2 Wafalme 22 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mufalme Yosia wa Yuda(2 Sik 34.1-2)

1Yosia alikuwa na umri wa miaka minane alipoanza kutawala akiwa kule Yerusalema na utawala wake ulidumu kwa miaka makumi tatu na mumoja. Mama yake aliitwa Yedida, binti wa Adaya mukaaji wa muji wa Bozikati.

2Yosia alitenda kwa usawa mbele ya Yawe. Alifuata mienendo yote ya babu yake Daudi; hakuiacha hata kidogo.

Kitabu cha sheria kinaonekana(2 Sik 34.8-28)

3Katika mwaka wa kumi na nane wa utawala wake, mufalme alimutuma Safanu mwana wa Azalia, mujukuu wa Mesulamu, mwandishi katika nyumba ya Yawe akisema:

4“Kwenda kwa Kuhani Mukubwa Hilkia kusudi ahesabu feza zilizoletwa katika nyumba ya Yawe, ambazo walinzi wa mulango walizikusanya kutoka kwa watu;

5nazo zitolewe kwa wale wanaosimamia kazi ya kutengeneza vizuri nyumba ya Yawe kusudi wapate kuwalipa wafundi wanaofanya kazi ya kutengeneza mabomoko,

6waseremala, wajengaji na watumishi wengine wenye kujenga, na kununua mbao na mawe yaliyochongwa kwa ajili ya kutengeneza nyumba.

7Watu wanaosimamia ujenzi wasiombwe kutoa hesabu ya matumizi ya feza watakazopewa, kwa sababu wanazitumia kwa uaminifu.”

8Kisha Kuhani Mukubwa Hilkia akamwambia Safanu, mwandishi: “Nimekipata kitabu cha Sheria katika nyumba ya Yawe.” Halafu Hilkia akamupatia Safanu kitabu, naye akakisoma.

9Mwandishi Safanu akamwendea mufalme na kutoa habari, akisema: “Watumishi wako wametoa feza zilizopatikana katika nyumba, halafu wakazipeleka kwa wafundi wanaosimamia kazi ya kutengeneza nyumba ya Yawe.”

10Kisha Safanu, mwandishi akamwambia mufalme: “Kuhani Hilkia amenipa kitabu.” Naye Safanu akakisoma mbele ya mufalme.

11Mufalme aliposikia maneno ya Kitabu cha Sheria, akapasua nguo zake.

12Akaamuru kuhani Hilkia, Ahikamu mwana wa Safanu na Akibori mwana wa Mikaya pamoja na mwandishi Safanu na Asaya mutumishi wa mufalme, akisema:

13“Mwende muombe shauri kutoka kwa Yawe kwa ajili yangu, na kwa watu wa Yuda wote juu ya maneno ya kitabu hiki kilichopatikana kwa sababu kasirani ya Yawe imewaka juu yetu, maana babu zetu hawakutii maneno ya kitabu hiki na kutimiza yote yaliyoandikwa juu yetu.”

14Kwa hiyo kuhani Hilkia, Ahikamu, Akibori, Safanu na Asahiya, wote walikwenda kuomba shauri kwa mwanamuke mumoja nabii jina lake Hulda aliyekuwa muke wa Salumu mwana wa Tikwa, mujukuu wa Harihasi, mutunza nguo za hekalu. Wakati ule, Hulda alikuwa anaishi katika mutaa wa pili wa Yerusalema, nao wakazungumuza naye.

15Basi akawaambia: “Hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli, anavyosema: Mumwambie yule aliyewatuma kwangu,

16Yawe anasema hivi: Nitaleta uovu juu ya pahali hapa na juu ya wakaaji wake kama vile inavyokuwa katika kitabu kilichosomwa na mufalme wa Yuda.

17Kwa sababu wameniacha na kufukizia miungu mingine ubani kusudi watu wanikasirikishe kwa kazi zote za mikono yao, basi, kasirani yangu juu ya Yerusalema itawaka na haitaweza kutulizwa.

18Lakini juu ya mufalme wa Yuda aliyewatuma kuomba shauri la Yawe, mumwambie kwamba, hivi ndivyo Yawe, Mungu wa Israeli anavyosema juu ya maneno uliyoyasikia.

19Wakati uliposikia niliyosema juu ya pahali hapa na juu ya wakaaji wake, kwamba watakuwa ukiwa na kulaaniwa, ulijuta na kunyenyekea mbele yangu, hata ukapasua nguo yako na kulia mbele yangu. Basi, nami vilevile nimekusikia.

20Kwa hiyo, nitakukusanya pamoja na babu zako nawe utazikwa katika kaburi kwa amani, macho yako hayataona uovu nitakaoleta juu ya pahali hapa.” Basi wajumbe wakamuletea mufalme Yosia habari hii.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help