1Paulo akafika Derbe na Listra, ambako kulikuwa mwanafunzi mumoja aliyeitwa Timoteo. Mama yake alikuwa Muyuda, naye alikuwa ameamini lakini baba yake alikuwa Mugriki.
2Nao wandugu waamini wa Listra na wa muji Ikonio walitoa ushuhuda muzuri juu ya Timoteo.
3Paulo alitaka Timoteo amusindikize katika safari zake. Kwa hiyo akamutahiri kwa sababu ya Wayuda waliokaa katika pande zile, kwa maana wote walijua kwamba baba yake alikuwa Mugriki.
4Na katika miji yote ambamo walipita walitangaza kwa wanafunzi yale maagizo yaliyotolewa na mitume na wazee wa kanisa la Yerusalema, wakiwaomba wayashike.
5Hivi makanisa yakaendelea kukomaa katika imani, nayo hesabu ya wanafunzi iliongezeka siku kwa siku.
Paulo anapata maono katika Troa6Paulo na wale waliomusindikiza wakapita katika inchi ya Furigia na ya Galatia kwa sababu Roho Mutakatifu alikuwa amewakataza wasihubiri Neno la Mungu katika jimbo la Azia.
7Nao walipofika katika wilaya ya Misia, wakajaribu kwenda katika jimbo la Bitinia, lakini Roho wa Yesu hakuwaruhusu.
8Kwa hiyo wakapita Misia, wakatelemuka mpaka wakafika katika muji Troa.
9Na ilipokuwa usiku akapata maono. Akaona mutu mumoja wa inchi ya Makedonia akisimama mbele yake akimusihi akisema: “Vuka, ufike kwetu Makedonia, utusaidie.”
10Na pale pale kisha kupata maono yale, tukajitayarisha kwenda Makedonia, kwa maana tulitambua hakika kwamba Mungu alituita kwenda kuhubiri Habari Njema kule.
Ludia anamwamini Bwana11Basi tukasafiri ndani ya chombo kutoka Troa na kwenda mara moja mpaka Samotirake, na kesho yake tukafika Neapoli.
12Kutoka kule tukafika mpaka Filipi, muji mukubwa wa inchi ya Makedonia uliokuwa chini ya utawala wa Waroma. Nasi tukakaa katika muji ule kwa muda wa siku chache.
13Siku ya Sabato ilipotimia tukatoka ndani ya muji ule na kwenda karibu na muto mumoja, kwenye nafasi tulipozania kuwa ya kufanyia maombi. Tukaikaa na kusemezana na wanawake waliokusanyika pale.
14Na kati ya wanawake wale kulikuwa mwanamuke mumoja aliyeitwa Ludia, wa muji Tuatera. Yeye alikuwa muchuuzi wa nguo nyekundu za bei kali na mwenye kuogopa Mungu. Mwanamuke yule akatusikiliza kwa maana Bwana alimufungua moyo kusudi apate kufuata kabisa maneno Paulo aliyosema.
15Kisha yeye na watu wa nyumba yake wakabatizwa. Naye akatusihi akisema: “Ikiwa munakubali kweli kwamba ninamwamini Bwana, basi mufike mupange ndani ya nyumba yangu.”
Akatulazimisha tuitike.
Paulo na Sila wanafungwa16Siku moja tulipokuwa tukienda kule kwenye nafasi ya kufanyia maombi, tukakutana na mujakazi mumoja. Yule mwanamuke alikuwa na pepo wa kuaguza ndani yake. Na kwa njia ya uaguzi ule aliwatajirisha wabwana wake.
17Mwanamuke yule akaendelea kumufuata Paulo na sisi, akilalamika akisema: “Watu hawa ni watumishi wa Mungu Mukubwa. Wanawatangazia ninyi namna gani munavyoweza kuokolewa.”
18Naye akafanya hivi kwa muda wa siku nyingi. Na kwa mwisho Paulo akachukizwa naye. Basi akageuka na kumwambia yule pepo: “Ninakuamuru kwa jina la Yesu Kristo, utoke ndani yake!”
