Amosi 6 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Azabu kwa sababu ya kujiaminia

1Ole kwenu ninyi munaostarehe kule Sayuni,

nanyi munaoishi katika usalama kwenye mulima Samaria!

Ninyi munaonekana kuwa waongozi wa taifa kubwa,

ambao Waisraeli wote wanawategemea.

2Muende Kalne, muangalie.

Tokea kule muende mpaka katika ule muji mukubwa wa Hamati,

kisha mutelemuke mpaka Gati kwa Wafilistini.

Mutatambua kwamba ninyi si bora kuliko falme zile,

hata kama eneo lao ni ndogo zaidi ya lenu.

3Ninyi munajaribu kuifukuza ile siku mbaya.

Lakini munaukaribisha utawala wa mateso.

4Ole kwenu ninyi munaolalia juu ya vitanda vya pembe za tembo

na kujinyoosha juu ya matandiko yao,

mukikula nyama za wana-kondoo na wana-ngombe!

5Ninyi munapenda kuimba ovyo na sauti ya vinubi

na kutunga ala mupya za muziki mukimwiga mufalme Daudi.

6Munakunywa divai katika mabakuli,

na kujipakaa marasi mazuri kabisa.

Lakini hamuhuzuniki hata kidogo

juu ya kuangamia kwa wazao wa Yosefu.

7Kwa hiyo mutakuwa wa kwanza kwenda katika uhamisho,

na karamu za wenye kustarehe zitatoweka.

8Bwana wetu Yawe ameapa kwa nafsi yake:

Ninachukizwa sana na kiburi cha wazao wa Yakobo;

tena ninachukia nyumba zao nzuri sana.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Muji wao na vyote vinavyokuwa ndani yake nitavipatia waadui zake.

9Kama wakibaki watu kumi katika nyumba moja, wote watakufa.

10Na mujomba wa yule aliyekufa atakapokuja kuitoa maiti inje aichome, akimwuliza yeyote atakayekuwa ndani pembeni ya nyumba: Kuna mutu mwingine pamoja nawe? Atajibiwa: Hakuna! Naye atamwambia: Nyamaza kimya! Tusilitaje hata jina la Yawe.

11Yawe anatoa amri,

na nyumba kubwa inabomoka vipandevipande,

na nyumba ndogo kusagikasagika.

12Farasi wanaweza kukimbia katika mawe makubwa?

Watu wanaweza kulima bahari na ngombe?

Lakini ninyi mumeigeuza sheria kuwa sumu,

na tunda la haki kuwa uchungu.

13Ninyi munashangilia juu ya muji wa Bure

na kusema mumeuteka muji wa Nguvu kwa nguvu zenu wenyewe.

14Enyi Waisraeli,

kweli nitaleta taifa moja likuje kuwashambulia.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Nalo litawatesa ninyi kuanzia Hamati upande wa kaskazini,

mpaka kwenye kijito cha Araba, upande wa kusini.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help