Ezekieli 32 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mufalme wa Misri analinganishwa na mamba

1Siku ya kwanza ya mwezi wa kumi na mbili, mwaka wa kumi na mbili tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

2Wewe mwanadamu! Imba wimbo wa kuomboleza juu ya Mufalme wa Misri.

Wewe Mufalme wa Misri unajiona kuwa simba kati ya mataifa,

lakini wewe ni kama mamba tu katika maji:

unachomoka kwa nguvu kwenye mito yako,

unayavuruga maji kwa miguu yako,

na kuichafua mito.

3Bwana wetu Yawe anasema:

Nitautupa wavu wangu juu yako,

nao watu watakuvua humo kwa wavu wangu.

4Nitakutupa juu ya inchi kavu,

nitakutupa chini juu ya uwanja,

nitaleta ndege wote watue juu yako,

na kuwashibisha nyama wote wa pori kwa mwili wako.

5Nitasambaza nyama yako juu ya milima,

na kujaza mabonde yote muzoga wako.

6Nitaikunywesha inchi damu yako mpaka juu ya milima,

mashimo yatajaa damu yako.

7Nitakapokuangamiza, nitazifunika mbingu,

nitazifanya nyota kuwa nyeusi,

jua nitalifunika kwa mawingu,

na mwezi hautatoa mwangaza wake.

8Nitaifanya miangaza yote mbinguni kuwa giza

nitatandaza giza juu ya inchi.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

9Nitaihuzunisha mioyo ya watu wengi, nitakapokupeleka katika utumwa kati ya mataifa, katika inchi ambazo hauzijui.

10Nitayashitusha mataifa mengi kwa habari zako,

wafalme wao watatetemeka kwa sababu yako,

nitakaponyoosha upanga wangu mbele yao.

Watatetemeka kila wakati,

kila mutu akiogopea maisha yake,

siku ile ya kuangamia kwako.

11Kwa maana, Bwana wetu Yawe anasema hivi:

Upanga wa mufalme wa Babeli utakufuatilia.

12Watu wako wengi watauawa kwa mapanga ya mashujaa,

watu wa hatari kuliko mataifa yote.

Watakomesha kiburi cha Misri na kuwaua watu wako wote.

13Nitawaangamiza nyama wako wote pembeni ya muto Nili.

Maji yake hayatavurugwa tena na mutu

wala kwato za nyama kuyachafua tena.

14Hapo nitayafanya maji yake yatulie

na kuitiririsha mito yake kama mafuta.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

15Nitakapoifanya inchi ya Misri kuwa jangwa na mali yake yote kunyanganywa, nitakapowaua wakaaji wake wote, halafu watatambua kwamba mimi ni Yawe.

16Huo ndio wimbo wa maombolezo,

wanawake wa mataifa watauimba,

wataimba juu ya Misri na watu wake wote.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Inchi ya wafu

17Siku ya kumi na tano ya mwezi wa kwanza, mwaka wa kumi na mbili tangu tulipopelekwa katika uhamisho, neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

18Wewe mwanadamu! Uwaombolezee watu wengi wa Misri. Uwapeleke chini kwenye inchi ya wafu pamoja na mataifa mengine yenye nguvu, waende huko pamoja na wanaoshuka chini kwa wafu.

19Uwaambie:

Ninyi ni wazuri kuliko nani?

Muende kuzimu mulalishwe pamoja na wasiomujua Mungu!

20Wamisri wataangamia pamoja na watu waliouawa katika vita. Upanga uko tayari kuangamiza Misri pamoja na watu wake wengi.

21Wakubwa wenye nguvu pamoja na wasaidizi wao wakiwa huko katika shimo kwa wafu watasema hivi: Wamisri wameshuka chini kwa wafu, wanalala pamoja na watu wasiomujua Mungu, waliouawa katika vita.

22Asuria iko huko. Makaburi ya waaskari wake yanaizunguka. Wote waliuawa katika vita.

23Makaburi yao yako sehemu za chini kabisa katika shimo kwa wafu. Waaskari wao wanaizunguka. Wote waliuawa katika vita. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima.

24Elamu nayo iko huko. Makaburi ya waaskari wake yanaizunguka. Wote waliuawa katika vita. Wakashuka kwenye inchi ya wafu, bila kujua Mungu. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima. Lakini sasa wanapata haya yao pamoja na wale wanaoshuka katika shimo kwa wafu.

25Elamu imelalishwa kati ya wale waliouawa katika vita. Makaburi yao yanaizunguka. Wote waliuawa katika vita, bila kujua Mungu. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima, na sasa wako wanapata haya yao pamoja na wale wanaoshuka katika shimo kwa wafu. Wanawekwa kati ya wale waliouawa.

26Mesaki na Tubali ziko huko. Makaburi ya watu wake wote yanazizunguka. Wote waliuawa katika vita, bila kujua Mungu. Walipokuwa wangali wanaishi, walieneza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima.

27Hawakuzikwa pamoja na mashujaa wa zamani, ambao walikwenda katika kuzimu kwa wafu wakiwa na silaha zao, mapanga yao chini ya vichwa vyao na ngao zao juu ya miili yao. Mashujaa hao walipokuwa wangali wanaishi walijaza vitisho vyao katika inchi ya wanaokuwa wazima.

28Basi, ninyi Wamisri mutaangamizwa na kulalishwa kati ya wasiomujua Mungu waliouawa katika vita.

29Edomu iko huko pamoja na wafalme wake na wakubwa wao wote. Walipokuwa wangali wanaishi walikuwa na nguvu sana, lakini sasa wamelalishwa kwa wafu pamoja na wasiomujua Mungu waliouawa katika vita.

30Wakubwa wote wa watu wa upande wa kaskazini wako huko vilevile; hata Wasidoni wote walikwenda kujiunga na wafu. Walipokuwa wangali wanaishi, walisababisha vitisho kwa nguvu zao, lakini sasa hao wasiomujua Mungu wamelalishwa chini na haya pamoja na wale waliouawa katika vita. Wanashiriki haya ya wale walioshuka ndani ya shimo kwa wafu.

31Mufalme wa Misri, atakapowaona hao wote atafarijika kwa ajili ya wingi wa majeshi yake yote.

32Nilimuwezesha mufalme wa Misri aeneze vitisho katika inchi ya wanaokuwa wazima, lakini sasa yeye mwenyewe pamoja na jeshi lake lote watauawa katika vita na kulalishwa pamoja na wasiomujua Mungu, waliokufa katika vita.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help