Walawi 22 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Utakatifu wa sadaka

1Yawe akamwambia Musa:

2Umwambie Haruni na wana wake makuhani waheshimu vitu ambavyo Waisraeli wametakasa kwa ajili yangu, kusudi wasichafue jina langu takatifu. Mimi ni Yawe.

3Uwaambie hivi: Kama mumoja wa wazao wenu katika vizazi vyenu vyote akikaribia vitu vitakatifu ambavyo Waisraeli wamevitakasa kwa ajili yangu mimi Yawe akiwa muchafu, mutu huyu atatengwa nami. Mimi ni Yawe.

4Mutu yeyote wa kizazi cha Haruni akiwa na ugonjwa wa ukoma au anatokwa usaha asikule vitu vitakatifu mpaka atakapokuwa safi. Mutu yeyote akigusa mutu aliyejichafua kwa kugusa maiti au mutu aliyetokwa na mbegu za uzazi,

5au akigusa kiumbe chochote chenye kutambaa ambacho kinamufanya mutu kuwa muchafu au mutu ambaye anaweza kumuchafua wa aina yoyote,

6mutu huyu, atakuwa muchafu mpaka magaribi na haruhusiwi kula vyakula vitakatifu mpaka pale atakapokuwa ameoga.

7Jua litakapotua ndipo atakapokuwa safi. Nyuma ya pale ataweza kula vyakula vitakatifu maana hicho ndicho chakula chake.

8Kuhani asikule nyama yoyote ya nyama aliyekufa peke yake au kuuawa na nyama wa pori, kusudi asijichafue. Mimi ni Yawe.

9Kwa hiyo, makuhani washike agizo langu, kusudi wasifanye zambi na kuuawa. Mimi Yawe ndiye ninayewatakasa.

10Mutu asiyekuwa wa ukoo wa makuhani haruhusiwi kula chakula kitakatifu. Hata mugeni wa kuhani au mutumishi wake haruhusiwi kula.

11Lakini kama kuhani amenunua mutumwa kwa kuwa mali yake, basi, yule mutumwa anaruhusiwa kula na vilevile wale waliozaliwa katika nyumba yake.

12Kama binti ya kuhani ameolewa na mutu asiyekuwa kuhani, haruhusiwi kula sadaka ya vitu vitakatifu.

13Lakini kama binti ya kuhani ni mujane au amefukuzwa na mume wake na hana mutoto, naye amerudi kwa baba yake na kukaa naye kama vile alipokuwa kijana, basi, anaweza kula chakula cha baba yake. Hata hivyo, mugeni haruhusiwi kula chakula hicho.

14Kama mutu mwingine akikula chakula kitakatifu bila kujua, basi, atalipa nyongezo ya sehemu moja ya tano pamoja na kipimo sawasawa alichokula na kumurudishia kuhani.

15Kuhani asichafue vitu ambavyo Waisraeli wamemutolea Yawe

16na hivyo kufanya watu wabebe sababu ya uovu na makosa yao kwa kula vitu vyao vitakatifu. Mimi Yawe ndiye ninayetakasa vitu hivyo.

17Yawe akamwambia Musa:

18Umwambie Haruni na wana wake makuhani na Waisraeli wote hivi: Kama mutu yeyote kati yenu au mugeni yeyote anayeishi katika Israeli akitoa sadaka yake, ikuwe ni ya kutimiza kiapo au sadaka ya mapenzi ya kumutolea Yawe kwa kuteketezwa,

19kusudi apate kukubalika, atatoa katika ngombe dume au katika kondoo beberu asiyekuwa na kilema.

20Inakatazwa kutoa chochote kinachokuwa na kilema maana hakitakubaliwa kwa faida yenu.

21Mutu yeyote anapomutolea Yawe sadaka ya amani kwa kutimiza kiapo au sadaka ya mapenzi kutoka katika kundi lake la mifugo, kusudi akubaliwe anapaswa kuwa nyama mukamilifu, nyama huyo asikuwe na kilema chochote.

22Usimutolee Yawe nyama yeyote anayekuwa kipofu, kilema, aliyevunjika, anayetokwa na usaha, mwenye upele au ukurutu, wala usiwatoe kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto juu ya mazabahu ya Yawe.

23Ngombe dume au mwana-kondoo anayekuwa na kiungo kimoja kirefu au kifupi kuliko kawaida wanaweza kumutoa sadaka ya mapenzi. Lakini huyo usimutoe kuwa sadaka ya kutimiza kiapo.

24Nyama ambaye kiungo chake cha uzazi kimeumizwa, kimepondwa, kimevunjwa au kimekatwa, usimutolee Yawe wala kumutoa kama vile sadaka katika inchi yako.

25Wala usipokee kutoka kwa wageni nyama wa namna hiyo na kunitolea mimi Mungu wako kama chakula. Nyama hao wana kilema kwa vile wamekatwa na hawatakubaliwa kwa faida yenu.

26Yawe akamwambia Musa:

27Ngombe dume, kondoo dume au beberu akizaliwa atabaki na mama yake kwa siku saba. Lakini tangu siku ya nane anaweza kutolewa kwa Yawe kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto.

28Lakini usichinje ngombe au kondoo siku moja pamoja na kitoto chake.

29Utakaponitolea mimi Yawe sadaka ya shukrani utaitoa kwa namna ambayo itakufanya ukubaliwe.

30Nyama huyo ni lazima akuliwe siku hiyohiyo. Musiache kitu mpaka kesho yake asubui. Mimi ni Yawe.

31Kwa hiyo mutashika na kutimiza amri zangu. Mimi ni Yawe.

32Musichafue jina langu takatifu, maana ni lazima niheshimiwe kati ya watu wa Israeli. Mimi Yawe ndiye ninayewatakasa.

33Ni mimi niliyewatoa katika inchi ya Misri kusudi nikuwe Mungu wenu. Mimi ni Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help