1 Samweli 26 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Daudi anamuhurumia tena Saulo

1Wamoja kati ya wanaume kutoka muji wa Zifu wakamwendea Saulo kule Gibea, wakamwambia kwamba Daudi alikuwa anajificha kwenye mulima Hakila, upande wa mashariki wa Yesimoni.

2Mara moja, Saulo alikwenda kwenye jangwa la Zifu kumutafuta Daudi akiwa na waaskari waliochaguliwa elfu tatu wa Israeli.

3Saulo akapiga kambi juu ya mulima Hakila, karibu na barabara, upande wa mashariki wa Yesimoni. Lakini Daudi alikuwa angali kule katika jangwa. Daudi alipojua kwamba Saulo alikuwa amekuja katika jangwa kwa kumutafuta,

4alituma wapelelezi, akafahamishwa kwamba ni kweli.

5Daudi akatoka, akaenda pahali Saulo alipopiga kambi. Akaona pahali ambapo Saulo alikuwa amelala. Saulo alikuwa pamoja na Abeneri mwana wa Neri, mukubwa wa waaskari, katikati ya kambi akizungukwa na waaskari wake.

6Daudi akamwambia Ahimeleki ambaye alikuwa Muhiti, na Abisai ndugu ya Yoabu (mama yao aliitwa Zeruya): “Nani atakwenda pamoja nami kwenye kambi ya Saulo?”

Abisai akamwambia: “Mimi nitakwenda pamoja nawe.”

7Kwa hiyo usiku, Daudi na Abisai wakaingia kwenye kambi ya Saulo, wakamukuta Saulo amelala katikati ya kambi hiyo, na mukuki wake umechomekwa katika udongo karibu na kichwa chake. Abeneri pamoja na waaskari walikuwa wamelala na kumuzunguka Saulo.

8Abisai akamwambia Daudi: “Leo Mungu amemutia adui yako katika mikono yako. Basi, uniache nimushindilie katika udongo kwa pigo moja tu la mukuki. Sitamupiga mara mbili.”

9Lakini Daudi akamwambia Abisai: “Usimwangamize; maana nani anaweza kunyoosha mukono wake juu ya mutu ambaye ni muchaguliwa wa Yawe, naye asiazibiwe?

10Kama vile Yawe anavyoishi, Yawe mwenyewe atamwua, au siku yake ya kufa itamufikia au atakuja kwenda katika vita na kuangamizwa kule.

11Lakini Yawe anakataza nisinyooshe mukono wangu juu ya mutu ambaye ni muchaguliwa wa Yawe. Lakini twaa mukuki wake unaokuwa karibu na kichwa chake pamoja na mufuko wake wenye maji, halafu tujiendee zetu.”

12Kwa hiyo, Daudi alitwaa ule mukuki na mufuko wa maji karibu na kichwa cha Saulo nao wakajiendea zao. Lakini hakuna mutu aliyeona au kujua tukio hilo, wala hakuna aliyeamuka, maana Yawe aliwaletea usingizi muzito.

13Kisha, Daudi akaenda upande wa pili wa bonde hilo, akasimama juu kwenye mulima mbali na kundi la Saulo.

14Akawaita kwa sauti waaskari wa Saulo na Abeneri mwana wa Neri akisema: “Abeneri, unanisikia?”

Abeneri akauliza: “Wewe ni nani unayemwita mufalme?”

15Daudi akamujibu: “Wewe si mwanaume? Nani anayekuwa sawa nawe katika Israeli? Mbona basi, haukumulinda bwana wako mufalme? Mutu mumoja kati yetu aliingia pale kwa kumwangamiza bwana wako mufalme!

16Ulilotenda si jambo zuri. Kama vile Yawe anavyoishi, unastahili kufa, maana haukumulinda bwana wako, ambaye ni muchaguliwa wa Yawe. Sasa angalia, mukuki wa mufalme na ule mufuko wa maji uliokuwa karibu na kichwa chake kama vipo!”

17Saulo alitambua sauti ya Daudi, akamwuliza: “Hiyo ni sauti yako mwana wangu Daudi?”

Daudi akamujibu: “Bwana wangu mufalme, ni sauti yangu.”

18Halafu akaendelea kusema: “Lakini kwa nini, wewe bwana wangu unanifuatilia mimi mutumishi wako? Nimefanya nini? Ni uovu gani nimekufanyia?

19Basi, sasa bwana wangu mufalme, usikie maneno ya mutumishi wako. Ikiwa Yawe ndiye aliyekuchochea ukuje kunishambulia, basi, apokee sadaka ambayo itamusukuma kubadilisha mawazo yake. Lakini ikiwa ni watu, basi, Yawe awalaani watu hao maana wamenifukuza kutoka urizi ambao Yawe aliotupa wakisema: ‘Kwenda uitumikie miungu mingine.’

20Usiniache nikufe katika inchi ya kigeni, mbali na Yawe. Kwa nini wewe mufalme wa Israeli umetoka kuyatafuta maisha yangu kama mutu anayewinda kwale juu ya milima?”

21Halafu Saulo akajibu: “Mimi nimefanya makosa. Rudi mwana wangu Daudi. Sitakuzuru tena kwa sababu leo maisha yangu yalikuwa ya bei kali mbele yako. Mimi nimekuwa mupumbafu na nimekosa vibaya sana.”

22Daudi akajibu: “Ee mufalme, mukuki wako uko hapa, utume kijana wako mumoja akuje aukamate.

23Yawe anamulinda kila mutu kwa haki yake na uaminifu wake. Leo Yawe alikutia katika mikono yangu, lakini mimi sikunyoosha mukono wangu juu ya yule ambaye ni muchaguliwa wa Yawe.

24Angalia kama vile leo maisha yako yalivyokuwa na bei kali mbele yangu, ndivyo maisha yangu yapate kuwa na bei kali mbele ya Yawe; naye aniokoe kutoka taabu zote.”

25Saulo akamwambia Daudi: “Mungu akubariki mwana wangu Daudi. Utafanya mambo makubwa, nawe utafanikiwa katika yote.” Basi, Daudi akaenda zake; Saulo naye akarudi kwake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help