1Mungu wenu anasema hivi:
Muwafariji watu wangu.
Muende kuwafariji.
2Museme na watu wa Yerusalema kwa upole,
muwaambie kwamba utumwa wao umekwisha,
wamesamehewa uovu wao.
Yawe amewaazibu mara mbili
kwa sababu ya zambi zao zote.
3Sauti inatangaza katika jangwa:
Mutengenezee Yawe njia,
munyooshe barabara kubwa kwa ajili ya Mungu wetu.
4Kila bonde litafunikwa,
kila mulima na kilima vitasawanishwa;
njia zenye lukumba zitanyooshwa,
nazo zenye mashimo zitalainishwa.
5Kisha utukufu wa Yawe utafunuliwa,
na watu wote pamoja watauona.
Maneno haya yanatoka katika kinywa cha Yawe.
6Sauti inasema: Tangaza!
Nami nikauliza: Nitangaze nini?
Naye: Tangaza: wanadamu wote ni kama majani;
usitawi wao ni kama maua ya shamba.
7Majani yananyauka na maua yanafifia,
Yawe anapovumisha upepo juu yake.
Hakika wanadamu ni kama majani.
8Majani yananyauka na maua yanafifia,
lakini neno la Mungu wetu linadumu milele.
9Kwenda juu ya mulima murefu,
ewe Sayuni, utangaze habari njema.
Lalamika kwa nguvu,
ewe Yerusalema, utangaze habari njema.
Lalamika bila kuogopa.
Uambie miji ya Yuda:
Muangalie: Mungu wenu!
10Bwana wetu Yawe anakuja na nguvu,
kwa mukono wake anatawala.
Yeye anakuja na mapato yake,
anafika na mushahara wake.
11Atachunga kundi lake kama muchungaji,
atawakusanya wana-kondoo katika mikono yake,
atawabeba kwa kifua chake,
na atawaongoza polepole kondoo wanaonyonyesha. Mungu wa Israeli hana kilinganisho
12Ni nani anayeweza kupima maji ya bahari katika kitanga cha mukono wake,
na kuzipima mbingu kwa mikono yake?
Ni nani anayeweza kuutia udongo wa dunia katika kikombe;
kuipima milima kwa mizani
au vilima kwa kipimo cha uzito?
13Nani anayeweza kuiongoza akili ya Yawe,
au kuwa mushauri wake na kumufundisha?
14Yawe alitaka shauri toka kwa nani,
halafu akapata kuwa mwenye akili?
Nani aliyemufundisha kuhukumu kwa haki?
Nani aliyemufundisha maarifa,
na kumwonyesha namna ya kuwa na akili?
15Kwake mataifa ni kama tone la maji katika mbeketi,
ni kama mavumbi juu ya kilo.
Kwake visanga ni vyepesi kama mavumbi laini.
16Kuni zote za Lebanoni
na nyama wake wote
havitoshi kwa sadaka ya kuteketezwa mbele yake.
17Mataifa yote si kitu mbele yake;
kwake ni vitu vya ovyo na bure kabisa.
18Mutamulinganisha Mungu na nini basi,
au ni kitu gani cha kumufananisha nacho?
19Anafanana na sanamu?
Hiyo, fundi anaichonga,
mufuaji wa zahabu anaipakaa zahabu,
na kuitengenezea mukufu wa feza!
20Au ni sanamu ya muti mugumu?
Hiyo ni kuni mutu anayochagua,
akamutafuta fundi anayeelewa kazi,
naye anamuchongea sanamu imara!
21Ninyi hamujui bado?
Hamujapata kusikia?
Hamukuambiwa tangu mwanzo?
Hamujafahamu mwanzo wa dunia?
22Dunia iliumbwa na yule anayeikaa juu ya mbingu;
kutoka huko wakaaji wa dunia ni kama mapanzi!
Yeye ametandika mbingu kama pazia,
na kuzikunjua kama hema la kuishi ndani yake.
23Yeye anawashusha wakubwa wenye nguvu,
anawafanya watawala wa dunia kuwa si kitu.
24Mara tu wanaposimikwa na kuanza kuota,
hata mbele hawajatoa mizizi kama miti katika udongo,
Yawe akiwapulizia wananyauka,
upepo mukali unawapeperusha kama makapi!
25Mungu Mutakatifu anauliza hivi:
Basi, mutanilinganisha na nani?
Kuna mutu anayeweza kuwa sawasawa mimi?
26Muinue macho yenu juu mbinguni!
Ni nani aliyeziumba nyota hizo?
Ni yule anayeziongoza kama jeshi lake,
anayeijua hesabu yake yote,
anayeziita kila moja kwa jina lake.
Kwa sababu yeye ni mwenye nguvu nyingi,
hakuna hata moja inayokosekana.
27Enyi watu wa Israeli wazao wa Yakobo,
kwa nini munalalamika na kusema:
Yawe hatujali sisi!
Mungu wetu hajali haki yetu!
28Ninyi hamujui bado?
Hamujapata kusikia?
Yawe ndiye Mungu wa milele;
yeye ndiye Muumba wa kila kitu katika dunia.
Yeye haregei hata kidogo wala kuchoka.
Maarifa yake hayachunguziki.
29Yeye anawapatia nguvu wanaokuwa zaifu,
anawaongezea nguvu wale wanaoregea.
30Hata vijana wataregea na kuchoka;
kweli washujaa wataanguka kwa muchoko.
31Lakini wote wanaomutumainia Yawe,
watapata nguvu mupya.
Watapanda juu kwa mabawa kama tai,
watakimbia bila kuchoka,
watatembea bila kuregea.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.