1Kwa mara nyingine, Daudi aliwakusanya wale waaskari bora wa Israeli. Jumla yao ilikuwa watu elfu makumi tatu.
2Daudi aliondoka pamoja nao wote kuenda Bali-Yuda kwa kuleta Sanduku la Mungu linaloitwa kwa jina la Yawe wa majeshi, anayeikaa kwenye kiti chake cha kifalme juu ya makerubi.
3Basi, wakaondoa Sanduku la Mungu kutoka katika nyumba ya Abinadabu iliyokuwa juu ya mulima, wakalibeba juu ya gari jipya. Wana wa Abinadabu, Uza na Ahio, wakaongoza gari lile jipya,
4likiwa na Sanduku lile la Mungu, naye Ahio akiwa anatangulia mbele ya Sanduku lile.
5Daudi na watu wote wa Israeli, walikuwa wanaimba nyimbo na kucheza kwa nguvu zao zote, mbele ya Yawe. Walipiga ala za muziki zilizotengenezwa na muti wa muvinje: vinubi, vinanda, matari, kayamba na matoazi.
6Walipofika kwenye uwanja wa kupepetea ngano wa Nakoni, Uza aliunyoosha mukono wake na kuligusa Sanduku la Mungu kwa sababu wale ngombe walijikwaa.
7Halafu, hasira ya Yawe ikawaka juu ya Uza. Mungu akamwua palepale. Uza akakufa palepale pembeni ya Sanduku la Mungu.
8Naye Daudi alikasirika maana Yawe alimwazibu Uza kwa hasira. Kwa hiyo, pahali pale pakaitwa “Azabu ya Uza” mpaka hivi leo.
9Siku hiyo Daudi alimwogopa Yawe akasema: “Sasa Sanduku la Yawe litanifikia namna gani?”
10Kwa hiyo, Daudi hakukuwa tayari kwa kulipeleka Sanduku la Yawe ndani ya muji wa Daudi, lakini Daudi alilipeleka katika nyumba ya Obedi-Edomu wa Gati.
11Sanduku hilo la Yawe lilikaa katika nyumba ya Obedi-Edomu kwa muda wa miezi mitatu; naye Yawe akamubariki Obedi-Edomu pamoja na jamaa yake.
12Mufalme Daudi aliposikia kwamba Yawe ameibariki jamaa ya Obedi-Edomu na vitu vyote alivyokuwa navyo kwa sababu ya Sanduku la Mungu, akaenda kuliondoa Sanduku la Agano kutoka katika nyumba ya Obedi-Edomu na kulipeleka kwenye muji wa Daudi kwa shangwe.
13Watu wale waliolibeba Sanduku la Yawe kila mara walipopiga hatua sita, Daudi alitoa sadaka: ngombe dume na mwana-ngombe mumoja wenye kunona.
14Daudi alikuwa amejifungia kizibao cha kuhani katika kiuno chake. Alicheza kwa nguvu zake zote mbele ya Yawe.
15Hivyo, yeye na Waisraeli wote walilipeleka Sanduku la Yawe mpaka katika muji wa Daudi kwa shangwe na sauti kubwa ya baragumu.
16Sanduku la Yawe lilipokuwa linaingia katika muji wa Daudi, Mikali binti wa Saulo alichungulia kwenye dirisha, akamwona mufalme Daudi akirukaruka na kucheza mbele ya Yawe. Basi, akamuzarau ndani ya moyo wake.
17Kisha waliliingiza Sanduku la Yawe ndani ya hema ambalo Daudi alikuwa amelisimamisha pale na kuliweka pahali pake. Naye Daudi akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani mbele ya Yawe.
18Daudi alipomaliza kutoa sadaka za kuteketezwa na za amani, aliwabariki watu kwa jina la Yawe wa majeshi,
19na akawagawanyia watu wote, kundi lote la Waisraeli, wanaume na wanawake, kila mumoja, mukate, kipande cha nyama na mukate wa sadaka. Kisha, watu wote waliondoka, kila mutu akarudi kwake.
20Daudi aliporudi kwake kwa kuibariki jamaa yake, Mikali, binti ya Saulo, alikwenda kumupokea, akasema: “Ni ajabu kwa mufalme wa Waisraeli kujiheshimu leo, kwa kujifunua uchi wake mbele ya watumishi wake na wajakazi wake sawa vile mushenzi anavyovua nguo zake mbele ya watu bila haya!”
21Daudi akamwambia Mikali: “Nilikuwa mbele ya Yawe ambaye alinichagua mimi pahali pa baba yako na jamaa yake, kwa kunichagua kuwa mukubwa juu ya Waisraeli, watu wa Yawe. Kwa hiyo mimi nitacheza tu mbele ya Yawe.
22Nitajishusha mwenyewe zaidi kuliko sasa. Wewe utaniona kuwa si kitu, lakini hao wajakazi uliowasema wataniheshimu.”
23Basi Mikali binti ya Saulo hakukuwa na mutoto mpaka kufa kwake.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.