1 Samweli 16 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Daudi anapakwa mafuta kwa kusimikwa kuwa mufalme

1Yawe akamwambia Samweli: “Utamulilia Saulo mpaka wakati gani? Wewe unajua kwamba mimi nimemukataa kuwa mufalme wa Israeli. Sasa, jaza ile pembe yako ya kuwekea mafuta, uondoke. Nitakutuma kwa Yese wa muji wa Betelehemu. Maana nimejipatia mufalme kati ya wana wake.”

2Samweli akasema: “Nitaweza kwenda namna gani? Kama Saulo akisikia habari hiyo, ataniua!”

Yawe akamwambia: “Twaa mwana-ngombe pamoja nawe, na ukifika kule useme: ‘Nimekuja kumutolea Yawe sadaka’.

3Umwalike Yese kwenye sadaka hiyo nami nitakuonyesha la kufanya. Utamupakaa mafuta kwa ajili yangu mutu yule nitakayekutajia.”

4Samweli akafanya sawa alivyoambiwa na Yawe, akaenda Betelehemu. Wazee wa muji wakatoka kwenda kumupokea wakiwa wanatetemeka, wakamwuliza: “Umekuja kwa amani?”

5Samweli akawajibu: “Nimekuja kwa amani. Nimekuja kumutolea Yawe sadaka. Mujitakase wenyewe halafu tuende kutolea sadaka.” Samweli akamutakasa Yese pamoja na wana wake, akawakaribisha kwenye sadaka.

6Walipofika, naye Samweli alipomwona Eliabu, alijisemesha ndani ya moyo wake: “Hakika, muchaguliwa wa Yawe ndiye huyu anayekuwa mbele ya Yawe!”

7Lakini Yawe alimwambia: “Usiangalie sura yake wala urefu wake. Mimi nimemukataa maana siangalii mambo kama vile wanadamu wenye kufa wanavyoangalia. Mwanadamu anaangalia umbo la inje, lakini mimi ninaangalia ndani ya moyo.”

8Kisha, Yese akamwita Abinadabu na kumuleta mbele ya Samweli. Lakini Samweli akasema: “Wala huyu hakuchaguliwa na Yawe.”

9Yese akamuleta Shama. Samweli akasema: “Wala huyu hakuchaguliwa na Yawe.”

10Yese aliwapitisha wana wake wote saba mbele ya Samweli lakini Samweli akamwambia: “Yawe hajamuchagua mutu yeyote kati ya hawa.”

11Halafu akamwambia: “Wana wako wote wako hapa?”

Yese akajibu: “Hapana, kungali mudogo wa hawa wote, lakini amekwenda kuchunga kondoo.”

Samweli akamwambia: “Utume mutu amulete. Sisi hatutaikaa chini, mpaka atakapokuja hapa.”

12Hivyo, Yese alituma mutu, naye akaletwa. Yule kijana alikuwa mwenye afya, mwenye macho yenye kungaa na wa kupendeza. Yawe akamwambia Samweli: “Sasa, huyu ndiye; simama umupakae mafuta.”

13Samweli akatwaa pembe lake lenye mafuta akamupakaa Daudi mafuta mbele ya kaka zake. Mara moja roho wa Yawe akamushika Daudi kwa nguvu na kuwa naye tangu siku hiyo. Kisha Samweli akarudi katika muji wa Rama.

Daudi kwenye baraza la Saulo

14Kisha roho wa Yawe alimwacha Saulo, na pepo muchafu kutoka kwa Yawe akamusumbua.

15Halafu watumishi wa Saulo wakamwambia: “Tunajua kwamba pepo muchafu kutoka kwa Mungu anakusumbua.

16Sasa, ee bwana wetu, amuru watumishi wako wanaokutumikia wamutafute mutu mwenye ufundi wa kupiga kinubi, na huyo pepo muchafu kutoka kwa Mungu atakapokufikia, mutu yule atapiga kinubi, nawe utapata utulivu.”

17Saulo akawaambia watumishi wake: “Munitafutie mutu yule anayeweza kupiga kinubi vizuri, muniletee naye.”

18Kijana mumoja kati ya watumishi akasema: “Nimemwona kijana mumoja wa Yese, wa muji wa Betelehemu. Kijana yule ana ujuzi wa kupiga kinubi. Yule kijana ni shujaa, hodari wa kupigana katika vita, ana hekima katika kusema na mwenye umbo zuri; Yawe yuko pamoja naye.”

19Hivyo, Saulo alituma ujumbe kwa Yese, na kusema: “Unitumie mwana wako Daudi, ambaye anachunga kondoo.”

20Yese alimutuma Daudi kwa Saulo pamoja na punda aliyebeba mikate, mufuko wa ngozi unaojaa divai na mwana-mbuzi.

21Daudi alipofika akaingia kwa kumutumikia Saulo. Saulo alimupenda sana, hata akamufanya akuwe mwenye kumubebea silaha zake.

22Halafu Saulo alituma ujumbe kwa Yese na kusema: “Umwache Daudi akae hapa anitumikie kwa sababu amepata kukubaliwa mbele yangu.”

23Kila mara, yule roho mwovu kutoka kwa Mungu alipomufikia Saulo, Daudi alitwaa kinubi chake na kuanza kukipiga, na roho yule alimwacha Saulo, naye akajisikia vizuri na kupata utulivu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help