Yobu 31 - Swahili Congo Revised Bible 2002

1Nimejizuiza kabisa mimi mwenyewe,

macho yangu yasimwangalie binti kwa tamaa.

2Au, ninangojea nini kutoka kwa Mungu anayekuwa juu?

Mungu Mwenye Uwezo ameniwekea kitu gani?

3Hasara haipati watu waovu

na maangamizi wale wanaotenda mabaya?

4Mungu haoni njia zangu

na kujua hatua zangu zote?

5-6Mungu anipime katika mizani ya haki,

naye ataona kwamba sina kosa.

Kama nimeishi kwa kufuata uongo,

kama nimekimbilia kudanganya watu,

7kama hatua zangu zimepotoka

nao moyo wangu ukafuata tamaa za macho yangu,

kama mikono yangu imechafuliwa na zambi,

8basi nipande na mwingine akule,

mazao yangu ya shamba yaongolewe.

9Kama moyo wangu umevutwa kwa muke wa mutu,

kama nimevizia kwenye mulango wa jirani yangu,

10basi, muke wangu amupikie mume mwingine,

na wanaume wengine walale naye.

11Jambo hilo ni kosa la kuchukiza,

uovu ambao mwamuzi anapaswa kuazibu.

12Kosa langu lingekuwa kama vile moto

wa kuniteketeza na kuangamiza,

na kuchoma kabisa mapato yangu yote.

13Kama nimekataa maneno ya mutumishi au mujakazi wangu,

waliponiletea malalamiko yao,

14nitafanya nini basi Mungu atakaposimama mbele yangu?

Akinichunguza, nitamujibu nini?

15Maana Mungu ndiye aliyeniumba mimi na mutumishi wangu;

yeye ndiye aliyetuumba sisi wote.

16Nimepata kumukatalia masikini mahitaji yake

au kuwafanya wajane watumaini bure?

17Nimekula chakula changu peke yangu,

bila kuwaachia wayatima nao wapate kitu chochote?

18Hapana! Tangu ujana wangu nimekuwa baba yao aliyewalea,

tangu utoto wangu nimewaongoza wajane.

19Nilipoona mutu anakufa kwa kukosa nguo,

au masikini ambaye hana nguo ya kuvaa,

20nilimupa joto kwa nguo za manyoya ya kondoo wangu

naye akanitakia baraka za shukrani ya moyo.

21Kama nimekunjia yatima ngumi katika tribinali

nikijua nitapendelewa na waamuzi,

22basi, bega langu liongoke,

mukono wangu ukwanyuke kwenye maungio yake.

23Maana hasara kutoka kwa Mungu ni kitisho kwangu;

mimi siwezi kusimama mbele ya ukubwa wake.

24Sikuweka tumaini langu katika zahabu,

sikuiambia zahabu safi: “Wewe ni usalama wangu”,

25sikupata kufurahia wingi wa utajiri wangu

au kujivunia mapato mengi ya mikono yangu.

26Sikuangalia jua likiangaza

au mwezi ukipita katika uzuri wake

27kusudi niviabudu kwa siri,

na kubusu mikono yangu kwa heshima yake.

28Huo ungekuwa uovu wa kuazibiwa na waamuzi

maana ningekuwa mwongo mbele ya Mungu anayekuwa juu.

29Nimefurahia kuangamia kwa adui yangu,

au kufurahi alipopatwa na hasara?

30Hapana!

Sikuruhusu kinywa changu kusema mabaya juu yake,

kwa kumulaani kusudi akufe.

31Watumishi wangu wote wanasema wazi,

kila mugeni amekaribishwa katika nyumba yangu.

32Musafiri hakulala inje ya nyumba yangu;

nilimufungulia mulango mupita njia.

33Nimeficha makosa yangu kama wengine?

Nimekataa kutambua zambi zangu?

34Sijaogopa kusimama mbele ya kundi la watu

wala kukaa kimya au kujifungia ndani,

kwa kuogopa kutishwa na mazarau yao.

35Heri kungekuwa mutu wa kunisikiliza!

Ninaweza kutia sahihi yangu katika kila neno nililosema.

Mungu Mwenye Uwezo anijibu!

Heri mashitaki waadui zangu wanayonitolea yangeandikwa!

36Ningeyabeba kwa sifa juu ya mabega yangu

na kuyavaa kwenye kichwa kama taji.

37Ningemuhesabilia Mungu kila kitu nilichofanya,

ningemwendea kama mwana wa mufalme.

38Kama nimeiba shamba ninalolima

na kusababisha mifereji yake iomboleze,

39kwa kufaidika na mazao yake bila kulipa

na kusababisha kifo cha wenyeji,

40basi miiba iote mule pahali pa ngano,

na magugu pahali pa shayiri.

Mwisho wa masemi ya Yobu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help