1Katika mwezi wa Nisani, kwa mwaka wa makumi mbili wa utawala wa mufalme Artasasta, wakati divai ilipokuwa mbele yake, nilitwaa divai na kumupatia mufalme. Mpaka sasa nilikuwa sijapata kuwa na huzuni mbele yake.
2Mufalme Artasasta akaniuliza: “Mbona unaonekana kuwa mwenye huzuni, ingawa hauonekani kuwa mugonjwa? Ninaona una huzuni sana ndani ya moyo wako!” Halafu nikaogopa sana.
3Nikamujibu: “Ee mufalme, uishi milele! Kwa nini nisikuwe mwenye huzuni wakati Yerusalema ambamo makaburi ya babu zangu uko tupu na milango yake imeteketezwa kwa moto?” Ang. 2 Fal 25.8-10; 2 Sik 36.19; Yer 52.12-14
4Halafu mufalme Artasasta akanijibu: “Sasa unaomba nini?” Nikamwomba Mungu wa mbinguni.
5Halafu nikamwambia mufalme: “Ee mufalme, ikikupendeza na ikiwa nimepata kukubaliwa mbele yako, ninakuomba unitume katika inchi ya Yuda kusudi niende kuujenga upya muji ambamo muko makaburi ya babu zangu.”
6Mufalme akaniuliza (malkia akiwa karibu naye): “Utakuwa kule kwa muda gani na utarudi hapa wakati gani?” Ombi langu akalikubali nami nikamujulisha wakati nitakaporudi.
7Nikamujibu: “Ee mufalme, ikikupendeza, ninaomba nipewe barua kusudi nizipeleke kwa watawala wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati kusudi waniruhusu nipite mpaka katika inchi ya Yuda.
8Vilevile ninakuomba kwamba barua ingine iandikwe kwa Asafu mulinzi wa pori la kifalme kusudi anipatie mbao za kutengeneza miimo ya milango ya munara wa hekalu, ukuta wa muji na nyumba yangu nitakamokaa.” Mufalme akakubali ombi langu kwa kuwa Mungu, kwa wema wake, alikuwa pamoja nami.
9Nilipowafikia wakubwa wa jimbo la upande wa magaribi wa muto Furati, nikawapa barua za mufalme. Mufalme alikuwa amenituma pamoja na wakubwa wa waaskari na waaskari wapanda-farasi.
10Lakini Sanibalati wa muji wa Muhori na Tobia, Mwamoni, mutumishi wake, waliposikia kwamba nimekuja kwa kushugulikia hali njema ya watu wa Israeli, hawakufurahia kabisa jambo hilo.
11Hivyo nikafika Yerusalema, nikakaa kule kwa siku tatu.
12Kisha nikaondoka usiku, mimi pamoja na watu wachache; sikumwambia mutu yeyote yale ambayo Mungu alikuwa ameyaweka ndani ya moyo wangu kwa ajili ya Yerusalema. Lakini siku moja usiku, nikaondoka na kutwaa watu wachache tu. Sikupeleka nyama yeyote isipokuwa punda niliyepanda juu yake mimi mwenyewe.
13Nikatoka nikipitia kwenye Mulango wa Bonde katika njia inayoelekea kwenye Kisima cha Joka na mulango wa Yalala; nikachunguza kuta za muji wa Yerusalema ambazo zilikuwa zimebomolewa pamoja na milango yake ambayo ilikuwa imeteketezwa kwa moto.
14Halafu, nikaenda kwenye Mulango wa Chemichemi na kwenye Ziwa la Mufalme. Lakini yule punda niliyepanda juu yake hakuweza kupita.
15Wakati ule wa usiku, nikapitia katika bonde na kuchunguza ukuta wa muji. Nikarudi nikipitia kwa Mulango wa Bonde.
16Wakubwa hawakujua pahali nilipokuwa nimekwenda wala nimefanya nini. Tena nilikuwa sijawaambia Wayuda, makuhani, viongozi, wakubwa wala wale watu ambao wangefanya kazi ya kujenga upya muji.
17Kisha nikawaambia: “Bila shaka munaona magumu yetu kwamba muji wa Yerusalema ni mabomoko na milango yake imeteketezwa kwa moto. Basi, tujenge tena ukuta wa Yerusalema kusudi tusifezeheshwe zaidi.”
18Nikawaelezea jinsi Mungu alivyokuwa pamoja nami akinitendea kwa wema wake. Nikawaelezea vilevile maneno ambayo mufalme alikuwa ameniambia. Wao waliposikia hayo, wakasema: “Sasa, na tuanze kazi ya ujenzi.” Hivyo wakajitayarisha kwa kazi hiyo njema.
19Lakini Sanibalati, Muhori, Tobia, Mwamoni mutumishi wake, na Gesemi, Mwarabu, waliposikia hayo, wakatucheka na kutuzomea wakisema: “Ni kitu gani hiki munachotenda? Munataka kumwasi mufalme?”
20Nikawajibu: “Mungu wa mbinguni atatufanikisha katika kazi hii, nasi tunaokuwa watumishi wake tutaanza kujenga. Lakini ninyi hamuna sehemu au haki wala ukumbusho katika Yerusalema.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.