Matendo ya Mitume 19 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Paulo anahubiri katika Efeso

1Wakati Apolo alipokuwa Korinto, Paulo akasafiri akipitia katika inchi ya vilima na kufika Efeso. Kule akakuta wanafunzi wamoja;

2akawauliza: “Ninyi mulipokea Roho Mutakatifu wakati mulipoamini?”

Nao wakamujibu: “Hapana! Hatujasikia hata kidogo kwamba kuko Roho Mutakatifu.”

3Halafu Paulo akawauliza: “Basi mulibatizwa kwa ubatizo gani?”

Wakamujibu: “Tulibatizwa kwa ubatizo wa Yoane.”

4Paulo akawaambia: “Yoane aliwabatiza wale waliogeuka toka zambi zao na kuwaambia Waisraeli kwamba wamwamini yule atakayekuja nyuma yake, naye ndiye Yesu.”

5Waliposikia maneno haya, walibatizwa kwa jina la Bwana Yesu.

6Paulo akaweka mikono yake juu yao, na Roho Mutakatifu akashuka juu yao, nao wakaanza kusema kwa luga na kutabiri.

7Wote walikuwa kadiri ya watu kumi na wawili.

8Kwa muda wa miezi mitatu Paulo alikuwa akiingia katika nyumba ya kuabudia na kuhubiri watu kwa uhodari. Akabishana nao juu ya habari za Ufalme wa Mungu, akitaka wazisadiki.

9Lakini wamoja wakakuwa na mioyo migumu hata wakakataa kuamini, wakaanza kusema vibaya juu ya Njia ya Bwana mbele ya mukutano. Kwa hiyo Paulo akajitenga nao, akaenda na wanafunzi peke yao. Na kila siku alibishana na watu katika chumba cha kufanyia usomi cha mutu mumoja aliyeitwa Tirano.

10Mambo haya yakaendelea kwa muda wa miaka miwili hata Wayuda na Wagriki wote waliokaa katika jimbo la Azia wakasikia neno la Bwana.

Wana wa Sikewa wanajaribu kufukuza pepo

11Mungu akaendelea kufanya miujiza ya ajabu kwa njia ya Paulo.

12Na hata watu walitwaa vitambaa na nguo zilizogusa mwili wa Paulo, wakazipeleka kwa wagonjwa, nao wakapona na pepo wakatoka ndani yao.

13Na kulikuwa Wayuda wamoja waliotangatanga huku na huko kwa kufukuza pepo. Watu wale wakajaribu vilevile kutaja jina la Bwana Yesu, wakiwaambia vilevile pepo: “Ninawaamuru muondoke kwa jina la Yesu, yule anayehubiriwa na Paulo.”

14(Waliofanya hivi walikuwa wana saba wa Sikewa, Kuhani Mukubwa mumoja wa Wayuda.)

15Lakini yule pepo akawajibu: “Ninamujua Yesu na ninamufahamu Paulo, lakini ninyi ni nani?”

16Na yule mutu aliyekuwa na pepo ndani yake akawarukia, akawashinda wote nguvu na kuwatendea vibaya hata wakakimbia toka nyumba yake wakiwa uchi na wakijaa vidonda.

17Wakaaji wote wa Efeso, Wayuda na Wagriki wakajua habari hii. Halafu wote wakashikwa na woga na wakalitukuza jina la Bwana Yesu.

18Wengi kati ya wale walioamini walikuja kuungama na kutangaza waziwazi mambo waliyofanya.

19Na watu wengi kati ya wale waliofanya mambo ya uchawi wakaleta vitabu vyao vya uganga na wakavichoma mbele ya watu wote. Bei ya vitabu vile ilipohesabiwa, ikafikia vikoroti vya feza elfu makumi tano.

20Ni hivi neno la Bwana lilivyoendelea kuenea fasi zote kwa uwezo wake na kuzidi kuonekana kuwa lenye nguvu.

Fujo inatokea Efeso

21Nyuma ya mambo yale, Paulo alikusudia kwenda Yerusalema, akipitia katika inchi ya Makedonia na katika jimbo la Akaya. Akasema: “Nikisha kufika kule, ni lazima niende Roma vilevile.”

