1Akapanga wanaume elfu makumi saba kuwa wabebaji wa mizigo, elfu makumi nane kuwa wachongaji wa mawe kwenye milima na wengine elfu tatu mia sita kuwa wasimamizi wao.
2Kisha, Solomono akatuma ujumbe kwa Hiramu, mufalme wa Tiro, akamwambia: “Unitendee na mimi kama vile ulivyomutendea baba yangu Daudi, ulipomupelekea mierezi ya kujenga nyumba ya kifalme.
3Ninataka kujenga nyumba ya kumwabudia Yawe wangu. Nitaitakasa kwa ajili yake, nayo itakuwa pahali pa kufukiza ubani wenye harufu nzuri mbele yake, na vilevile pahali pa kumutolea mikate mitakatifu siku zote, na sadaka za kuteketezwa asubui na magaribi na za siku za Sabato, za Mwandamo wa Mwezi, na sikukuu zingine za Yawe, Mungu wetu, kama vile alivyoagiza Waisraeli milele.
4Nyumba ninayokusudia kujenga itakuwa kubwa sana, maana Mungu wetu ni mukubwa zaidi ya miungu yote.
5Lakini ni nani anayeweza kumujengea nyumba ikiwa mbingu zenyewe hazimutoshi, wala mbingu za juu sana? Nami ni nani basi, hata nimujengee nyumba isipokuwa tu kama pahali pa kufukizia ubani mbele yake? Ang. 1 Fal 8.27; 2 Sik 6.18
6Basi, sasa unitumie mutu mwenye ujuzi wa kutengeneza vyombo kwa zahabu, feza, shaba, na chuma, na nguo ya rangi nyekundu-nyeusi, za rangi nyekundu na ya samawi, anayejua vilevile kuchora. Yeye atashirikiana katika kazi hiyo na wafundi wanaokuwa pamoja nami katika Yuda na Yerusalema, ambao baba yangu Daudi aliwaweka.
7Tena unitumie miti ya mierezi, miberoshi na musandali kutoka Lebanoni, kwa maana ninajua kwamba watumishi wako ni hodari sana wa kupasua mbao kule Lebanoni. Nao watumishi wangu watashirikiana na watumishi wako,
8kusudi wanipasulie mbao kwa wingi, maana nyumba ninayokusudia kujenga ni kubwa na ya ajabu.
9Kwa ajili ya watumishi wako, ni kusema waseremala watakaopasua mbao, nitatoa toni mia mbili za ngano iliyopondwa, toni mia mbili za shayiri, litre elfu mia ine za divai na litre elfu mia ine za mafuta.”
10Naye Hiramu, mufalme wa Tiro, akamujibu Solomono kwa barua akisema: “Kwa sababu Yawe anawapenda watu wake, amekufanya kuwa mufalme wao.
11Atukuzwe Yawe, Mungu wa Israeli, aliyeumba mbingu na dunia! Amemupa mufalme Daudi mwana mwenye hekima, ufahamu na akili, atakayemujengea Yawe nyumba, na kujijengea nyumba ya kifalme.
12Sasa ninakutumia fundi mwenye ujuzi sana na mwenye akili, jina lake Huruma-Abi.
13Mama yake ni wa kabila la Dani, na baba yake ni wa Tiro. Yeye ana ujuzi mwingi wa kazi ya zahabu, feza, shaba, chuma, mawe, miti, nguo ya rangi nyekundu-nyeusi, ya samawi, ya nyekundu na ya kitani safi. Tena ni hodari na anaweza kuchora kila aina ya michoro kufuatana na maelezo yoyote ambayo angepewa. Yeye atafanya kazi pamoja na wafundi wako, wafundi wa bwana wangu, Daudi baba yako.
14Sasa basi, bwana wangu, tafazali ututumie sisi watumishi wako vitu ulivyosema: ngano, shayiri, mafuta na divai.
15Nasi tutapasua mbao kadiri ya mahitaji yako kutoka kule Lebanoni. Kisha tutazifunga pamoja kwa njia ya bahari zielee mpaka Yopa. Kutoka kule utazipeleka Yerusalema.”
16Mufalme Solomono akawahesabu wageni wote waliokuwa katika inchi ya Israeli. Hesabu hii ni kama ile Daudi baba yake aliyofanya. Kulikuwa wageni yapata elfu mia moja makumi tano na tatu na mia sita.
17Kati yao akawapa watu elfu makumi saba kazi ya kubeba mizigo, watu elfu moja wakakuwa wachongaji wa mawe kwenye milima, na watu elfu tatu mia sita wakakuwa wasimamizi kusudi wawasukume watu kufanya kazi.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.