1Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi.
2Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu;
anga linaeleza kazi ya mikono yake.
3Muchana unaupasha habari muchana unaofuata,
usiku unaufahamisha usiku unaofuata.
4Si kwa musemo au kwa maneno;
wala hakuna sauti inayosikilika;
5hata hivyo, ujumbe wao unaenea katika dunia yote,
na habari zao zinafika miisho ya ulimwengu.
Mungu amewekea jua makao yake katika anga;
6nalo linatoka kama vile bwana-arusi kutoka chumba chake,
linakimbia kwa furaha katika njia yake kama shujaa.
7Linatokea kwa upande mumoja,
na kuzunguka mpaka upande mwingine;
hakuna kinachoweza kuepuka joto lake.
Sheria ya Mungu8Sheria ya Yawe ni kamilifu;
inamupa mutu uzima mupya.
Maagizo ya Yawe ni ya kuaminiwa;
yanawapa wajinga hekima.
9Kanuni za Yawe ni sawa;
zinafurahisha moyo.
Amri za Yawe ni safi;
zinamufungua mutu macho.
10Kumutii Yawe ni jambo jema;
kunadumu milele.
Maagizo ya Yawe ni sawa,
yote ni ya haki kabisa.
11Yanatamanika kuliko zahabu,
kuliko zahabu safi kabisa.
Ni matamu kuliko asali,
kuliko asali safi kabisa.
12Yananifundisha mimi mutumishi wako;
kuyafuata kunaniletea zawadi kubwa.
13Lakini nani anayeona makosa yake mwenyewe?
Ee Mungu, unisamehe makosa nisiyoyajua.
14Unikinge mimi mutumishi wako na makosa ya makusudi,
usikubali hayo yanitawale.
Hapo nitakuwa mukamilifu,
wala sitakuwa na kosa kubwa.
15Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu,
yakubalike mbele yako, ee Yawe,
kikingio changu na mwokozi wangu!
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.