1Amazia alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mitano alipoanza kutawala, akatawala kwa muda wa miaka makumi mbili na mitano katika Yerusalema. Mama yake aliitwa Yoadani wa Yerusalema.
2Alitenda kwa usawa mbele ya Yawe ingawa hakutenda kwa moyo mukamilifu.
3Mara tu Amazia alipojiimarisha katika mamlaka akawaua watumishi waliomwua mufalme baba yake.
4Lakini hakuwaua watoto wao, kama vile ilivyoandikwa katika sheria zinazokuwa katika kitabu cha Musa, ambamo Yawe anatoa amri akisema: “Wazazi hawatauawa kwa ajili ya watoto wao, wala watoto hawatauawa kwa ajili ya wazazi wao; lakini kila mutu atauawa kwa ajili ya zambi zake mwenyewe.” Vita katika Edomu(2 Fal 14.7)
5Mufalme Amazia akawakusanya wanaume wa Yuda, akawapanga katika vikundi mbalimbali kulingana na ukoo zao, akawaweka chini ya majemadari wa maelfu na wa mamia kwa ajili ya Yuda na Benjamina. Alipowakagua wale wenye miaka makumi mbili na zaidi, akapata watu elfu mia tatu kwa jumla. Wote walikuwa watu waliochaguliwa wanaofaa kwa vita, wanaoweza kutumia mikuki na ngao.
6Tena, alilipa waaskari wengine mashujaa elfu moja kutoka Israeli, kwa bei ya kilo elfu tatu za feza.
7Lakini mutu wa Mungu akamwendea na kumwambia: “Ee mufalme, usiende kwenye vita pamoja na hawa waaskari wa Israeli, maana Yawe hayuko pamoja na watu wa Israeli. Hayuko pamoja na hawa Waefuraimu wote.
8Lakini ukitaka kwenda, basi ufanye vile, ukuwe hodari katika vita, lakini Mungu atakufanya ushindwe na waadui, kwa maana Mungu ana nguvu kwa kusaidia au kumufanya mutu ashindwe.”
9Amazia akamwuliza yule mutu wa Mungu: “Tutafanya nini na feza yote ambayo nimekwisha wapa waaskari wa Israeli?”
Naye akamujibu: “Yawe anaweza kukupa zaidi ya hiyo.”
10Kwa hiyo Amazia akawaacha waaskari waliotoka Efuraimu warudi kwao. Basi wakarudi kwao wakiwa wamewakasirikia sana watu wa Yuda.
11Amazia akajipa moyo akaongoza jeshi lake mpaka kwenye Bonde la Chumvi. Hapo akapigana na kuwaua watu elfu kumi wa Seiri.
12Na wengine watu elfu kumi, wakakamatwa na kuwapandisha juu ya jiwe kubwa na kuwatupa chini toka juu ya jiwe, wakavunjika vipandevipande.
13Wakati uleule, wale waaskari Waisraeli ambao Amazia aliwaacha warudi kwao akiwakataza wasijiunge naye katika vita, wakakwenda na kuishambulia miji ya Yuda, toka Samaria mpaka Beti-Horoni, wakaua watu elfu tatu na kunyanganya vitu vingi.
14Amazia aliporudi kisha kuwashinda Waedomu, akaleta miungu ya Waedomu akaifanya kuwa miungu yake, akainama uso mpaka chini mbele yao na kuifukizia ubani.
15Hayo yakamukasirisha sana Yawe, akatuma nabii kwa Amazia. Nabii huyo akamwuliza Amazia: “Kwa nini unategemea miungu ya watu wengine ambayo hata haikuweza kuwaokoa watu wake wenyewe kutoka katika mikono yako?”
16Na alipokuwa angali akisema naye, Amazia akamwambia: “Nyamaza! Tulikufanya wewe kuwa mushauri wa mufalme? Kwa nini uawe?”
Nabii akanyamaza, lakini akasema: “Ninafahamu kwamba Mungu ameamua kukuangamiza kwa maana umetenda haya yote, kisha unazarau shauri langu.”
Vita katika Israeli(2 Fal 14.8-20)17Basi Amazia mufalme wa Yuda alifanya shauri, akatuma ujumbe kwa Yoasi, mwana wa Yoahazi, mwana wa Yehu mufalme wa Israeli, akamwambia: “Kuja tuonane uso kwa uso.”
18Lakini Yoasi mufalme wa Israeli akamupelekea Amazia ujumbe akisema: “Siku moja, muti wa mubaruti wa Lebanoni ukauambia mwerezi nao ni wa kule hivi: ‘Umwoeshe binti yako kwa mwana wangu!’ Lakini nyama mumoja wa pori akapita pale na kukanyagakanyaga mubaruti ule.
19Sasa wewe Amazia unasema: ‘Nimewaua Waedomu’ na moyo unakufanya ujivune. Basi, ikaa ndani ya nyumba yako; kwa nini kujitafutia taabu zitakazokuangamiza wewe mwenyewe pamoja na watu wako wa Yuda?”
20Lakini Amazia hakujali kwa maana lilikuwa kusudi la Mungu apate kuwekwa katika mukono wa waadui zao kwa sababu alitegemea miungu ya Edomu.
21Kwa hiyo, Yoasi, mufalme wa Israeli akatoka akapambana uso kwa uso na Amazia, mufalme wa Yuda katika vita kule Beti-Semesi, katika inchi ya Yuda. Ang. 25.17
22Watu wa Yuda wakashindwa na watu wa Israeli na kila mumoja akarudia kwake.
23Halafu Yoasi mufalme wa Israeli alimukamata Amazia mufalme wa Yuda, mwana wa Yoasi, mwana wa Ahazia kule Beti-Semesi akamupeleka mpaka Yerusalema. Kule, akabomoa ukuta wa muji ule, kuanzia kwenye mulango wa Efuraimu mpaka kwenye mulango wa Pembeni, umbali wa karibu metre mia mbili.
24Akatwaa zahabu yote na feza hata na vifaa vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Yawe chini ya ulinzi wa Obedi-Edomu; vilevile akatwaa hazina ya nyumba ya kifalme mateka, kisha akarudi Samaria.
25Amazia mufalme wa Yuda aliishi miaka kumi na mitano nyuma ya kifo cha mufalme Yoasi mwana wa Yoahazi mufalme wa Israeli.
26Matendo mengine yote ya Amazia kutoka mwanzo mpaka mwisho yameandikwa katika Kitabu cha Wafalme wa Yuda na Israeli.
27Mashauri mabaya ya kumwua Amazia yalifanywa Yerusalema tangu alipomwacha Yawe, kwa hiyo akakimbilia Lakisi. Lakini waadui wakatuma watu Lakisi wakamwua kule.
28Maiti yake ikaletwa juu ya farasi, na kuzikwa kwenye makaburi ya kifalme katika muji wa Daudi.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.