Walawi 1 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Sadaka za kuteketezwa

1Yawe akamwita Musa na kuongea naye katika hema la mukutano, akamwambia:

2Uwaambie Waisraeli kwamba kama mutu anapenda kumutolea Yawe sadaka ya nyama, nyama huyo atamuchagua kutoka kundi lake la ngombe, kondoo au mbuzi.

3Kama sadaka mutu anayotoa ni ya kuteketezwa kwa moto, atamuchagua nyama dume asiyekuwa na kilema kutoka kundi lake, atamutolea mbele ya mulango wa hema la mukutano kusudi apate kukubaliwa na Yawe;

4ataweka mukono wake juu ya kichwa cha nyama wa sadaka ya kuteketezwa kwa moto, ambayo itakubaliwa kwa ajili ya kumufanyia huyo mutu upatanisho.

5Kisha, atamuchinja huyo ngombe mbele ya Yawe. Nao makuhani wazao wa Haruni wataichukua damu na kuinyunyizia mazabahu inayokuwa kwenye mulango wa hema la mukutano, pande zake zote.

6Huyo mutu atachuna huyo nyama wa sadaka ya kuteketezwa na kumukata vipandevipande.

7Hao makuhani wazao wa Haruni watazipanga kuni juu ya mazabahu na kuwasha moto.

8Kisha makuhani hao watatwaa vile vipande vya nyama, kichwa na mafuta, na kuviweka juu ya kuni juu ya mazabahu.

9Lakini matumbotumbo na miguu ya nyama yule vitasafishwa kwa maji. Kuhani atateketeza sadaka yote juu ya mazabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe.

10Kama sadaka yake ya kuteketezwa ataitwaa katika kundi la kondoo au mbuzi, basi atachagua dume asiyekuwa na kilema.

11Atamuchinjia upande wa kaskazini wa mazabahu, mbele ya Yawe, hao makuhani wazao wa Haruni watainyunyizia mazabahu damu pande zake zote.

12Kisha yule mutu atamukata vipandevipande, akivitenga kichwa pamoja na mafuta yake, na kuhani ataviweka kwenye moto juu ya mazabahu.

13Lakini matumbotumbo na miguu yake atavisafisha kwa maji. Kuhani ataiteketeza yote juu ya mazabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe.

14Ikiwa anamutolea Yawe sadaka ya kuteketezwa ya ndege, basi, ataleta sadaka yake ya hua au kitoto cha njiwa.

15Kuhani ataleta ndege huyo kwenye mazabahu, atakongonyoa kichwa chake na kukiteketeza juu ya mazabahu. Damu yake itanyunyiziwa kwenye ubavu wa mazabahu.

16Kibofu chake pamoja na uchafu wake ataviondoa na kuvitupa upande wa mashariki wa mazabahu ambako majivu yanawekwa.

17Atamushika mabawa na kumupasua, lakini asimwachanishe vipande viwili. Kisha, kuhani atamuteketeza kwenye mazabahu, juu ya kuni. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help