Isaya 43 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu anaahidi kuwaokoa watu wake

1Yawe aliyewaumba enyi watu wa Yakobo,

yeye aliyewafanya enyi watu wa Israeli, anasema hivi:

Musiogope, maana mimi nimewakomboa;

nimewaita kwa jina lenu nanyi ni wangu.

2Mukipita katika maji,

mimi nitakuwa pamoja nanyi;

mukipita katika mito,

haitawashinda nguvu.

Mukitembea katika moto,

hamutaungua;

ulimi wa moto hautawaunguza.

3Maana mimi ni Yawe, Mungu wenu,

Mungu Mutakatifu wa Israeli, Mwokozi wenu.

Ninaitoa inchi ya Misri kwa ajili ya ukombozi wenu,

ninaitoa Kushi na Seba kusudi muachwe huru.

4Ninyi ni wa bei kali mbele yangu,

ninawaheshimu na kuwapenda.

Kwa hiyo, ninatoa watu kusudi niwapate ninyi,

ninayaachilia mataifa pahali pa maisha yenu.

5Musiogope maana mimi nipo pamoja nanyi.

Nitawarudisha wazao wenu toka mashariki,

nitawakusanya ninyi kutoka magaribi.

6Nitaiambia kaskazini: “Uwaache waondoke”,

na kusini: “Usiwazuize!

Muwarudishe watu kutoka mbali,

kutoka kila pahali katika dunia.

7Kila mumoja anajulikana kwa jina langu;

niliwaumba wote na kuwafanya

kwa ajili ya utukufu wangu.”

Israeli ni ushuhuda wa Yawe

8Muwalete mbele watu hao,

ambao wana macho lakini hawaoni,

wana masikio lakini hawasikii!

9Mataifa yote yakusanyike,

watu wote wakutane pamoja.

Nani kati ya miungu yao anayeweza kutangaza yatakayotukia?

Nani anayeweza kutuonyesha yanayotukia sasa?

Wawalete washuhuda wao,

kuhakikisha kwamba walifanya hivyo.

Uwaache wasikilize na kusema: Ilikuwa kweli.

10Ninyi Waisraeli ni washuhuda wangu.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Niliwachagua mukuwe watumishi wangu,

mupate kunijua na kuniamini,

kwamba mimi ni Mungu.

Mbele yangu hakukuwa mungu mwingine,

wala hakutakuwa mungu mwingine nyuma yangu.

11Mimi peke yangu ndiye Yawe,

hakuna mukombozi mwingine isipokuwa mimi.

12Nilitangaza yale ambayo yangetukia,

kisha nikakuja na kuwakomboa.

Hakuna mungu mwingine aliyetangulia kufanya hivyo,

nanyi ni washuhuda wangu.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

13Mimi ni Mungu na nitakuwa Mungu siku zote.

Hakuna anayeweza kuepuka nguvu yangu;

hakuna anayeweza kupinga ninayofanya.

Kukombolewa kutoka Babeli

14Yawe, Mukombozi wenu,

Mutakatifu wa Israeli, anasema hivi:

Kwa ajili yenu nitatuma waaskari kwenda Babeli.

Nitavunja vifungio vya milango ya muji wake,

na kelele za wale Wakaldea zitageuka maombolezo.

15Mimi ni Yawe, Mutakatifu wenu;

Mimi ndiye Muumba wa Israeli, Mufalme wenu.

16-17Zamani Yawe alifanya barabara katika bahari

na kuweka njia kati ya maji mengi.

Alipiga kundi la waaskari lenye nguvu,

kundi la magari na farasi wa vita,

waaskari na mashujaa wa vita.

Aliwaangusha chini hata hawawezi kusimama tena,

Aliwakomesha na kuwazimisha kama utambi wa taa.

Sasa Yawe anasema hivi:

18Musiyakumbuke mambo yaliyopita,

wala musifikiri juu ya vitu vya zamani.

19Muangalie, mimi ninafanya kitu kipya.

Kinafanyika sasa hivi,

nanyi mutaweza kukiona.

Nitafanya njia katika mbuga,

na kububujisha mito katika jangwa.

20Nyama wa pori wataniheshimu,

mbweha na mbuni,

maana nitaweka maji katika mbuga,

na kububujisha mito katika jangwa,

kwa kuwakunywesha watu wangu niliojichagulia,

21watu niliowaumba kwa ajili yangu mwenyewe,

kusudi wazitangaze sifa zangu!

Zambi ya Israeli

22Lakini ewe taifa la Yakobo, haukuniabudu mimi;

enyi watu wa Israeli, mulichoka nami!

23Hamujaniletea kondoo wenu wa sadaka za kuteketezwa,

wala kuniheshimu kwa sadaka zenu.

Nami sikuwalemea ninyi kwa kutaka sadaka,

wala sikuwachokesha kwa kuwadai ubani.

24Hamukuninunulia marasi kwa mali yenu,

wala kunishibisha kwa mafuta za sadaka.

Pahali pake zambi zenu zimekuwa muzigo kwangu,

mumenichokesha kabisa kwa makosa yenu.

25Lakini mimi ndiye niliyefuta makosa yenu kwa heshima yangu,

ndiye ninayefuta makosa kwa ajili yangu mwenyewe,

wala sitazikumbuka zambi zenu.

26Munikumbushe tena makosa yangu,

tusambe nanyi,

mutoe mashitaki yenu kusudi tuuone ukweli wenu!

27Babu yenu wa kwanza alitenda zambi,

wapatanishi wenu waliniasi.

28Kwa hiyo niliwazaraulisha wakubwa wa Pahali Patakatifu

nikawaacha watu wa Yakobo waangamizwe,

nikawaacha Waisraeli watukaniwe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help