1Wakati ule, Hezekia aligonjwa sana karibu kufa. Halafu nabii Isaya mwana wa Amozi akamwendea, akamwambia:
Yawe anasema hivi: Panga mambo yako sawasawa katika nyumba yako kwa sababu utakufa, hautapona.
2Hezekia akageukia upande wa ukuta na kumwomba Yawe,
3akisema: Ee Yawe, ninakusihi ukumbuke jinsi nilivyokutumikia kwa uaminifu na kwa moyo wangu wote, na kutenda mazuri mbele yako. Hezekia akalia kwa uchungu sana.
4Kisha neno la Yawe lilimufikia Isaya kusema hivi:
5Kwenda umwambie Hezekia kwamba:
Mungu wa baba yako Daudi, anasema hivi: Nimesikia ombi lako na nimeyaona machozi yako. Basi, ninakuongezea miaka kumi na mitano ya kuishi.
6Nitakuokoa wewe pamoja na muji huu toka katika mikono ya mufalme wa Asuria na kuulinda.
7Isaya akamujibu: Hiki kitakuwa kitambulisho kwako kutoka kwa Yawe kwamba Yawe atafanya kama alivyoahidi.
8Nitafanya kivuli kwenye daraja iliyojengwa na Ahazi, kirudi nyuma hatua kumi. Nacho kivuli kikarudi nyuma hatua kumi.
9Kisha mufalme Hezekia alipopona, akatunga wimbo huu wa shukrani:
10Nilisema: nikiwa mubichi kabisa,
inanipasa niage dunia.
Mimi nimepangiwa kwenda katika kuzimu
siku zote zilizonibakilia.
11Nilisema sitamwona tena Yawe,
katika inchi ya wanaokuwa wazima;
wala sitamwona mutu yeyote tena,
kati ya wakaaji wa ulimwengu.
12Makao yangu yameongolewa kwangu;
kama hema la muchungaji;
kama, mufumaji nimefika kwa mwisho wa kizingo cha maisha yangu;
Mungu amekata nyuzi zinazokishika;
hata mbele ya mwisho wa siku amenikomesha.
13Usiku kucha nililia kwa kuomba musaada;
kama simba, anavunjavunja mifupa yangu;
muchana na usiku ananikomesha.
14Ninalia kama mbaruwayi,
ninaugua kama njiwa.
Macho yangu yamefifia kwa kuangalia juu.
Ee Bwana, ninateseka;
ukuwe wewe usalama wangu!
15Lakini niseme nini:
yeye mwenyewe aliniambia,
naye mwenyewe ametenda hayo.
Usingizi wangu wote umenitoroka
kwa sababu ya uchungu ndani ya moyo wangu.
16Ee Bwana, sisi tunaishi kutokana na yote uliyotenda,
kwa hayo yote mimi peke yangu vilevile ninaishi.
Unirudishie afya, uniwezeshe kuishi.
17Nilipata mateso makali kwa faida yangu;
lakini umeyaokoa maisha yangu
kutoka shimo la uharibifu,
maana umezitupa zambi zangu nyuma yako.
18Huko kuzimu mutu hawezi kukushukuru wewe;
waliokufa hawawezi kukushukuru wewe.
Wala wanaoshuka kule katika shimo
hawawezi tena kutumainia uaminifu wako.
19Wanaokuwa wazima ndio wanaokushukuru,
kama na mimi ninavyofanya leo.
Wababa wanajulisha watoto wao uaminifu wako.
20Yawe ataniokoa.
Nasi tutamusifu kwa nyimbo za vinubi
siku zote za maisha yetu,
katika nyumba ya Yawe.
21Isaya alikuwa amesema: Mutwae mukate wa tini na kuuweka kwenye jipu lake, apate kupona.
22Hezekia akauliza: Ni kitambulisho gani kitakachonijulisha kwamba mimi nitakwenda kwa nyumba ya Yawe?
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.