Hesabu 6 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maagizo juu ya kufanya kiapo

1Yawe akamwambia Musa:

2Uwape Waisraeli maagizo haya: Ikiwa mwanaume au mwanamuke atafanya kiapo kuwa munaziri, ni kusema kujitenga kwa ajili ya Yawe,

3basi, asikunywe divai au kileo, asikunywe siki ya divai au ya namna nyingine, asikunywe maji ya zabibu wala kula zabibu zilizoiva au kavu. Ang. Lk 1.15

4Muda wote atakaokuwa munaziri asikule kitu chochote kinachotokana na muzabibu, tangu kokwa hata maganda yake.

5Siku zote za kiapo chake cha kujitenga, hatanyoa nywele zake. Mpaka muda wa kiapo chake cha kujitakasa kwa Yawe utakapomalizika, atakuwa mutakatifu, ataacha nywele zake zikuwe ndefu.

6Siku zote atakazokuwa amejitakasa kwa Yawe, mutu huyo asikaribie maiti,

7hata kama ni ya baba, mama, ndugu au dada yake, kusudi asijichafue kwa maana amejitakasa kwa Yawe kwa kiapo.

8Muda wote atakaokuwa munaziri atakuwa mutakatifu kwa Yawe.

9Kama mutu anakufa kwa rafla karibu na munaziri na kuchafua nywele zake, huyu munaziri atanyoa kichwa chake wakati wa siku ya kutakaswa kwake; atakinyoa katika siku ya saba.

10Katika siku ya nane atapeleka hua wawili au vitoto viwili vya njiwa kwa kuhani kwenye mulango wa hema la mukutano.

11Kuhani atamutoa mumoja kuwa sadaka kwa ajili ya zambi na mwingine kuwa sadaka ya kuteketezwa, naye atamufanyia ibada ya upatanisho, kwa sababu alitenda zambi kwa sababu ya maiti. Siku hiyohiyo atatakasa kichwa chake

12na kujitakasa kwa Yawe kwa siku zake za kujitenga. Hizo siku za kwanza hazitahesabiwa kwa sababu nywele zake zilizokuwa zimetakaswa zimechafuka. Atatoa mwana-kondoo dume wa mwaka mumoja kuwa sadaka ya kosa.

13Hii ndiyo sheria ya munaziri wakati akisha kamilisha muda wake wa kujitakasa: Ataletwa kwenye mulango wa hema la mukutano, Ang. Mdo 21.23-24

14na kumutolea Yawe zawadi zake: mwana-kondoo dume mumoja wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa; mwana-kondoo dike mumoja wa mwaka mumoja asiyekuwa na kilema kwa ajili ya sadaka ya zambi; na kondoo dume mumoja asiyekuwa na kilema kwa ajili ya sadaka ya amani.

15Vilevile atatoa kikapu cha mikate isiyotiwa chachu: maandazi ya unga laini na mafuta, na mikate myembamba iliyopakwa mafuta pamoja na sadaka za vyakula na za kinywaji.

16Kuhani atamutolea Yawe vitu vyote hivi pamoja na sadaka yake ya zambi na sadaka yake ya kuteketezwa.

17Atamutolea Yawe huyo kondoo kama sadaka ya amani, atamutoa pamoja na kikapu cha mikate isiyotiwa chachu, sadaka ya vyakula na ya kinywaji.

18Hapo kwenye mulango wa hema la mukutano, munaziri huyo atanyoa nywele zake na kuzitia katika moto unaokuwa chini ya sadaka ya amani.

19Kisha kuhani atatwaa bega la yule kondoo dume likiwa limepikwa pamoja na andazi moja lililotiwa chachu kutoka kikapu na mikate myembamba vilevile isiyotiwa chachu na kumupa munaziri katika mikono akisha kumaliza kunyoa nywele zake alizokuwa nazo wakati wa kutakaswa.

20Halafu kuhani atavitikisa vitu hivyo kama sadaka ya kutikisa mbele ya Yawe; vyote hivi ni sehemu takatifu kwa kuhani, pamoja na kilali kilichotikiswa na paja lililotolewa kama sadaka. Nyuma ya hayo yote, munaziri anaweza kunywa divai.

21Hiyo ndiyo sheria inayoelekea munaziri anayeahidi kwa kiapo. Sadaka yake kwa Yawe ilingane na kiapo chake, zaidi ya kitu chochote kingine anachoweza kutoa; atafanya kulingana na kiapo alichoweka, kadiri ya sheria ya kujitakasa kwake.

Baraka ya makuhani

22Yawe akamwambia Musa:

23Uwambie Haruni na wana wake kwamba hivi ndivyo mutakavyowabariki Waisraeli: Mutawaambia:

24Yawe awabariki na kuwalinda;

25Yawe awaangalie kwa wema, na kuwatendea mema;

26Yawe awaonyeshe wema wake na kuwapa amani.

27Ndivyo watakavyotamka jina langu juu ya Waisraeli, nami nitawabariki.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help