Waamuzi 17 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Sanamu za Mika

1Kulikuwa mutu mumoja kule katika milima ya Efuraimu, jina lake Mika.

2Siku moja akamwambia mama yake: “Vile vikoroti vya feza elfu moja na mia moja ulivyoibiwa, nawe ukamulaani aliyekuiba nami nikiwa ninasikia, mimi niko navyo. Mimi ndiye niliyevibeba.” Mama yake akasema: “Mwana wangu ubarikiwe na Yawe.”

3Mika akamurudishia mama yake hivyo vikoroti vya feza elfu moja na mia moja. Mama yake akasema: “Kusudi laana niliyotoa isikupate, feza hii ninaitoa kwa Yawe kwa kutengeneza sanamu ya kuchonga na ya kuyeyushwa. Sasa ninakurudishia vikoroti vya feza.”

4Mika alipomurudishia mama yake hiyo feza, mama yake akatwaa vikoroti vya feza mia mbili akamupatia mufua feza ambaye alifua sanamu ya kuchonga na ya kuyeyushwa. Sanamu hiyo ikawekwa katika nyumba ya Mika.

5Mutu huyo, Mika alikuwa na pahali pake pa ibada. Alitengeneza kizibao cha kuhani na sanamu, kisha akamufanya mumoja wa watoto wake kuwa kuhani wake.

6Siku hizo hakukukuwa mufalme katika Israeli. Kila mutu alifanya chochote alichotaka.

7Wakati ule kulikuwa kijana mumoja Mulawi katika muji wa Betelehemu katika inchi ya Yuda.

8Kijana huyo akaondoka Betelehemu katika inchi ya Yuda, akaenda kutafuta pahali pengine pa kuishi. Katika safari yake akafika katika nyumba ya Mika katika inchi ya milima ya Efuraimu.

9Mika akamwuliza: “Umetoka wapi?” Naye akamujibu: “Mimi ni Mulawi, kutoka katika muji wa Betelehemu katika inchi ya Yuda. Nitakaa popote nitakapopata nafasi ya kukaa kama mugeni.”

10Mika akamwambia: “Kaa pamoja nami, ukuwe kwangu kama baba na kuhani wangu. Nitakulipa vikoroti kumi vya feza kila mwaka na nguo pamoja na mahitaji yako.”

11Yule Mulawi akakubali, akakaa kule na kuwa kama mumoja wa wana wa Mika.

12Naye Mika akamufanya kijana huyo Mulawi kuwa kuhani wake kule katika nyumba yake.

13Kisha akasema: “Sasa ninajua kwamba Yawe atanifanikisha maana nina kijana huyu Mulawi kama kuhani wangu.”

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help