2 Wafalme 19 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mufalme anaomba shauri kwa Isaya(Isa 37.1-7)

1Mufalme Hezekia aliposikia habari hiyo, alipasua nguo yake, akavaa nguo ya gunia, akaingia katika nyumba ya Yawe.

2Aliwaamuru Eliakimu, musimamizi wa nyumba ya kifalme, Sebuna mwandishi, na wazee wa makuhani, wamwendee nabii Isaya mwana wa Amozi, wakiwa wamevaa nguo za magunia.

3Nao wakamwambia Isaya: “Hezekia anasema hivi: ‘Leo ni siku ya huzuni, ya kuazibiwa na ya kuzarauliwa. Sisi tumekuwa kama mwanamuke anayetaka kuzaa mutoto, lakini hana nguvu ya kumuzaa.

4Labda Yawe, Mungu wako, alisikia maneno ya yule jemadari ambaye ametumwa na bwana wake mufalme wa Asuria, kwa kumutukana Mungu Mwenye Uzima, naye Yawe, Mungu wako atamwazibu kwa ajili ya maneno aliyosikia. Uwaombee watu wanaobaki.’ ”

5Basi, hao watumishi wa mufalme Hezekia walipokwisha kufika kwa Isaya,

6aliwaambia: “Mumwambie bwana wenu kwamba Yawe anasema hivi: ‘Usiogope kwa sababu ya maneno uliyoyasikia, ambayo watumishi wa mufalme wa Asuria wameyasema kwa kunitusi.

7Sikia, nitamufanya mufalme asikie uvumi, halafu atarudi katika inchi yake, na kule nitamufanya auawe kwa upanga.’ ”

Kitisho kingine cha Waasuria(Isa 37.8-20)

8Kisha yule jemadari aliposikia kwamba mufalme wa Asuria alikuwa ameondoka Lakisi, aliondoka na kumukuta akishambulia muji wa Libuna.

9Halafu mufalme alipata habari kwamba Tiraka mufalme wa Etiopia anakuja kupigana naye. Akatuma wajumbe kwa Hezekia, akisema:

10“Mumwambie Hezekia mufalme wa Yuda: ‘Usikubali Mungu wako unayemutegemea akudanganye kwa kukuahidi kwamba Yerusalema hautatekwa na mufalme wa Asuria.

11Wewe umekwisha kusikia jinsi wafalme wa Asuria walivyotendea inchi nyingine na kuziangamiza kabisa. Unazani wewe utaokoka?

12Miungu ya mataifa iliokoa Gozani, Harani, na Resefu na Waedeni waliokaa Telasari, mataifa ambayo babu zangu waliyaangamiza?

13Wako wapi wafalme wa Hamati, Arpadi, Sefarwaimu, Hena na Iwa?’ ”

14Mufalme Hezekia alipokea barua kutoka kwa wajumbe na kuisoma. Kisha akaenda na kuingia katika nyumba ya Yawe, akaiweka mbele ya Yawe.

15Halafu akamwomba Yawe akisema: “Ee Yawe, Mungu wa Israeli, unayeikaa katika kiti cha kifalme juu ya makerubi, ni wewe tu unayekuwa Mungu, unayetawala falme zote za ulimwengu. Wewe uliumba dunia na mbingu.

16Ee Yawe, fumbua macho uone, tega sikio lako uyasikie matusi yote ambayo Saniharibu amepeleka kukutukana wewe Mungu Mwenye Uzima.

17Ee Yawe, ni kweli kwamba wafalme wa Asuria wameangamiza mataifa na inchi zao.

18Walitupa miungu yao katika moto kwa sababu haikukuwa miungu ya kweli, lakini sanamu za miti na mawe zilizochongwa na mikono ya watu.

19Sasa, ee Yawe, Mungu wetu, utuokoe toka katika makucha ya Saniharibu, kusudi falme zote za dunia zijue kwamba ni wewe tu, ee Yawe peke yako, ee Yawe, ambaye ni Mungu.”

