1Nyuma ya mambo hayo, Yosefu akapewa habari kwamba baba yake ni mugonjwa. Hivyo, akatwaa wana wake wawili, Manase na Efuraimu, akakwenda nao kwa baba yake.
2Yakobo alipofahamishwa kwamba mwana wake Yosefu amefika kumwona, akajikaza kuamuka, akaikaa juu ya kitanda.
3Yakobo akamwambia Yosefu: “Mungu Mwenye Nguvu alinitokea nilipokuwa kule Luzu katika inchi ya Kanana, akanibariki.
4Akaniambia: ‘Nitakufanya ukuwe na wazao na uongezeke. Nitakufanya ukuwe babu ya jamii kubwa za watu. Inchi hii nitawapa wazao wako, wairizi milele.’ ”
5Yakobo akaendelea kusema: “Wana wako wawili uliowapata hapa Misri mbele sijafika, ni wana wangu. Efuraimu na Manase watakuwa wangu kama vile Rubeni na Simeoni wanavyokuwa.
6Lakini, watoto utakaopata nyuma watakuwa wako, kwa jina la wandugu zao wataitwa katika urizi wao.
7Ninaamua hivyo kwa sababu ya mama yako, Rakeli. Nilipokuwa ninarudi kutoka Padani yeye alikufa katika inchi ya Kanana, tukiwa karibu kufika Efurata, akaniachia huzuni. Basi, nikamuzika palepale, kando ya njia inayokwenda Efurata, maana yake Betelehemu.”
8Israeli alipowaona wana wa Yosefu, akamwuliza: “Ni wa nani hawa?”
9Yosefu akamujibu baba yake: “Hawa ni wana wangu Mungu alionijalia nikiwa huku.”
Israeli akasema: “Tafazali, uwalete karibu nipate kuwabariki.”
10Macho ya Israeli yalikuwa hayaoni vizuri kwa sababu ya uzee. Basi, Yosefu akasogeza wana wake karibu na baba yake, naye akawabusu na kuwakumbatia.
11Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Sikutazamia kuuona uso wako tena, lakini, kumbe, Mungu amenijalia hata kuwaona watoto wako!”
12Hapo Yosefu akawaondoa wana wake kwenye magoti ya baba yake, kisha akainama kwa heshima.
13Yosefu akawainua wana wake wawili, Efuraimu katika mukono wake wa kuume, akimwelekeza kwenye mukono wa kushoto wa baba yake, na Manase katika mukono wake wa kushoto, akimwelekeza kwenye mukono wa kuume wa baba yake, akawasogeza kwa babu yao.
14Lakini Israeli akaipishanisha mikono yake: mukono wake wa kuume akauweka juu ya kichwa cha Efuraimu, ingawa alikuwa mudogo na mukono wake wa kushoto akauweka juu ya kichwa cha Manase, aliyekuwa muzaliwa wa kwanza.
15Kisha Israeli akamubariki Yosefu, akisema:
“Mungu ambaye babu zangu
Abrahamu na Isaka walimutii katika maisha yao,
Mungu ambaye ameniongoza katika maisha yangu mpaka leo,
16na malaika ambaye aliniokoa katika mabaya yote,
awabariki vijana hawa!
Jina langu na majina ya babu zangu, Abrahamu na Isaka,
yadumishwe katika vijana hawa;
nao waongezeke kwa wingi katika dunia.”
17Yosefu alipoona kwamba baba yake ameuweka mukono wake wa kuume juu ya kichwa cha Efuraimu hakupendezwa. Basi, akaushika mukono wa baba yake, akitaka kuuondoa juu ya kichwa cha Efuraimu auweke juu ya kichwa cha Manase.
18Akamwambia baba yake: “Sivyo, baba! Huyu hapa ndiye muzaliwa wa kwanza. Tafazali, uweke mukono wako wa kuume juu ya kichwa chake.”
19Lakini baba yake akakataa, akisema: “Ninajua, mwana wangu, ninajua. Wana wa Manase vilevile watakuwa taifa na wakubwa. Hata hivyo, ndugu yake mudogo atakuwa mukubwa kuliko yeye na wazao wake watakuwa mataifa mengi.”
20Basi, Israeli akawabariki siku hiyo, akisema:
“Waisraeli watatumia majina yenu kwa kubariki,
watasema: ‘Mungu akutendee mema kama Efuraimu na Manase!’ ”
Ndivyo Israeli alivyomuweka Efuraimu mbele ya Manase.
21Kisha Israeli akamwambia Yosefu: “Kama vile unavyoona, mimi niko karibu kufa. Hata hivyo, Mungu atakuwa pamoja nanyi, na kuwarudisha katika inchi ya babu zenu.
22Zaidi ya hayo, nimekupa wewe, wala si wandugu zako, eneo moja kwenye milima, nililowanyanganya Waamori kwa upanga na upinde wangu.”
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.