1Kwa ajili ya Sayuni sitakaa kimya,
kwa ajili ya Yerusalema sitatulia,
mpaka kuokolewa kwake kuonekane kama umeme,
wokovu wake utokee kama mwangaza.
2Mataifa watauona wokovu wako,
wafalme wote watauona utukufu wako.
Nawe utaitwa kwa jina jipya
ambalo litapangwa na Yawe mwenyewe.
3Utakuwa taji zuri katika mukono wa Yawe;
taji la kifalme katika mukono wa Mungu wako.
4Hautaitwa tena: Aliyeachwa,
wala inchi yako haitaitwa: “Ukiwa”.
Lakini utaitwa: “Ninamufurahia”,
na inchi yako itaitwa: “Aliyeolewa”.
Maana Yawe amependezwa nawe,
naye atakuwa kama mume wa inchi yako.
5Maana kama vile kijana mwanaume anavyomwoa binti,
ndivyo aliyekujenga atakavyokuwa mume wako.
Kama bwana arusi anavyofurahi juu ya bibi arusi,
ndivyo Mungu atakavyofurahi juu yako.
6Juu ya kuta zako, ee Yerusalema, nimeweka walinzi,
usiku na muchana hawatakaa kimya hata kidogo.
Enyi munaomukumbusha Yawe ahadi yake,
musikae kimya;
7musimupe hata nafasi ya kupumzika,
mpaka atakapousimika Yerusalema,
na kuufanya kuwa wenye sifa katika ulimwengu wote.
8Yawe ameapa kwa uwezo wake mukubwa,
ameapa kwa nguvu yake akisema:
Sitawapa tena waadui zako ngano yako;
wala wageni hawatakunywa tena divai yako
ambayo umeitoshea jasho.
9Lakini ninyi muliovuna ngano hiyo,
mutaikula na kunitukuza mimi Yawe.
Ninyi muliochuma mizabibu hiyo,
mutakunywa divai yake katika viwanja vya hekalu langu takatifu.
10Enyi wakaaji wa Yerusalema, mutoke, mutoke inje ya muji,
muwatayarishie njia watu wenu wanaorudia!
Mujenge! Mujenge barabara na kuondoa mawe yote!
Muweke bendera kuwa kitambulisho kwa ajili ya watu.
11Yawe ametangaza katika dunia yote,
muwaambie watu wa Sayuni hivi:
Mukombozi wenu anakuja,
yeye anakuja na mapato yake,
anafika na mushahara wake.
12Ninyi mutaitwa: Watu Watakatifu,
Watu waliokombolewa na Yawe.
Nawe Yerusalema utaitwa: Muji Mungu anaoupenda,
Muji ambao Mungu hakuuacha.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.