumbe wa Esteri,
13akamutumia onyo hili: “Usizani kwamba kwa sababu upo katika nyumba ya kifalme wewe uko salama zaidi kuliko Muyuda mwingine yeyote.
14Ukikaa kimya wakati kama huu, musaada utawafikia Wayuda kutoka pahali pengine, nao wataokolewa; lakini wewe utakufa, na jamaa ya baba yako itaangamia. Ni nani anayejua pengine umefanywa kuwa malkia kwa ajili ya wakati kama huu!”
15Esteri akamupelekea Mordekayi jibu hili:
16“Kwenda uwakusanye pamoja Wayuda wote wanaokuwa katika muji wa Susani. Mufunge, musikule wala musikunywe kwa siku tatu, usiku na muchana, kwa ajili yangu. Na mimi na wajakazi wangu tutafanya vile vile. Kisha, nitamwendea mufalme, ingawa ni kinyume cha sheria. Kama ni kuuawa, niuawe.”
17Basi, Mordekayi akaenda zake na kufanya kama vile Esteri alivyomwambia.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.