Matayo 10 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mitume kumi na wawili(Mk 3.13-19; Lk 6.12-16)

1Yesu akawaita wanafunzi wake kumi na wawili na akawapa mamlaka ya kufukuza pepo na kuponyesha magonjwa yote na uzaifu wa kila namna.

2Na haya ndiyo majina ya hao mitume wake kumi na wawili: kwanza Simoni (anayeitwa vilevile Petro) na ndugu yake Andrea; Yakobo na ndugu yake Yoane, ambao ni wana wa Zebedayo;

3kisha Filipo na Bartolomayo, Toma na Matayo aliyekuwa mulipishaji wa kodi; Yakobo mwana wa Alfayo, na Tadeo;

4Simoni wa kundi la Wazeloti, na Yuda Iskariota aliyemutoa Yesu.

Yesu anawatuma mitume kumi na wamili(Mk 6.7-13; Lk 9.1-6)

5Hao ndio wanafunzi kumi na wawili Yesu aliowatuma, akiwaagiza mambo haya: “Musiende katika inchi za watu wa mataifa mengine wala musiingie katika muji wowote wa Samaria.

6Lakini muwaendee wandugu zenu wa inchi ya Israeli, wanaokuwa kama kondoo wanaopotea.

7Mutakapokuwa mukienda, muhubiri kwa watu kwamba Ufalme wa mbinguni umekaribia!

8Muponyeshe wagonjwa, mufufue wafu, mutakase wenye ukoma, mufukuze pepo. Mulipokea bure, mutoe bure vilevile.

9Musibebe zahabu, wala feza, wala vikoroti vya shaba ndani ya mikaba yenu.

10Vilevile musibebe mifuko, kanzu mbili, viatu wala fimbo, kwa sababu mutumishi anastahili kupewa posho lake.

11“Mutakapoingia katika muji au katika kijiji, mutafute mutu anayekuwa tayari kwa kuwakaribisha, nanyi mukae kwake mpaka mutakapotoka kule.

12Mutakapoingia ndani ya nyumba, muwasalimie watu wanaokuwa mule, mukisema: ‘Amani kwenu.’

13Kama watu wa nyumba ile wakiwakaribisha, wakuwe na amani ile muliyowatakia, lakini wasipowakaribisha, amani ile iwarudilie.

14Na katika nyumba au muji wowote watakapokataa kuwakaribisha na kukataa kusikiliza maneno yenu, mutakapotoka kule mukungute mavumbi toka juu ya miguu yenu.

15Kweli ninawaambia: kwa Siku ya hukumu, watu wa muji ule wataazibiwa vikali zaidi kuliko watu wa muji wa Sodoma na wa Gomora.

Mateso yatakayokuja(Mk 13.9-13; Lk 21.12-17)

16“Muangalie! Ninawatuma kama kondoo katikati ya imbwa wa pori. Basi mukuwe waangalifu kama nyoka na wakamilifu kama njiwa.

17Mujilinde, kwa maana watu watawapeleka mbele ya tribinali kubwa nao watawapiga fimbo ndani ya nyumba zao za kuabudia.

18Vilevile mutapelekwa mbele ya wakubwa na wafalme kwa ajili yangu, kusudi mutoe ushuhuda wangu mbele yao na mbele ya watu wa mataifa mengine.

19Lakini watakapowapeleka kwa kuhukumiwa, musijihangaishe juu ya maneno mutakayoyasema wala juu ya namna mutakavyosema, kwa maana saa ile ile mutapewa maneno mutakayoyasema.

20Maneno mutakayoyasema hayatatoka kwenu, lakini yatatoka kwa Roho wa Baba wenu Mungu atakayesema ndani yenu.

21“Ndugu atamutoa ndugu, kusudi auawe, na baba atamutoa mutoto wake, nao watoto watawageukia wazazi wao na kuwaua.

22Na watu wote watawachukia kwa ajili yangu. Lakini atakayevumilia mpaka mwisho ataokolewa.

23Watakapowatesa katika muji mumoja, mukimbilie katika muji mwingine. Kweli ninawaambia: hamutamaliza kuzunguka katika miji yote ya Israeli mbele ya kurudi kwa Mwana wa Mutu.

24“Mwanafunzi hamupiti mwalimu wake, wala mutumishi hamupiti bwana wake.

25Lakini inatosha kwa mwanafunzi kufanana na mwalimu wake na mutumishi kufanana na bwana wake. Ikiwa wanamwita mukubwa wa jamaa Belzebuli, hawatakosa kuwaita watu wa jamaa yake kwa majina mabaya zaidi.

Mungu tu anatahili kuogopewa(Lk 12.2-7)

26“Basi musiwaogope watu wale. Hakuna kitu chochote kinachofichwa kitakachokosa kuvumbulikana wala hakuna siri itakayokosa kujulikana.

27Neno ninalowaambia katika giza, muliseme muchana kati. Vilevile neno munalosikia kwa siri, mulitangaze mukisimama juu ya paa ya nyumba.

28Musiwaogope wale wanaoweza kuua tu mwili, lakini wasioweza kuua roho. Lakini zaidi mumwogope Mungu anayeweza kuharibu mwili pamoja na roho katika jehenamu.

29Ndege wawili wadogo wanauzishwa kwa bei chini kabisa. Ingawa vile hakuna hata mumoja wao anayekufa bila mapenzi ya Baba yenu.

30Na kwa upande wenu, yeye anajua hesabu ya nywele zote za vichwa vyenu.

31Basi musiogope, kwa sababu ninyi ni bora zaidi kuliko kundi la ndege wengi!

Kumukubali na kumukana Kristo(Lk 12.8-9)

32“Kila mutu anayenikubali mbele ya watu, nami nitamukubali vilevile mbele ya Baba yangu anayekuwa mbinguni.

33Lakini kila mutu anayenikana mbele ya watu, nami nitamukana vilevile mbele ya Baba yangu anayekuwa mbinguni.

Yesu analeta matengano(Lk 12.51-53; 14.26-27)

34“Musifikiri kwamba nimekuja kuleta amani katika dunia. Mimi sikukuja kuleta amani, lakini upanga.

35Kwa maana nimekuja kuleta matengano kati ya mutu na baba yake, kati ya binti na mama yake, kati ya mukwe na mama mukwe;

36na adui wa mutu atakuwa wa jamaa yake mwenyewe.

37“Yeye anayemupenda baba yake au mama yake kuliko mimi, hastahili kuwa wangu, na yeyote anayemupenda mwana wake au binti yake kuliko mimi hastahili kuwa wangu vilevile.

38Naye asiyejitolea kwa kubeba musalaba wake na kunifuata hastahili kuwa wangu.

39Kwa maana mutu anayetaka kulinda uzima wake, ataupoteza; lakini yule atakayetoa uzima wake kwa ajili yangu, ataupata tena.

Zawadi ya wenye kupokea wafuasi wa Yesu(Mk 9.41)

40“Mutu anayewapokea ninyi, ananipokea mimi; naye anayenipokea, anamupokea yule aliyenituma.

41Yule anayemupokea nabii wa Mungu, kwa sababu ni nabii, atapokea zawadi sawa nabii yule. Vilevile yule anayemupokea mwenye haki, kwa sababu ni mwenye haki, atapokea zawadi sawa yule mwenye haki.

42Na yeyote atakayetoa hata kikombe kimoja tu cha maji ya baridi kwa mumoja wa hao wanaokuwa wadogo kati ya wanafunzi wangu, kwa sababu yeye ni mwanafunzi wangu, kweli ninawaambia: mutu yule hatakosa kupewa zawadi yake.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help