1 Samweli 30 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Vita na Waamaleki

1Kisha siku tatu, Daudi na watu wake wakarudi Ziklagi. Waamaleki walikuwa wamekwisha kushambulia Negebu pamoja na muji wa Ziklagi na kuuteketeza kwa moto.

2Walikuwa wameteka wanawake na watu wote waliokuwa katika muji, wakubwa kama vile wadogo. Hao waliowateka, waliondoka nao wakiwa wazima, bila kumwua mutu yeyote.

3Daudi na watu wake walipofika katika muji waliukuta muji umeteketezwa, na wanawake, watoto wao wanaume na wanawake wamekamatwa mateka.

4Halafu Daudi na watu wake wakaanza kulalamika, wakalia mpaka walipoishiwa nguvu.

5Wake wawili wa Daudi, Ahinoamu kutoka Yezereheli na Abigaili mujane wa Nabali, nao vilevile walikuwa wamekamatwa mateka.

6Sasa, Daudi alikuwa katika matatizo makubwa kwa sababu watu wake walikuwa na uchungu katika roho zao kwa kupoteza watoto wao. Kwa hiyo wakakuwa wakitaka kumupiga mawe. Lakini Daudi alijipa moyo kwa kumutegemea Yawe, Mungu wake.

7Daudi akamwambia kuhani Abiatari mwana wa Ahimeleki: “Uniletee kizibao cha kuhani.” Abiatari akamupelekea.

8Daudi akamwomba Yawe shauri: “Nikifuata kundi hili nitalikamata?”

Yawe akamujibu: “Ulifuate maana utalipata na kuwaokoa hao waliotekwa.”

9Kwa hiyo, Daudi akaondoka pamoja na wale watu mia sita aliokuwa nao. Walipofika kwenye kijito cha Besori, wakawakuta wamoja kati ya watu waliotekwa wameachwa pale.

10Lakini Daudi aliendelea kulifuatilia lile kundi akiwa na watu mia ine. Watu mia mbili wakabaki pale kwa sababu walichoka sana hata hawakuweza kuvuka kijito kile.

11Wale watu waliokuwa na Daudi walimukuta mutu mumoja Mumisri katika jangwa, nao wakamupeleka kwa Daudi. Wakamupa mutu yule mukate na maji.

12Vilevile walimupa kipande cha mukate wa tini na vishada viwili vya zabibu zenye kukauka. Alipomaliza kula, akapata nguvu, maana alikuwa hajakula wala kunywa kitu chochote kwa muda wa siku tatu, muchana na usiku.

13Daudi akamwuliza: “Bwana wako ni nani? Na umetoka wapi?”

Yeye akamwambia: “Mimi ni kijana Mumisri. Ni mutumishi wa Mwamaleki mumoja. Bwana wangu aliniacha nyuma siku tatu zilizopita kwa maana nilikuwa mugonjwa.

14Sisi tulishambulia Negebu ya Wakereti na eneo la Yuda pamoja na Negebu ya Kalebu. Muji wa Ziklagi tuliuteketeza kwa moto.”

15Daudi akamwuliza: “Utaweza kunipeleka kwenye kundi lile?”

Kijana akamujibu: “Ikiwa utaniapia kwa jina la Mungu kwamba hautaniua, wala kunitia katika mikono ya bwana wangu, nitakupeleka.”

16Yule kijana alimwongoza Daudi mpaka kwenye kundi lile. Walipofika kule waliwakuta wanyanganyi wale wakiwa wametawanyika kila pahali maana walikuwa wakikula na kunywa kwa sababu vitu walivyonyanganya kutoka inchi ya Wafilistini na inchi ya Yuda vilikuwa vingi sana.

17Daudi aliwapiga tangu asubui mpaka siku ya pili magaribi. Hakuna mwanaume yeyote aliyeponyoka isipokuwa vijana mia ine ambao walipanda juu ya ngamia na kukimbia.

18Daudi aliokoa kila kitu Waamaleki walichokuwa wameteka, hata na wake zake wawili.

19Chochote kilichokuwa chao, kikuwe kikubwa au kidogo, mutoto mwanaume au mwanamuke, Daudi alikikomboa.

20Vilevile Daudi aliteka makundi yote ya kondoo na ngombe, na watu walioongoza nyama wale walisema: “Hivi ni vitu vya Daudi.”

21Daudi akawarudilia wale watu mia mbili ambao waliachwa kwenye kijito cha Besori kwa sababu walikuwa wamechoka kwa kumufuata. Wale watu walipomwona Daudi pamoja na wale waliokuwa pamoja naye, wakaenda kumupokea. Daudi alipofika karibu na watu hao, akawasalimia.

22Lakini watu wote waovu na wa ovyo ovyo kati ya watu waliofuatana na Daudi, wakasema: “Hatutawapa watu hawa kitu chochote tulichokikomboa maana hawakuendelea pamoja nasi. Lakini wawatwae wake zao na watoto wao, waende zao.”

23Daudi akawaambia: “Sivyo wandugu zangu. Hamuwezi kufanya vile kwa kile ambacho Yawe ametupatia. Alitulinda salama, na akalitia katika mikono yetu kundi lililokuja kutushambulia.

24Hakuna mutu atakayekubaliana na mawazo yenu! Yule aliyekwenda katika vita na yule aliyebaki na mizigo yetu, kila mutu atapewa sehemu inayolingana na ya mwenzake.”

25Tangu siku ile Daudi alifanya uamuzi ule kuwa sharti na agizo katika inchi ya Israeli mpaka hivi leo.

26Daudi aliporudia Ziklagi, aliwapelekea warafiki zake ambao ni wazee wa Yuda sehemu ya vitu akisema: “Ninawaletea zawadi kutoka katika vitu vya waadui wa Yawe.”

27Zawadi hizo zilikuwa kwa ajili ya wakaaji wa Beteli, wakaaji wa Ramoti katika Negebu, wakaaji wa Yatiri,

28wakaaji wa Aroeri, wakaaji wa Sifumoti, wakaaji wa Estemoa,

29wakaaji wa Rakali, wakaaji wa miji ya Wayerameli, wakaaji wa miji ya Wakeni,

30wakaaji wa Horma, wakaaji wa Borasani, wakaaji wa Ataki,

31na wakaaji wa Hebroni. Daudi aliwapelekea vilevile wakaaji wa miji yote ambako yeye na watu wake walitembelea.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help