Ujumbe wa Isaya kwa mufalme(Isa 37.21-38)

20Kisha Isaya mwana wa Amozi akatuma ujumbe kwa Hezekia, akisema: “Yawe, Mungu wa Israeli anasema hivi: Nimesikia ombi lako kwangu juu ya Saniharibu mufalme wa Asuria.

21Hili ndilo neno Yawe alilosema juu yake:

“Watu wa Sayuni wanakuzarau kabisa,

watu wa Yerusalema wanakutikisia kichwa kwa kukuchekelea.

22Wewe umemutukana nani?

Umemutusi nani?

Umesubutu kumufokea nani kwa majivuno?

Ni Mungu, Mutakatifu wa Israeli!

23Umewatuma watumishi wako kuchekelea Yawe;

wewe umesema: Kwa magari yangu mengi ya vita,

nimefika juu kwenye vichwa vya milima,

mpaka kwenye vichwa vya milima ya Lebanoni.

Nimeangusha mierezi yake mirefu,

na misunobari mizurimizuri.

Nimevifikia vichwa vyake

na ndani ya pori zake kubwa.

24Nimechimba visima na kunywa maji ya kigeni,

nilikausha vijito vya Misri

kwa miguu yangu.

25Haujasikia, ewe Saniharibu, kwamba

mimi Yawe nilipanga jambo hili tangu zamani?

Ninachotimiza sasa nilikipanga zamani.

Nilikuweka uifanye miji yenye kuzungukwa na kuta

kuwa lundo la mabomoko.

26Wakaaji wake wakiwa wameishiwa nguvu,

wametishika na kufazaika,

wamekuwa kama mimea ya shamba,

kama majani changa,

kama majani yanayoota juu ya paa,

yanayokauka mbele ya kukomaa.

27Lakini, ninakujua wewe Saniharibu;

ninajua wakati unaikaa, wakati unatoka, na wakati unaingia;

ninajua vilevile wakati kasirani yako inawaka juu yangu.

28Kwa vile umefanya mipango juu yangu

na nimesikia majivuno yako,

nitatia ndoana yangu ndani ya pua yako,

na lijamu yangu ndani ya kinywa chako.

Nitakurudisha katika njia ileile uliyokuja ndani yake.

29“Na hiki ndicho kitakuwa kitambulisho kwako Hezekia: Mwaka huu na mwaka unaokuja mutakula kinachoota chenyewe bila kupandwa. Lakini katika mwaka wa tatu mutapanda na kuvuna mavuno; mutapanda mizabibu na kula matunda yake.

30Wale watakaobaki katika ukoo wa Yuda wataongezeka na kuwa wengi kama vile muti unavyotoa mizizi yake katika udongo na kuzaa matunda juu.

31Maana kutakuwa watu watakaobaki kule Yerusalema; kule kwenye mulima Sayuni kutakuwa watu wachache watakaobakia. Yawe wa majeshi amekusudia kukamilisha hayo.

32“Yawe anasema hivi juu ya mufalme wa Asuria: Hataingia katika muji huu, wala kuupiga mushale, wala kuingia akishika ngao, wala hatalundika udongo kandokando yake apate kuubomoa.

33Atarudi kwa njia ileile aliyokuja nayo wala hataingia katika muji huu. –Ni ujumbe wa Yawe.–

34Kweli, kwa ajili ya heshima yangu mimi na kwa ajili ya mutumishi wangu Daudi, nitaulinda na kuukoa muji huu.”

35Basi, malaika wa Yawe aliingia ndani ya kambi ya Waasuria na kuwaua watu elfu mia moja makumi nane na watano. Kesho yake, wakati watu walipoamuka, waliona yale maiti yote.

36Kisha Saniharibu mufalme wa Asuria akaondoka, akaenda kwake, akakaa Ninawe.

37Siku moja wakati Saniharibu alipokuwa akiabudu katika nyumba ya Nisiroki mungu wake, wana wake wawili, Adarameleki na Sarezeri walimwua kwa upanga, halafu wakakimbilia katika inchi ya Ararati. Halafu mwana wake Esari-Hadoni akatawala kwa pahali pake.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help