2 Mambo ya Siku 8 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mafanikio ya Solomono(1 Fal 9.10-28)

1Kisha miaka makumi mbili, ambayo Solomono alipitisha kwa kujenga nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme,

2Solomono akajenga upya miji aliyopewa na Hiramu, halafu akawapa Waisraeli miji hiyo waishi mule.

3Nyuma ya pale Solomono akaenda katika muji wa Hamati-Soba na kuuteka,

4na kuujenga muji wa Tadimori katika jangwa. Alijenga upya miji ya gala iliyokuwa kule Hamati.

5Vilevile, Solomono akajenga miji hii: Beti-Horoni wa juu, na Beti-Horoni wa chini, miji yenye minara ya kufichamia, kuta, milango na vifungio,

6muji wa Balati, na miji yake yote ya kuwekea magari yake ya vita na ya waaskari wapanda-farasi wake, na kitu chochote alichotaka kujenga katika Yerusalema, Lebanoni au nafasi ingine katika ufalme wake.

7Watu wengine wote waliobaki kati ya Wahiti, Waamori, Waperizi, Wahivi na Wayebusi, ni kusema wote ambao hawakukuwa Waisraeli,

8vilevile kati ya wazao wao ambao Waisraeli hawakuwaangamiza, Solomono akawatumikisha kazi za kulazimishwa, na hivi ndivyo wanavyofanya hata sasa.

9Lakini kati ya watu wa Israeli, Solomono hakumufanya mutu yeyote kuwa mutumwa; kwa ajili ya kazi yake: wao walikuwa waaskari, majemadari wa wakubwa wake, majemadari wa magari yake ya vita na waaskari wapanda-farasi wake.

10Hii ndiyo jumla ya wakubwa wa mufalme Solomono: walikuwa mia mbili makumi tano, waliokuwa na mamlaka juu ya watu.

11Solomono alimuhamisha binti wa mufalme wa Misri, kutoka muji wa Daudi, akamupeleka kwenye nyumba aliyomujengea. Akasema: “Muke wangu hataishi katika nyumba ya Daudi mufalme wa Israeli, kwa maana pahali pote ambapo sanduku la Yawe limekuwa, ni patakatifu.”

12Solomono akamutolea Yawe sadaka za kuteketeza juu ya mazabahu aliyokuwa amemujengea Yawe mbele ya baraza la hekalu.

13Alitoa sadaka zile kadiri ilivyotakiwa na amri ya Musa kila siku takatifu, ni kusema siku za Sabato, sikukuu za mwandamo wa mwezi, na sikukuu tatu za kila mwaka – sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu, sikukuu ya majuma na sikukuu ya vibanda. Ang. Kut 23.14-17; 34.22-23; Hes 28.9; 29.39; Kumb 16.16

14Akifuata maagizo ya Daudi baba yake, alipanga zamu za kila siku za makuhani na za Walawi waliowasaidia makuhani kusifu na kutimiza kazi zao. Vilevile aliwapanga walinzi wa milango katika makundi aliyoweka kwa kulinda kila mulango; maana ndivyo Daudi, mutu wa Mungu alivyoamuru.

15Nao hawakuacha maagizo ya mufalme aliyowaamuru makuhani na Walawi kwa jambo lolote na juu ya hazina.

16Basi kazi zote Solomono alizokusudia kufanya zikamalizika. Yeye alitimiza kazi zile zote tangia jiwe la musingi wa nyumba ya Yawe lilipowekwa mpaka ilipomalizika kujengwa. Hivi nyumba ya Yawe ikamalizika.

17Kisha Solomono akakwenda Ezioni-Geberi na Eloti kwa vivuko vya bahari, katika inchi ya Edomu.

18Hiramu akamupelekea mashua zilizokuwa chini ya uongozi wa watumishi wake, pamoja na wafundi wa mashua. Wale, pamoja na watumishi wa Solomono, wakasafiri mpaka Ofiri, na kubeba kutoka kule zahabu, wakamuletea mufalme Solomono yapata kilo elfu kumi na tano.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help