1Yawe anasema hivi:
Munisikilize enyi munaotaka kukombolewa,
ninyi munaonitafuta mimi Yawe.
Muangalie jiwe mulilochongwa toka ndani yake,
mulima mulimochimbuliwa.
2Mukumbuke Abrahamu babu yenu,
na Sara aliyewazaa ninyi.
Abrahamu alikuwa hana mutoto wakati nilipomwita,
lakini nilimubariki na kumufanya kuwa na wengi.
3Mimi Yawe nitaufariji Sayuni,
nitatengeneza pahali pake pote palipoharibika.
Nitazifanya mbuga zake kama shamba la Edeni,
jangwa yake kama bustani ya Yawe.
Ndani yake kutapatikana furaha na shangwe,
na nyimbo za shukrani zitasikilika humo.
4Munisikilize, enyi watu wangu,
munitegee sikio, enyi taifa langu.
Sheria na haki zitatoka kwangu mimi;
nazo zitakuwa mwangaza wa mataifa.
5Ukombozi wangu unakaribia upesi;
wokovu nitakaoleta unaanza kutokea.
Mimi mwenyewe nitayatawala mataifa.
Wakaaji wa inchi za mbali wananingojea,
wanaitegemea nguvu yangu.
6Muinue macho, muangalie mbingu,
kisha muangalie dunia kule chini.
Mbingu zitatoweka kama moshi,
dunia itachakaa kama nguo,
na wakaaji wake watakufa kama vidudu.
Lakini wokovu ninaouleta unadumu milele;
ukombozi wangu hautakoma hata kidogo.
7Munisikilize, enyi munaojua mambo ya haki,
ambao sheria zangu ziko ndani ya mioyo yenu.
Musiogope mazarau ya watu,
wala kufazaishwa na masimango yao.
8Maana watakuliwa na nondo kama vile nguo;
vidudu watawakula kama wanavyokula nguo ya manyoya ya kondoo.
Lakini ukombozi ninaouleta mimi utadumu milele;
wokovu wangu hautakuwa na mwisho.
9Amuka! Amuka na nguvu,
ee mukono wa Yawe!
Amuka kama ulivyofanya hapo zamani,
nyakati za vizazi vilivyopita.
Si wewe ndiwe uliyemukatakata yule nyama mukubwa Rahabu,
ukamutoboa yule nyoka mukubwa wa kuogopesha?
10Wewe ndiwe uliyekausha bahari,
ndiwe uliyevikausha vilindi vya maji
na kufanya njia katika vilindi vya bahari,
kusudi wale uliowakomboa wavuke humo.
11Watu wako uliowakomboa, ee Yawe, watarudia,
watakuja Sayuni wakiimba;
watajaa furaha ya milele,
watapata furaha na shangwe.
Huzuni na maombolezo vitatoweka kabisa.
12Yawe anasema hivi:
Mimi, kweli mimi, ndiye ninayekufariji.
Kwa nini wewe unamwogopa mutu ambaye ni wa kufa,
mwanadamu ambaye anatoweka kama majani?
13Wewe umenisahau mimi Yawe Muumba wako,
niliyezitandaza mbingu,
na kuiweka misingi ya dunia!
Kwa sababu ya kasirani ya yule anayekutesa,
unaendelea kuogopa siku zote
kwamba yuko tayari kukuangamiza!
Lakini hasira yake itafikia wapi?
14Wafungwa watafunguliwa upesi,
hawatakufa na kushuka katika shimo,
wala hawatakosewa chakula.
15Mimi ni Yawe, Mungu wako,
ninayechafua bahari, zoruba yake ikinguruma;
Yawe wa majeshi, ndilo jina langu!
16Nimeyaweka maneno yangu katika kinywa chako;
nimekuficha katika kivuli cha mukono wangu.
Mimi nilizitandaza mbingu,
nikaiweka misingi ya dunia.
Mimi ninawaambia, enyi watu wa Sayuni:
Ninyi ni watu wangu.
Mwisho wa mateso ya Yerusalema17Amuka, ewe Yerusalema!
Amuka usimame wima!
Yawe amekukunywesha kikombe cha kasirani yake,
nawe umekikunywa mpaka tone la mwisho,
mpaka ukayumbayumba.
18Kati ya watoto wote uliowazaa
hakuna yeyote wa kukuongoza.
Hakuna hata mumoja wa kukushika mukono
kati ya watoto wote uliowalea.
19Hasara hizi mbili zimekupata:
uharibifu na maangamizi; njaa na mauaji.
Nani atakayekuonea huruma?
Nani atakayekufariji?
20Watoto wako wamezimia,
wamelala pembeni ya kila barabara,
wako kama paa aliyenaswa ndani ya mutego.
Wamepatwa na kasirani ya Yawe,
wamepatwa na azabu ya Mungu wako.
21Basi, sikiliza, ewe Yerusalema unayeteseka;
sikiliza wewe uliyelewa, lakini sio kwa divai.
22Bwana, Yawe, Mungu wako,
anayewatetea watu wake, anasema hivi:
Nimekuondolea kikombe cha kuyumbisha,
hautakunywa tena kikombe cha kasirani yangu.
23Nami nitakitia katika mikono ya wanaokutesa,
waliokuambia ulalie tumbo wapite juu yako,
nawe ukaufanya mugongo wako kama vile udongo wa njia,
kama vile barabara ya kupitia.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.