1Hili ni neno la Yawe lililomufikia Zefania mwana wa Kusi, mujukuu wa Gedalia mwana wa Amaria, wa uzao wa mufalme Hezekia, wakati wa utawala wa mufalme Yosia mwana wa Amoni, mufalme wa Yuda:
2Nitateketeza kabisa viumbe vyote katika dunia:
3wanadamu, nyama, ndege
na samaki. Vyote nitaviangamiza.
Waovu nitawaangamiza kabisa;
wanadamu nitawateketeza kabisa katika dunia.
4Nitaunyoosha mukono wangu kwa kuazibu inchi ya Yuda,
pamoja na wakaaji wote wa Yerusalema.
Nitaangamiza mabaki yote ya mungu Bali kutoka inchi hii,
na hakuna atakayetambua jina lao.
5Nitawaangamiza wote wanaoinama juu ya dari,
wakiabudu jeshi la mbinguni.
Nitawaangamiza wale wanaoniabudu
na kuapa kwa jina langu,
tena wanaapa vilevile kwa jina la mungu Milkomu.
6Nitawaangamiza wote walioniacha mimi Yawe,
wote walioacha kunitafuta na kuniuliza shauri.
7Munyamaze mbele ya Bwana wenu Yawe,
maana siku ya Yawe iko karibu.
Yawe ametayarisha sadaka,
naye amekwisha kutakasa waalikwa wake.
8Yawe anasema hivi:
Katika siku ile ya karamu yangu,
nitawaazibu wakubwa wa watu hao,
vilevile na wana wa mufalme
pamoja na wote wanaoiga desturi za kigeni.
9Siku hiyo nitawaazibu wote
wanaoruka kizingiti cha nyumba kama wapagani,
wanaojaza nyumba ya bwana wao vitu vya mateso na udanganyifu.
10Siku hiyo,
kutasikilika kilio kutoka Mulango wa Samaki,
maombolezo kutoka Mutaa wa Pili,
na mulio mukubwa kutoka katika milima.
–Ni ujumbe wa Yawe.–
11Mulie, enyi wakaaji wa Makitesi!
Wachuuzi wote wameangamia,
wote wanaopima feza wameteketezwa.
12Wakati huo nitauchunguza Yerusalema kwa taa,
nitawaazibu wanaoishi wakitulia kama machicha ya divai,
wote ambao wanasema kati yao:
Yawe hatafanya kitu: chema au kibaya.
13Utajiri wao utanyanganywa,
na nyumba zao zitaachwa tupu!
Watajijengea nyumba, lakini hawataishi humo.
Watapanda mizabibu, lakini hawatakunywa divai yake.
14Ile siku kubwa ya Yawe imekaribia,
iko karibu na inakuja mbio.
Mulio wa siku ya Yawe ni wa uchungu;
hapo, hata shujaa atalia kwa sauti.
15Siku hiyo itakuwa siku ya kasirani,
ni siku ya taabu na uchungu,
siku ya giza na huzuni;
siku ya uharibifu na maangamizi,
siku ya mawingu na giza kubwa.
16Siku hiyo ni ya mulio wa baragumu ya vita,
juu ya miji yenye vikingio na kuta ndefu.
17Kwa maana watu wamemukosea Yawe,
yeye atawaletea taabu kubwa,
wao watatembea kama vipofu.
Damu yao itamwangwa kama mavumbi,
na miili yao kama mavi.
18Feza yao wala zahabu yao havitaweza kuwaokoa
katika siku hiyo ya kasirani ya Yawe.
Kwa moto wa wivu wake
dunia yote itateketezwa.
Kwa ukamilifu na kwa namna ya kuogopesha
atawafanya wakaaji wote katika dunia watoweke.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.