22Halafu akawatuma wawili kati ya wasaidizi wake, Timoteo na Erasto watangulie kwenda Makedonia. Yeye mwenyewe akabaki tena kwa muda katika jimbo la Azia.

23Katika siku zile kulitokea fujo kubwa kwa ajili ya Njia ya Bwana.

24Kulikuwa fundi mumoja wa kufua feza, jina lake Demetrio. Alikuwa akitengeneza sanamu ndogo za feza zinazofanana na hekalu la mungu muke Artemi. Na kwa njia ile aliwapatia wafundi faida kubwa.

25Yeye alikusanya wale wafundi wote pamoja na watu wengine waliofanya kazi sawasawa na ile na kuwaambia: “Wandugu, munajua kwamba sisi tunapata mali mengi kwa njia ya kazi hii.

26Sasa ninyi wenyewe munaona na kusikia namna huyu Paulo anayofanya. Amekwisha kuwavuta na kuwaonya watu wengi, si hapa Efeso tu, lakini ni karibu katika jimbo lote la Azia. Anasema kwamba miungu inayotengenezwa na watu si miungu hata kidogo.

27Hivi kunakuwa hatari, na si kwa kazi hii yetu kuzarauliwa tu, lakini vilevile hekalu la mungu mukubwa muke, Artemi, litahesabiwa kuwa kitu bure. Na tena utukufu wake utapunguka, yeye anayeabudiwa na watu wote wa Azia na dunia nzima!”

28Watu wale waliposikia maneno haya, wakajaa na hasira na kuanza kulalamika wakisema: “Artemi wa Waefeso atukuzwe!”

29Fujo ikajaa katika muji wote. Wale watu wakawakamata wanainchi wa Makedonia, Gayo na Aristarko waliokuwa wakisafiri pamoja na Paulo. Nao wote pamoja wakawapeleka kwa haraka katika nyumba ya makutano.

30Paulo alitaka kujionyesha mbele ya lile kundi la watu, lakini wanafunzi wakamukataza.

31Hata wakubwa wamoja wa jimbo la Azia, waliokuwa warafiki zake wakamutumia ujumbe wakimusihi kwamba asiingie ndani ya nyumba ile.

32Wakati ule, mukutano ulikuwa umejaa fujo kwa sababu watu wamoja walikuwa wakilalamika na kusema hivi na wengine hivi, na wengi kati yao hawakujua hata ni kwa sababu gani walikusanyika.

33Watu wamoja katika mukutano wakaeleza mambo yaliyotokea kwa Alesanduro, yeye aliyesukumwa na Wayuda kwenda kusema mbele ya watu. Basi Alesanduro akainua mukono kwa kuwanyamazisha watu, kwa maana alitaka kujitetea mbele yao.

34Lakini walipotambua kwamba yeye ni Muyuda, wakalalamika wote pamoja kwa muda wa saa mbili, wakisema: “Artemi wa Waefeso atukuzwe!”

35Kwa mwisho katibu mukubwa wa muji akawatuliza watu, akisema: “Ninyi wanainchi wenzangu wa Efeso, watu wote wanajua kwamba ni wakaaji wa Efeso ndio wanaoshugulika na kulinda hekalu la mungu Artemi na sanamu yake iliyoshuka toka mbinguni.

36Basi kwa maana hakuna anayeweza kukana maneno haya, ni lazima mutulie, wala musifanye kitu chochote kwa haraka.

37Kwa maana mumewaleta watu hawa hapa, ingawa hawakuiba vitu vya hekalu, wala kumutukana mungu wetu.

38Basi ikiwa Demetrio na wafundi wenzake wanakuwa na mashitaki juu ya mutu fulani, tuko na tribinali na wakubwa wako pale. Wanaweza kupeleka mashitaki yao kule!

39Na kama mukiwa na neno lingine, litakatwa katika mukutano ulioruhusiwa.

40Kwa maana kufuatana na mambo yaliyotukia leo, tunaweza kushitakiwa kwamba tumeleta fujo. Tena hakuna neno tunaloweza kusema kwa kueleza sababu ya kufanya mukutano huu.”

41Kisha kusema maneno haya, akaaga mukutano.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help