Waamuzi 11 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Kule Gileadi kulikuwa mupiganaji mumoja anayeitwa Yefuta, mwana wa mama mumoja kahaba, na baba yake aliitwa Gileadi.

2Gileadi alikuwa vilevile na wana wengine toka kwa muke wake. Watoto wa muke huyo walipokuwa wakubwa, wakamufukuza Yefuta kutoka kwao, wakamwambia: “Wewe hauna haki ya kupata urizi kutoka kwa baba yetu, maana wewe ni mutoto wa mwanamuke mwingine.”

3Basi, Yefuta akawakimbia wandugu zake akaenda kuishi katika inchi ya Tobu. Kule watu wa ovyo wakakusanyika kujiunga naye, wakamufuata katika safari zake za mashambulio.

4Nyuma ya muda fulani, Waamoni wakawashambulia Waisraeli.

5Wakati vita ilipopamba moto, wazee wa Gileadi wakaenda kumuleta Yefuta kutoka inchi ya Tobu,

6wakamwambia: “Kuja utuongoze katika vita yetu na Waamoni.”

7Lakini Yefuta akawaambia hao wazee wa Gileadi: “Si mulinichukia hata mukanifukuza kutoka kwa jamaa ya baba yangu? Kwa nini munanifikia sasa mukiwa katika taabu?”

8Hao wazee wa Gileadi wakamwambia: “Ndiyo maana tumekufikia kusudi uende nasi kupigana na Waamoni, nawe utakuwa kiongozi wetu na wa wakaaji wote wa Gileadi.”

9Yefuta akawaambia hao wazee wa Gileadi: “Kama mukinirudisha kwetu kwa kupigana na Waamoni halafu Yawe akiwatia katika mikono yangu, mimi nitakuwa kiongozi wenu.”

10Wale wazee wa Gileadi wakamwambia Yefuta: “Yawe atakuwa mushuhuda kati yetu. Hakika tutafanya kama ulivyosema.”

11Yefuta akafuatana na wazee wa Gileadi, nao watu wakamufanya kiongozi wao. Yefuta akasema masharti yake kule Misipa mbele ya Yawe.

12Yefuta akapeleka ujumbe kwa mufalme wa Amoni akamwambia: “Kuna maneno gani kati yako nasi hata ukuje kuishambulia inchi yetu?”

13Mufalme wa Amoni akawajibu hao wajumbe: “Waisraeli walipotoka Misri, walitwaa inchi yangu kutoka muto Arnoni mpaka kwenye muto Yaboki na muto Yordani. Sasa munirudishie inchi hiyo kwa amani.”

14Yefuta akatuma tena wajumbe kwa mufalme wa Amoni

15wamwambie kwa jina lake: “Waisraeli hawakutwaa inchi ya Wamoabu wala inchi ya Waamoni.

16Lakini Waisraeli walipotoka Misri, walisafiri katika jangwa mpaka kwenye bahari Nyekundu na kufika Kadesi.

17Kisha Waisraeli wakatuma wajumbe kwa mufalme wa Edomu wakimwomba awaruhusu kupita katika inchi yake, lakini mufalme wa Edomu akakataa. Basi wakamwomba mufalme wa Moabu ruhusa naye vilevile akakataa. Kwa hiyo Waisraeli wakabaki Kadesi.

18Kisha wakasafiri wakipitia katika jangwa kuzunguka inchi ya Edomu na Moabu mpaka walipofika upande wa mashariki wa Moabu, wakapiga kambi ngambo ya muto Arnoni. Lakini hawakuingia katika eneo la Moabu. Muto Arnoni ndio uliokuwa mupaka wa Moabu.

19Hapo Waisraeli wakatuma wajumbe kwa mufalme Sihoni wa Waamori kule Hesiboni, wakamwomba awaruhusu kupita katika inchi yake waende katika inchi yao.

20Lakini Sihoni hakuwakubali Waisraeli wapite katika inchi yake. Basi, Sihoni akakusanya watu wake wote, akapiga kambi kule Yahasa, akawashambulia Waisraeli.

