Isaya 55 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mukuje hata kama hamuna feza

1Ee ninyi wote wenye kiu mukuje kwenye maji!

Mukuje, wote hata musiokuwa na feza;

mununue chakula na mupate kula,

mununue divai na maziwa.

Bila feza, bila malipo!

2Mbona munatumia feza zenu

kwa ajili ya kitu kisichokuwa chakula?

Kwa nini kutoa jasho lenu kwa kitu kisichoshibisha?

Munisikilize mimi kwa uangalifu,

nanyi mutakula vinavyokuwa vitamu,

na kufurahia vinavyokuwa bora.

3Mutege sikio, enyi watu wangu, mukuje kwangu;

munisikilize, kusudi mupate kuishi.

Nami nitafanya nanyi agano la milele;

nitawatendea mema niliyomwahidi Daudi.

4Mimi nilimufanya kuwa mukubwa na mutawala wa mataifa

kusudi yeye anishuhudie kwa watu wa mataifa.

5Sasa utayaita mataifa usiyoyajua,

watu wa mataifa yasiyokutambua watakuja mbio kwenu,

kwa sababu yangu mimi Yawe, Mungu wako;

kwa sababu yangu mimi Mutakatifu wa Israeli

niliyekufanya wewe upate utukufu.

6Mumutafute Yawe wakati angali anaweza kupatikana,

mumwombe musaada wakati angali karibu.

7Waovu waache njia zao mbaya,

watu wabaya waachane na mawazo yao mabaya;

wamurudilie Yawe apate kuwahurumia,

wamwendee Mungu wetu maana atawasamehe.

8Maana mawazo yangu si kama mawazo yenu,

wala njia zangu si kama njia zenu.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

9Kama vile mbingu zinavyokuwa mbali na dunia,

ndivyo njia zangu zinavyokuwa mbali na zenu,

na mawazo yangu mbali na mawazo yenu.

10Kama vile mvua na teluji inavyoshuka toka mbinguni,

wala hairudi kule lakini inalowanisha udongo,

kuuzalisha na kuchipukiza mimea,

na kumupatia mupandaji mbegu na kuwapa watu chakula,

11ni vilevile na neno langu mimi:

halitanirudilia bila mafanikio,

lakini litatimiza mapenzi yangu,

litafikia shabaha nililoliwekea.

12Mutatoka Babeli kwa furaha;

mutaongozwa muende kwa amani.

Milima na vilima mbele yenu vitapiga kelele na kuimba,

na miti yote katika mashamba itawapigia mikono.

13Pahali pa miiba kutaota miti ya shindano,

na pahali pa michongoma kutaota misunobari.

Hilo litakuwa jambo litakalowakumbusha watu

juu ya mambo niliyotenda mimi Yawe,

kitambulisho cha milele ambacho hakitafutwa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help