Matayo 23 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maonyo juu ya Wafarisayo(Mk 12.38-39; Lk 11.43,46; 20.45-46)

1Halafu Yesu akawaambia makundi ya watu na wanafunzi wake:

2“Walimu wa Sheria na Wafarisayo wamepewa madaraka ya kueleza Sheria ya Musa.

3Basi kwa hiyo munapaswa kuwatii na kushika maneno yote wanayowaambia; lakini musifuate matendo yao, kwa maana mambo wanayoyasema, si ndiyo wanayofanya.

4Wanafunga mizigo mizito na kuibebesha watu wengine kwa mabega, lakini wao wenyewe hawafikiri hata kidogo juu ya namna ya kuwasaidia kuibeba.

5Wanafanya matendo yao yote tu kusudi wajionyeshe mbele ya watu. Wanajifungia kwa paji za nyuso vibweta vipana vyenye vikaratasi vya Maandiko Matakatifu. Nao wanavaa kanzu zenye pembe ndefu.

6Wanapenda kuikaa kwenye nafasi za heshima katika karamu na katika viti vya mbele ndani ya nyumba za kuabudia.

7Wanapenda vilevile kusalimiwa kwa heshima kwenye nafasi za makutano, na kuitwa ‘Mwalimu.’

8Lakini ninyi musikubali kuitwa ‘Mwalimu’, kwa maana ninyi wote ni wandugu, nanyi muko na Mwalimu mumoja tu.

9Vilevile hapa katika dunia musimwite mutu yeyote ‘Baba’ kwa maana muko na Baba mumoja tu, anayekuwa mbinguni.

10Musikubali kuitwa ‘Waongozi,’ kwa maana muko na Mwongozi Mukubwa mumoja tu, ndiye Kristo.

11Lakini anayekuwa mukubwa kati yenu sherti akuwe mutumishi wenu.

12Na yeyote anayejiinua, atashushwa, lakini anayejishusha, atainuliwa.

Udanganyifu wa Wafarisayo na walimu wa Sheria(Mk 12.40; Lk 11.39-42,44,52; 20.47)

13“Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munawafungia watu wengine njia ya kuingia katika Ufalme wa mbinguni. Ninyi wenyewe hamwingii mule na zaidi ya hii munawazuiza wale wanaotaka kuingia.

[

14“Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munanyanganya mali za wajane na kuomba maombi marefu kwa kujionyesha. Kwa sababu hii azabu yenu itakuwa kubwa zaidi!]

15“Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munasafiri kuvuka bahari na inchi mbalimbali kusudi mupate kumugeuza hata mutu mumoja tu kuwa mufuasi wenu. Nanyi munapomupata, munamufanya kuwa mwenye kustahili azabu ya jehenamu mara mbili zaidi kuliko ninyi.

16“Ole kwenu, ninyi waongozi vipofu! Ninyi munaosema kwamba mutu akiapa kwa jina la hekalu, si kitu; lakini kama akiapa akitaja zahabu inayokuwa ndani ya hekalu, anapaswa kutimiza kiapo chake.

17Ninyi wapumbafu na vipofu! Ni nini inayokuwa kubwa zaidi, zahabu au hekalu linaloifanya zahabu ile ihesabiwe kuwa takatifu?

18Munasema vilevile kwamba mutu akiapa akitaja mazabahu, si kitu; lakini kama akiapa akitaja sadaka inayokuwa juu yake, anapaswa kutimiza kiapo chake.

19Ninyi vipofu! Ni nini inayokuwa kubwa zaidi, sadaka au mazabahu ndiyo inayoifanya sadaka ile ihesabiwe kuwa takatifu?

20Katika haya yote mutu anayeapa kwa jina la mazabahu anaapa kwa jina lile na kwa majina ya vyote vinavyokuwa juu yake.

21Vilevile anayeapa kwa jina la hekalu anaapa kwa jina lile na kwa jina la Mungu anayekuwa ndani yake.

22Naye anayeapa kwa jina la mbingu anaapa kwa jina la kiti cha kifalme cha Mungu na kwa jina la Mungu anayeikaa juu yake.

23“Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munatoa fungu moja la kumi la vijani vya kukoleza chakula, lakini mumeacha mambo makubwa yanayoamuriwa na Sheria, kama vile haki, huruma, na uaminifu. Mambo hayo ndiyo muliyopaswa kushika pasipo kuacha mengine.

24Ninyi waongozi vipofu! Munapokunywa, munachuya inzi toka katika vinywaji vyenu, lakini munameza ngamia!

25“Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Ninyi ni kama mutu anayesafisha tu inje ya kikombe na sahani, lakini ndani kumejaa vitu mulivyovipata kwa njia ya wizi na tamaa mbaya.

26Wewe kipofu Mufarisayo! Safisha kwanza ndani ya kikombe na ya sahani, na kisha inje yake kutakuwa safi vilevile.

27“Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munafanana na makaburi yaliyopakaliwa chokaa, yanayoonekana kuwa mazuri kwa inje, lakini ndani yanajaa mifupa ya wafu na uchafu wa kila namna.

28Ni vile ninyi munavyokuwa, kwa inje munaonekana kuwa wenye haki mbele ya watu, lakini ndani yenu munajaa unafiki na uovu.

Azabu ya Wafarisayo na walimu wa Sheria(Lk 11.47-51)

29“Ole kwenu, ninyi walimu wa Sheria na Wafarisayo, ninyi wanafiki! Munajenga makaburi ya manabii na kupamba makaburi ya watu waliokuwa wema.

30Nanyi munasema: ‘Kama sisi tungaliishi katika nyakati za babu zetu, hatungalijiunga nao katika shauri la kuwaua manabii.’

31Hivi munajishuhudia ninyi wenyewe kuwa ninyi ni ukoo wa watu waliowaua manabii.

32Basi mutimize hayo mambo babu zenu waliyoyaanza!

33Ninyi kikundi cha nyoka! Namna gani mutaweza kuepuka azabu ya jehenamu?

34Kwa sababu hiyo, nitawatumia manabii na watu wenye hekima na walimu. Mutawaua wamoja wao, mutatundika wengine juu ya misalaba, mutawapiga wengine fimbo ndani ya nyumba zenu za kuabudia na kuwafukuza muji kwa muji.

35Na hivi mutabeba lazima ya damu iliyomwangwa katika dunia pasipo kosa, tangia kuuawa kwa Abeli aliyekuwa mukamilifu mpaka kuuawa kwa Zakaria, mwana wa Barakia, muliyemwuia kwenye hekalu katikati ya Pahali Patakatifu na mazabahu.

36Kweli ninawaambia: watu wa kizazi hiki watabeba lazima ya mambo hayo yote.

Yesu analilia Yerusalem(Lk 13.34-35)

37“Ewe Yerusalema, Ewe Yerusalema. Wewe unaua manabii na kuwatupia mawe wale ambao Mungu anakutumia. Mara nyingi nilitaka kuwakusanya wakaaji wako kama vile kuku anavyokusanya vitoto vyake chini ya mabawa yake, lakini ninyi hamukutaka!

38Angalia, makao yenu yanaachwa ukiwa.

39Kwa maana ninawaambia, tangia sasa hamutaniona tena mpaka mutakaposema: ‘Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana.’ ”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help