1 Mambo ya Siku 28 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Maagizo ya Daudi juu ya hekalu

1Mufalme Daudi akakusanya kule Yerusalema wakubwa wote wa Waisraeli: wa makabila, majemadari na vikundi waliomutumikia mufalme, wakubwa wa maelfu na mamia, wasimamizi wa mali yote, ya ngombe wote wa mufalme na wana wake pamoja na wakubwa wa nyumba ya kifalme, mashujaa na waaskari wenye heshima.

2Halafu mufalme Daudi akasimama na kusema: “Enyi wandugu zangu na watu wangu, munisikilize. Nilikusudia ndani ya moyo wangu kujenga nyumba kwa ajili ya Sanduku la Agano la Yawe, kiti cha kuwekea miguu ya Mungu wetu; na nilifanya matayarisho ya kujenga. Ang. 2 Sam 7.1-16; 1 Sik 17.1-14

3Lakini Mungu alinikataza, kwa sababu mimi ni mutu wa vita na nimekwisha mwanga damu nyingi.

4Lakini Yawe, Mungu wa Israeli, alinichagua mimi kati ya jamaa ya baba yangu kuwa mufalme wa Israeli kwa milele. Alichagua kabila la Yuda kusudi liongozeke; na kutokana na kabila lile, alichagua jamaa ya baba yangu, na kati ya wana wa baba yangu, alipendezwa nami na kuniweka nikuwe mufalme wa Israeli yote.

5Yawe amenijalia wana wengi, na kati ya hao wote, amemuchagua Solomono mwana wangu, aikae juu ya kiti cha kifalme cha ufalme wa Yawe atawale.

6“Yawe aliniambia: ‘Mwana wako Solomono ndiye atakayenijengea nyumba na viwanja vyangu, kwa maana nimemuchagua yeye akuwe mwana wangu, nami nitakuwa baba yake.’

7Nitaimarisha ufalme wake milele ikiwa ataendelea kushika kwa moyo amri zangu na maagizo yangu kama vile anavyofanya leo.

8“Basi sasa, mbele ya kusanyiko hili la Waisraeli wote, taifa la watu wa Yawe, na mbele ya Mungu wetu, muangalie na mushike amri zote za Yawe, Mungu wenu, kusudi muendelee kurizi inchi hii nzuri, na kuwarizisha wazao wenu nyuma yenu, hata milele.

9“Nawe Solomono mwana wangu, umujue Mungu wa baba yako, na umutumikie kwa moyo wako wote na kwa nia nzuri; yeye Yawe anachunguza mioyo na anafahamu mipango na mafikiri ya mwanadamu. Ukimutafuta yeye, utamwona; lakini ukimwacha, atakutupilia mbali milele.

10Basi fanya angalisho na kukumbuka kwamba Yawe amekuchagua wewe umujengee nyumba ya ibada. Ukuwe hodari na utende hivyo.”

11Halafu Daudi akamupa Solomono mwana wake mufano wa majengo yote ya hekalu, nyumba zake, hazina zake, gorofi zake, vyumba vyake vya ndani na pahali pa kiti cha rehema.

12Alimupatia mufano wa yote aliyokusudia ndani ya moyo juu ya viwanja vya nyumba ya Yawe, vyumba vya Mungu na gala za kuwekea vitu vitakatifu.

13Akamupatia vilevile mufano wa jinsi ya kuwapanga makuhani na Walawi kwa kutimiza kazi zao, kutumikia nyumba ya Yawe na kutunza vyombo vyote vya nyumba ya Yawe.

14Alimupatia kiasi cha zahabu iliyohitajika kwa kutengeneza vyombo vyote vya zahabu vya utumishi wa kila namna, kiasi cha feza iliyohitajika kwa utumishi wa kila namna,

15uzito wa vinara vya zahabu na taa zake, uzito wa kila kinara na taa zake kiasi cha feza ya kutengeneza kinara na taa zake kulingana na matumizi ya kila kinara;

16na kiasi cha zahabu ya kutengeneza meza za zahabu za kuwekea mikate iliyotolewa kwa Mungu, hata kiasi cha feza ya kutengeneza meza za feza;

17vilevile alitoa maagizo juu ya kiasi cha zahabu safi iliyohitajika kwa kutengeneza makanya, mabeseni na vikombe, vilevile kiasi cha zahabu na feza iliyohitajika kwa kutengeneza mabakuli ya zahabu na ya feza,

18na kiasi cha zahabu safi ya kutengeneza mazabahu ya kufukizia ubani. Alimupatia vilevile mufano wake wa gari la zahabu la makerubi yaliyotandaza mabawa na kufunika Sanduku la Agano la Yawe.

19Hayo yote, mufalme Daudi aliyaweka wazi kwa maandiko aliyopewa na Yawe. Kazi yote itendeke kulingana na mufano ule.

20Kisha, mufalme Daudi akamwambia Solomono mwana wake: “Uwe imara na hodari, ufanye kazi hii. Usiogope wala kuwa na wasiwasi. Yawe Mungu ambaye ni Mungu wangu, yuko pamoja nawe. Hatakuachilia lakini atakuwa nawe mpaka itakapomalizika kazi yote ambayo inayohitajika kufanyiwa kwa nyumba ya Yawe.

21Makuhani na Walawi wamekwisha kupangiwa kazi watakazofanya katika nyumba ya Mungu. Watumishi wenye ujuzi wa kila aina watakuwa tayari kabisa kukusaidia, na watu wote pamoja na viongozi wao watakuwa chini ya mamlaka yako.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help