Ruta 1 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Elimeleki na jamaa yake wanakwenda Moabu

1Hapo zamani, wakati waamuzi walipokuwa wanatawala Waisraeli, kulitokea njaa katika inchi. Mutu mumoja kutoka Betelehemu katika Yuda pamoja na muke wake na watoto wao wanaume wawili walikwenda kuishi kwa muda katika inchi ya Moabu kwa kuishi kama wageni.

2Mutu yule aliitwa Elimeleki na muke wake aliitwa Naomi. Watoto wao wawili wanaume, mumoja aliitwa Malona na mwingine Kiliona. Mutu yule na jamaa yake walikuwa wa kabila la Efuraimu kule Betelehemu katika Yuda. Walikwenda katika inchi ya Moabu, wakakaa kule.

3Lakini Elimeleki, mume wa Naomi, akakufa na Naomi akaachwa na wana wake.

4Vijana hao walioa wabinti wa Kimoabu, Orupa na Ruta. Nyuma ya miaka kumi hivi,

5Malona na Kiliona nao vilevile wakakufa.

Naomi na Ruta wanarudi Betelehemu

6Kisha, Naomi akapata habari kwamba Yawe alikuwa amewabariki watu wake kwa kuwapa chakula. Basi, akaondoka kutoka Moabu kurudi kwao, pamoja na wakwe zake.

7Akaondoka pahali pale alipoishi pamoja na wakwe zake, wakashika njia ya kurudi Yuda.

8Naomi akawaambia hao wakwe zake wawili: “Murudi kila mumoja kwa mama yake. Ninaomba Yawe awatendee mema kama vile mulivyonitendea mema mimi na wale watu wangu waliokufa.

9Yawe awajalie, kila mumoja wenu apate mume na nyumba yake.” Kisha Naomi akawaaga kwa kuwabusu. Lakini wao walianza kulia kwa sauti

10na kumwambia: “Hapana hata kidogo! Tutakwenda pamoja nawe kwa watu wako.”

11Naye Naomi akawasihi: “Murudi, wabinti zangu. Kwa nini kunifuata? Munafikiri ninaweza kupata tena watoto watakaokuwa waume zenu?

12Murudi kwenu wabinti zangu, kwa maana mimi ni muzee sana, siwezi kuolewa tena. Hata kama ningesema nina tumaini, na hata kama ningepata mume usiku huu na kupata watoto,

13mungeweza kungoja mpaka wakomae? Mungeweza kujizuia musiolewe na wanaume wengine? Sivyo, wabinti zangu! Mambo yangu ni magumu sana kwa ajili yenu, maana Yawe amenipiga pigo.”

14Kwa hiyo wakalalamika wakaanza kulia tena. Halafu Orupa akamukumbatia mama mukwe wake, akamwaga na kurudi kwao. Lakini Ruta, akashikamana naye.

15Basi Naomi akamwambia: “Ruta, angalia dada yako amerudi kwao na kwa mungu wake; basi, nawe vilevile urudi, umufuate dada yako.”

16Lakini Ruta akamujibu:

“Usinisihi nikuache wewe,

wala usinizuie kufuatana nawe.

Popote utakapokwenda ndipo nami nitakapokwenda,

na pale utakapokaa mimi nitakaa,

watu wako watakuwa watu wangu,

na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.

17Pale utakapokufia ni pale nitakufia nami,

na ni palepale nitazikwa.

Yawe anipe azabu kali kama nikitenganishwa nawe

isipokuwa tu kwa kifo.”

18Naomi alipoona kwamba Ruta ameamua kwenda pamoja naye, aliacha kumushawishi.

19Halafu wote wawili wakaendelea na safari mpaka Betelehemu. Walipofika kule, watu wote wakashangaa, hata wanawake wakaulizana: “Huyu ni Naomi?”

20Naomi akasema: “Musiniite tena Naomi muniite Mara, kwa maana Mungu Mwenye Nguvu ameyafanya maisha yangu yakuwe machungu sana.

21Nilipoondoka hapa, nilikuwa na vitu vingi, lakini sasa Yawe amenirudisha mikono mitupu. Mbona munaniita Naomi ijapokuwa Yawe ameniazibu, naye Mungu Mwenye Nguvu amenitesa?”

22Hivi ndivyo Naomi pamoja na mukwe wake Ruta wa Moabu walivyorudia kutoka Moabu, na wakafika Betelehemu wakati mavuno ya shayiri yalipokuwa yanaanza.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help