21Naye Yawe, Mungu wa Israeli, akamutia Sihoni pamoja na watu wake katika mikono ya Waisraeli, wakawashinda. Hivyo Waisraeli wakatwaa inchi yote ya Waamori ambao walikuwa wanaishi kule.

22Walilitwaa eneo lote la Waamori tangu muto Arnoni mpaka kwenye muto Yaboki na tangu katika jangwa upande wa mashariki mpaka kwenye muto Yordani upande wa magaribi.

23Kwa hiyo, Yawe, Mungu wa Israeli, akawafukuza Waamori mbele ya Waisraeli. Sasa, wewe unataka kutunyanganya inchi yetu?

24Tosheka na kile ambacho mungu wako Kemosi amekupa. Lakini inchi yoyote ambayo Yawe, Mungu wetu, amewafukuza wakaaji wake, akatupa sisi, hiyo ni mali yetu sisi.

25Unazani wewe una nguvu kuliko Balaki mwana wa Sipori aliyekuwa mufalme wa Moabu? Yeye hakushindana na Waisraeli au kupigana nao.

26Wakati wote Waisraeli walipoishi katika muji wa Hesiboni na vijiji vyake, na muji wa Aroeri na vijiji vyake pamoja na miji yote inayokuwa kwa ukingo wa muto Arnoni kwa muda wa miaka mia tatu, kwa nini haukulikomboa eneo hilo wakati huo?

27Mimi sijakukosea kitu na ndiyo maana unafanya kosa unaponishambulia. Yawe ambaye ndiye Mwamuzi ataamua leo hii kati ya Waisraeli na watu wa Amoni.”

28Lakini mufalme wa Amoni akazarau ujumbe ule wa Yefuta.

29Kisha roho wa Yawe akamujaza Yefuta, naye akaondoka na kupitia Gileadi na Manase, akarudi Misipa katika inchi ya Gileadi na kuendelea mpaka Amoni.

30Yefuta akamwapia Yawe akisema: “Kama utawatia Waamoni katika mikono yangu,

31basi, yeyote atakayetoka inje kutoka katika nyumba yangu kuja kunipokea nitakapokuwa ninarudi nyuma ya kuwashinda Waamoni, huyo atakuwa wako wewe Yawe. Nitakutolea kama sadaka ya kuteketezwa.”

32Basi, Yefuta akavuka muto, akapigana na Waamoni, naye Yawe akawatia Waamoni katika mikono yake.

33Akajipatia ushindi mukubwa, akateka maeneo makumi mbili yaliyokuwa kati ya Aroeri, sehemu zilizozunguka Miniti na Abeli-Keramimu. Basi Waamoni wakashindwa kabisa na Waisraeli.

34Yefuta alipokuwa anarudi kwake kule Misipa, binti yake akatoka kuja kumupokea akicheza na kupiga matari. Binti huyo alikuwa ndiye mutoto wake wa pekee. Yefuta hakukuwa na mutoto mwingine mwanaume wala mwanamuke.

35Yefuta alipomwona, akapasua nguo yake kwa huzuni na kusema: “Ee binti yangu! Umenivunja moyo. Wewe umekuwa chanzo kikubwa cha matatizo kwangu. Nimekwisha kumwapia Yawe nami siwezi kuvunja kiapo changu.”

36Naye akamwambia: “Baba, kama umemwapia Yawe kitu, basi unitendee kama ulivyoahidi, kwa vile sasa amekuwezesha kuwalipiza kisasi waadui zako Waamoni.”

37Kisha, akamwambia baba yake: “Ninakuomba jambo hili moja, unipatie muda wa miezi miwili, niende na warafiki zangu kwenye milima, niomboleze kifo changu mbele ya kuolewa.”

38Baba yake akamuruhusu aende kule kwa miezi miwili. Naye akaenda pamoja na warafiki zake, wakaomboleza kufa kwake mbele ya kuolewa.

39Nyuma ya miezi miwili akarudi kwao. Kisha baba yake akamutendea kulingana na kiapo chake. Binti huyo hakukuwa amemujua mwanaume yeyote. Basi, tangu wakati ule kukakuwa desturi hii katika Israeli:

40Kila mwaka wanawake wa Israeli wanaenda kuomboleza kwa siku ine kifo cha binti ya Yefuta wa Gileadi.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help