Nehemia 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kujitenga na watu wengine

1Katika siku ile ya sherehe, kitabu cha Musa kikasomwa na ikajulikana kwamba Waamoni na Wamoabu hawaruhusiwi kuingia katika mukutano wa watu wa Mungu. Ang. Kumb 23.3-5

2Kwa sababu watu wa Israeli, walipokuwa wanasafiri toka Misri, wao hawakuwapa chakula wala maji ya kunywa, pahali pake wakamulipa Balamu kwa kuwalaani watu wa Israeli, lakini Mungu wetu akageuza laana yao kuwa baraka. Ang. Hes 22.1-6

3Watu wa Israeli waliposikia Sheria hiyo wakawatenga watu wa mataifa mengine.

Nehemia anafanya mapinduzi

4Mbele ya siku ya sherehe, kuhani Eliasibu aliyekuwa amechaguliwa kwa kulinda vyumba vya nyumba ya Mungu wetu, na mwenye ushirika mwema na Tobia,

5alimuruhusu Tobia kutumia chumba kikubwa ambamo pale mbele walikuwa wakiweka sadaka za unga, ubani, vyombo, zaka za unga, divai, mafuta; vitu hivyo vyote Waisraeli walivyoagizwa kutoa kwa Walawi, waimbaji, walinzi wa milango, na matoleo kwa makuhani.

6Wakati mambo haya yalipokuwa yanatendeka mimi sikukuwa Yerusalema; maana katika mwaka wa makumi tatu na mbili wa utawala wa mufalme Artasasta wa Babeli, nilikuwa nimeomba ruhusa; nami nikaenda kwake.

7Niliporudi Yerusalema ndipo nikagundua uovu wa Eliasibu wa kumutayarishia Tobia chumba katika kiwanja cha nyumba ya Mungu.

8Nikakasirika sana na nikavitupilia inje vyombo vyote vya Tobia.

9Nikaamuru watu, nao wakatakasa vyombo hivyo halafu nikarudisha mule vifaa vya nyumba ya Mungu, pamoja na sadaka ya unga na ubani.

10Tena nikagundua kwamba Walawi hawakupewa haki zao; na matokeo yake ni kwamba Walawi na waimbaji waliokuwa wakifanya kazi pale mbele, sasa walikwisha kurudilia mashamba yao. Ang. Kumb 12.19

11Nikawakaripia viongozi, nikisema: “Kwa nini nyumba ya Mungu imeachwa?” Nikawakusanya pamoja na kuwarudisha katika kazi.

12Kisha, watu wote wa Israeli, wakaanza tena kuleta zaka zao za unga, divai na mafuta kwenye gala. Ang. Mal 3.10

13Nikachagua watu hawa kuwa walinzi wa gala: kuhani Selemia, Zadoki mwandishi na Pedaya, Mulawi. Hanani mwana wa Zakuri mujukuu wa Matania akakuwa musaidizi wao. Walikuwa waaminifu na kazi yao ilikuwa kuwagawanyia wandugu zao mahitaji yao.

14Ee Mungu wangu, unikumbuke kwa ajili ya haya yote na usiyasahau matendo yangu mema niliyofanya kwa ajili ya nyumba yako na kwa ajili ya kazi yako.

15Wakati uleule, nikawaona watu wa Yuda wakikamua zabibu katika vikamulio siku za Sabato. Tena wengine walikuwa wakiwabebesha punda wao ngano, divai, zabibu, tini na vitu vingine wakivipeleka Yerusalema. Nikawaonya kwamba hawana ruhusa ya kuuzisha katika siku hiyo. Ang. Kut 20.8-10; Kumb 5.12-14; Yer 17.21-23

16Watu wengine toka muji wa Tiro walileta samaki na biashara nyingine Yerusalema na kuwauzishia watu wetu siku ya Sabato.

17Nikawakaripia viongozi wa watu wa Yuda, nikisema: “Uovu gani huu munaofanya, kuichafua siku ya Sabato?

18Babu zetu hawakufanya uovu wa namna hiihii na kumusukuma Mungu wetu kutuletea hasara pamoja na muji huu? Na munazidi kuamusha kasirani yake juu ya watu wa Israeli kwa kuchafua siku ya Sabato.”

19Halafu, nikaamuru kwamba milango ya Yerusalema ifungwe wakati siku ya Sabato inapoanza magaribi, wakati giza linapoanza kuingia, na isifunguliwe mpaka Sabato imekwisha. Nikaweka watumishi wangu wamoja kwenye milango na kuwaagiza kwamba kitu chochote kisiletwe katika muji siku ya Sabato.

20Mara mbili au tatu hivi wachuuzi waliokuwa wakiuzisha biashara ya aina mbalimbali walipaswa kulala inje ya muji.

21Nikawaonya na kuwaambia: “Hakuna maana kulala inje ya muji. Mukijaribu tena nitatumia nguvu.” Hivyo tangu wakati ule hawakurudi tena siku ya Sabato.

22Nikaagiza Walawi kujitakasa na kwenda kulinda milango kwa kutakasa siku ya Sabato.

Ee, Mungu wangu, unikumbuke hata na kwa hili vilevile unihurumie kutokana na rehema zako kubwa.

23Tena wakati ule nikaona Wayuda waliooa wanawake toka Asidodi, Amoni na Moabu; Ang. Kut 34.11-16; Kumb 7.1-5

24na nusu ya watoto wao waliosema luga ya Kiasidodi au luga nyingine na hawakuweza kusema luga ya inchi ya Yuda.

25Nikawakaripia na kuwalaani, hata nikawapiga wamoja kati yao na kuwaongoa nywele zao. Nikawalazimisha kuapa kwa jina la Mungu, nikisema: “Wabinti zenu musiwaoeshe kwa vijana wao, wala wabinti zao wasiolewe na vijana wenu au na ninyi wenyewe.

26Si Solomono alitenda zambi kwa sababu ya wanawake wa namna hiyo? Yeye alikuwa mufalme mukubwa kuliko wafalme wa mataifa mengine. Mungu akamupenda na akamufanya kuwa mufalme juu ya watu wote wa Israeli, hata hivyo wanawake wa mataifa mengine, wakamusukuma kutenda zambi. Ang. 2 Sam 12.24-25; 1 Fal 11.1-8

27Basi, sasa tufuate mufano wenu na tutende zambi hii kubwa ya kutomutii Mungu wetu kwa kuoa wanawake wa kigeni?”

28Mumoja kati ya wana wa Yoyada mwana wa Kuhani Mukubwa Eliasibu, alioa binti wa Sanibalati kutoka muji wa Beti-Horoni, kwa sababu hiyo nikamufukuza kutoka mbele yangu. Ang. Neh 4.1

29Ee Mungu, kumbuka jinsi watu walivyochafua ukuhani na agano la kikuhani na la Walawi.

30Nikawatakasa watu kutokana na chochote kilichokuwa cha kigeni. Nikatayarisha utaratibu kwa ajili ya makuhani na Walawi juu ya kazi ya kila mumoja wao.

31Nikaagiza matoleo ya kuni kufanyika katika wakati unaopaswa na malimbuko wakati wake. Ee Mungu wangu, unikumbuke kwa ajili ya haya yote na unijalie mema.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help