2 Wafalme 7 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Elisha akamujibu: “Sikiliza neno la Yawe: Kesho kwa wakati kama huu, humu Samaria kilo tatu za unga bora wa ngano zitanunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza.”

2Jemedari mulinzi wa mufalme akamwambia Elisha: “Hata kama Yawe mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, jambo hilo litawezekana?” Elisha akamujibu: “Utaona kwa macho yako mwenyewe, lakini wewe hautakula.”

Waaskari wa Aramu wanaondoka

3Kulikuwa watu wane wenye ugonjwa wa ukoma waliokuwa inje ya milango ya muji wa Samaria ambao walisemezana, wao kwa wao: “Mbona tunakaa hapa tukikufa na njaa?

4Hakuna maana ya kuingia katika muji kwa sababu kule tutakufa. Kwa hiyo kumbe tuende kwenye kambi ya Waaramu. Kama wakituacha kuishi, tutaishi; kama wakituua, tutakufa tu.”

5Hivyo, giza lilipoanza kuingia, wakaenda kwa kambi ya Waaramu, lakini walipofika kule, hakukuwa mutu.

6Maana Yawe alikuwa amewasikilizisha waaskari wa Waaramu sauti kama ya kundi kubwa lililokuwa na magari na farasi. Waaramu wakazani kwamba mufalme wa Israeli amelipa waaskari wa Wahiti na Wamisri kuja kuwashambulia.

7Basi, katika usiku ule, Waaramu walikimbia wote kwa kuyaokoa maisha yao wakiacha mahema yao, farasi na punda wao, na hata kambi yao jinsi ilivyokuwa.

8Wale watu wane wenye ukoma walipofika pembeni ya kambi, waliingia ndani ya hema moja, wakakula na kunywa vile walivyopata mule, wakatwaa feza, zahabu na nguo, wakaenda kuzificha. Wakaingia katika hema ingine na kufanya vivyo hivyo.

9Lakini wakaambiana: “Tunalofanya si sawa! Hii ni habari njema tunayokuwa nayo leo, na ikiwa tutangoja mpaka asubui, bila shaka tutaazibiwa. Tuende mara moja tuwaambie watu wa nyumba ya mufalme!”

10Hivyo, wakaondoka katika kambi ya Waaramu na kuwaita walinda milango ya muji na kuwaambia: “Tulikwenda katika kambi ya Waaramu na hatukuweza kumwona wala kumusikia mutu yeyote. Farasi na punda wangali wanafungwa, na mahema yako kama walivyoyaacha.”

11Walinda milango wakaita mutu mumoja kupasha habari hii katika nyumba ya mufalme.

12Ingawa kulikuwa bado giza, mufalme aliamuka na kuwaambia wakubwa wa waaskari wake: “Mimi ninajua mupango wa Waaramu! Wanajua tuna njaa katika muji. Sasa wameacha kambi yao kwenda kujificha kusudi tutakapokwenda kutafuta chakula, watukamate wote tungali wazima na kuuteka muji.”

13Mumoja kati ya wakubwa wake akasema: “Tafazali, utume watu wachache na farasi watano wa wale waliobaki kusudi waende kuona kumetokea nini. Matokeo yao hayatakuwa mabaya zaidi kuliko Waisraeli wote wanaoangamia hapa.”

14Wakachagua watu na kuwapa magari mawili. Mufalme akawatuma kuwafuata Waaramu, akisema: “Mwende muwaone.”

15Watu hao wakaenda mpaka Yordani na katika njia waliona nguo na vifaa vingine Waaramu walivyoacha walipokuwa wanakimbia. Wakarudi na kumupasha mufalme habari.

16Watu wa Samaria wakatoka na kuteka kambi ya Waaramu. Kama vile Yawe alivyosema, kilo tatu za unga bora wa ngano zilinunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza.

17Naye mufalme alikuwa amemuweka jemadari mulinzi wake kwa kulinda mulango wa muji. Jemadari yule alikanyagwa na watu palepale kwenye mulango, akakufa kama vile Elisha mutu wa Mungu alivyotabiri wakati mufalme alipokwenda kumwona.

18Elisha alikuwa amemwambia mufalme kwamba “Kesho kwa wakati kama huu, humu Samaria kilo tatu za unga bora wa ngano zitanunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza.”

19Yule jemedari mulinzi wa mufalme alikuwa amemwambia Elisha: “Hata kama Yawe mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, jambo hilo litawezekana?” Naye Elisha alikuwa amemujibu: “Utaona kwa macho yako mwenyewe, lakini wewe hautakula.”

20Na hivi ndivyo ilivyotokea: alikanyagwa na watu palepale kwenye mulango, akakufa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help