Waroma 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Uhuru toka vifungo vya Sheria

1Wandugu zangu, munajua uhakika juu ya maneno haya nitakayowaambia, kwa maana ninyi ni watu wanaoelewa Sheria vizuri: Sheria haina mamlaka juu ya mutu isipokuwa tu wakati angali muzima.

2Kwa mufano, mwanamuke aliyeolewa anafungwa na Sheria katika maisha yake na mume wake wakati mume wake angali muzima. Lakini kama mume wake akikufa, yeye anakuwa huru kufuatana na Sheria ile iliyomufunga.

3Basi kama akiolewa na mutu mwingine wakati mume wake angali muzima, atahesabiwa kuwa muzinzi. Lakini kama mume wake akikufa, yeye anakuwa huru toka Sheria ile iliyomufunga na hata akiolewa na mutu mwingine hatahesabiwa kuwa muzinzi.

4Nanyi wandugu zangu, ni hivi inavyokuwa kwa ngambo yenu. Kufuatana na maneno ya Sheria, ninyi vilevile mumekufa, kwa maana muliungana na mwili wa Kristo. Na sasa munakuwa wa mutu mwingine, ndiye yule aliyefufuka, kusudi tupate kufanya matendo yanayofaa katika kazi ya Mungu.

5Kwa maana tulipoishi maisha ya kimwili, tamaa ya kufanya zambi iliyotokana na Sheria ilitumika ndani yetu na kutuletea kifo.

6Lakini sasa tumekuwa huru toka vifungo vya Sheria, kwa maana tunakuwa kama waliokufa kufuatana na mambo yale yaliyotufunga. Kwa hiyo tunaweza kumutumikia Mungu kwa kufuata njia mupya chini ya uongozi wa Roho wake, wala si kufuata njia ya zamani chini ya uongozi wa maandiko ya Sheria.

Zambi inajulikana kutokana na Sheria

7Tuseme nini basi? Sheria ni zambi? Hapana hata kidogo! Lakini pasipo Sheria singejua zambi ni nini. Kwa maana singejua kutamani ni nini kama Sheria isingesema: “Usitamani.”

8Kutokana na amri, zambi ilipata njia hata kuamusha kila namna ya tamaa ndani yangu. Kwa maana pasipo Sheria zambi ingekuwa kama mufu.

9Zamani nilikuwa muzima pasipo kujua Sheria, lakini wakati amri ilipotokea, zambi ikaanza kutenda kazi,

10nami nikakufa. Hivi ile amri iliyopasa kuniletea uzima ikaniletea kifo.

11Maana kutokana na amri ile, zambi ilipata njia ya kunidanganya na kuniua kufuatana na amri ile ile.

12Basi Sheria yenyewe ni takatifu na amri ni takatifu, ya haki na nzuri.

13Basi ni kusema kile kinachokuwa kizuri kimeniletea kifo? Hapana hata kidogo! Ni zambi ndiyo iliyoniletea kifo. Lakini kusudi zambi ionekane kuwa zambi kweli kweli, ilipitia kwa njia ya kile kinachokuwa kizuri kwa kusababisha kifo changu. Hivi kwa njia ya amri ile, zambi ilizidi kujikamilisha kuwa zambi kabisa.

Mapigano ndani ya mutu

14Tunajua kwamba Sheria inaelekea maisha ya kiroho, lakini mimi ni mutu wa kimwili, kwa maana nimeuzishwa kama vile mutumwa wa zambi.

15Hakika sijui kitu ninachofanya. Kwa maana kile ninachotaka kufanya, sikifanyi; lakini kile ninachochukia, ndicho ninachofanya.

16Ikiwa kile ninachofanya ndicho nisichotaka, maana yake ninakubali ya kuwa Sheria ni nzuri.

17Basi sasa si mimi ninayekifanya, lakini ni zambi inayokaa ndani yangu.

18Kwa maana ninajua kwamba hakuna kitu kizuri kinachokaa ndani yangu, ni kusema katika hali yangu ya kimwili. Ni hivi kwa sababu ninakuwa na utashi wa kufanya jambo jema, lakini sifikii kulifanya.

19Jambo jema ninalotaka kufanya, silifanyi, lakini jambo baya nisilotaka, ndilo ninalofanya.

20Basi kama ninafanya kile nisichotaka kufanya, si mimi ninayekifanya, lakini ni ile zambi inayokaa ndani yangu.

21Basi ninatambua kanuni hii: wakati ninapotaka kufanya jambo jema, mara moja ninavutwa kufanya jambo baya.

22Ndani ya roho yangu ninapendezwa na Sheria ya Mungu,

23lakini ndani ya mwili wangu ninaona sheria ingine ikipigana na mafikiri yangu. Nayo inanifanya mufungwa wa sheria ya zambi inayotumika ndani ya mwili wangu.

24Ole kwangu, mimi mutu wa taabu! Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili huu unaokuwa wa kufa?

25Mungu ashukuriwe kwa ajili ya Bwana wetu Yesu Kristo!

Basi hivi kwa upande mumoja ninatumikia sheria ya Mungu kwa akili yangu, lakini kwa upande mwingine ninatumikia sheria ya zambi kwa hali yangu ya kimwili.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help