Na saa ile ile yule pepo akatoka ndani yake.
19Halafu wabwana wa yule mujakazi wakaona kwamba hawataweza tena kupata mali kutoka kwa yule aliyekuwa kitumaini chao. Kwa hiyo wakakamata Paulo na Sila, wakawakokota na kuwapeleka mbele ya wakubwa kwenye nafasi ya makutano.
20Walipowafikisha kwa watawala wa Waroma, wakasema: “Watu hawa ni Wayuda, nao wanaleta fujo katika muji wetu.
21Wanafundisha desturi ambazo sisi Waroma tunakatazwa kukubali na kufuata.”
22Basi kundi la watu waliokuwa pale wakawashambulia Paulo na Sila, nao watawala wakaamuru wawavue nguo kwa kinguvu na kuwapiga fimbo.
23Walipokwisha kuwapiga sana, wakawatia ndani ya kifungo na kumwagiza mulinzi wa kifungo awachunge kabisa.
24Na kufuatana na agizo lile, akawatia katika chumba cha ndani kabisa na kuwafungia miguu juu ya vipande vya miti kusudi ibaki imepanuka.
25Na katikati ya usiku, Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za sifa, nao wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza.
26Kwa rafla kukatokea tetemeko kubwa la inchi hata misingi ya nyumba ya kifungo ikatikisika. Na pale pale milango yote ikafunguka na minyororo ya wafungwa wote ikakatika.
27Mulinzi akaamuka, naye alipoona kwamba milango ilikuwa wazi, akachomoa upanga wake kusudi ajiue, kwa sababu aliwaza kama wafungwa wametoroka.
28Lakini Paulo akalalamika kwa nguvu akisema: “Usijiue, kwa maana sisi wote tuko hapa!”
29Basi yule mulinzi akaomba wamuletee taa, akarukia mbio ndani, akajitupa mbele ya Paulo na Sila, akitetemeka kwa hofu.
30Kisha akawapeleka inje na kuwauliza: “Wabwana wangu, inanipasa kufanya nini kusudi nipate kuokolewa!”
31Nao wakajibu: “Umwamini Bwana Yesu, nawe utaokolewa pamoja na watu wote wa nyumba yako.”
32Halafu wakamwelezea neno la Bwana pamoja na watu wote wa nyumba yake.
33Saa ile ile ya usiku mulinzi wa kifungo akawatwaa na kuwasafisha vidonda, naye akabatizwa pale pale na watu wake wote.
34Kisha akapeleka Paulo na Sila ndani ya nyumba yake na kuwapatia chakula. Yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake walifurahi sana kwa sababu wamemwamini Mungu.
35Na kesho yake kulipokucha, watawala wakatuma watumishi wamoja kwa yule mulinzi wa kifungo kwa kumwambia: “Uwafungue wale watu.”
36Yule mulinzi wa kifungo akamwelezea Paulo habari ile akimwambia: “Wakubwa wametuma habari kwamba mufunguliwe. Basi sasa mutoke na kujiendea na amani.”
37Lakini Paulo akawaambia wajumbe: “Wametupiga mbele ya watu wote bila kutusambisha, ijapokuwa sisi ni wanainchi wa Roma, na kisha wakatutia ndani ya kifungo. Na sasa namna gani wanataka kututosha kwa uficho? Haiwezekani! Wao wenyewe wafike kutufungua!”
38Wale wajumbe wakarudi na kuwapasha wakubwa maneno yale. Nao waliposikia kwamba Paulo na Sila ni wanainchi wa Roma, wakaogopa sana.
39Basi wakakuja, wakawabembeleza, wakawapeleka inje ya kifungo na kuwasihi watoke katika muji ule.
40Paulo na Sila walipotoka ndani ya kifungo, wakaenda kwa Ludia. Nao walipokwisha kuonana na wandugu na kuwatia moyo, wakaondoka.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.