1Ujumbe wa Mungu juu ya inchi ya Misri.
Yawe amepanda juu ya wingu linaloenda mbio
na kuja mpaka katika inchi ya Misri.
Sanamu za miungu ya Wamisri zitatetemeka mbele yake,
mioyo ya Wamisri itayeyuka kwa woga.
2Mimi nitawachonganisha Wamisri wao kwa wao.
Ndugu atapigana na ndugu yake,
jirani atapigana na jirani yake,
muji mumoja na muji mwingine,
mufalme mumoja na mufalme mwingine.
3Nitawaondolea Wamisri uhodari wao.
Nitaivuruga mipango yao.
Watatafuta shauri kwa sanamu na mizimu,
wachawi, mizuka na pepo.
4Nitawatia Wamisri katika mikono ya bwana mukali,
mufalme mukali ambaye atawatawala.
–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi.
5Maji ya muto Nili yatakaushwa,
nao utakauka kabisa.
6Mifereji yake itatoa harufu mbaya,
vijito vyake vitapunguka na kukauka.
Nyasi na matete yake yataoza.
7Sehemu za kandokando ya Nili zitakuwa tupu.
Mimea yote iliyopandwa humo itakauka
na kupeperushiwa mbali na kutoweka.
8Wavuvi wataomboleza,
wote wanaotumia ndoana watalalamika,
wote wanaotega nyavu humo watavunjika moyo.
9Wafuma nguo za kitani watafazaika,
wote kwa pamoja watavunjika moyo.
10Wafuma nguo watafezeheshwa,
na wafanya kazi watahuzunika.
11Wakubwa wa muji wa Soani ni wapumbafu kabisa,
washauri wa Mufalme wa Misri wanatoa shauri la kijinga!
Kila mumoja anaweza namna gani kumwambia Mufalme wa Misri:
Mimi ni wa uzao wa wenye hekima,
wa uzao wa wafalme wa zamani!
12Wako wapi, ewe Mufalme wa Misri, wenye hekima wako?
Uwaache basi wakwambie na kukujulisha mambo
Yawe wa majeshi aliyopanga juu ya Misri!
13Lakini wakubwa wa Soani ni wapumbafu,
wakubwa wa Nofi wamedanganyika.
Hao wanaokuwa musingi wa makabila yao
wamelipotosha taifa la Misri.
14Yawe amewamwangia roho ya fujo,
wakawapotosha Wamisri katika mipango yao yote,
nao wakakuwa kama mulevi anayeyumbayumba akitapika.
15Hakuna mutu yeyote katika inchi ya Misri,
mutawala au wanainchi, wakubwa au watu wadogo,
anayeweza kufanya jambo lolote la maana.
Wamisri watamwabudu Yawe16Siku ile watu wa Misri wataogopa kama wanawake. Watatetemeka kwa hofu watakapomwona Yawe wa majeshi ameunyoosha mukono wake juu yao.
17Yuda atakuwa kitisho kikubwa kwa Wamisri. Wote watakaoambiwa habari za Yuda wataingiwa na woga kwa sababu ya jambo Yawe wa majeshi aliloamua kuwatendea.
18Siku hiyo luga ya Kiebrania itatumika katika miji mitano ya Misri, na watu wa miji hiyo wataapa kuwa waaminifu kwa Yawe wa majeshi. Muji mumoja kati ya miji hiyo utaitwa “Muji wa Jua”.
19Siku hiyo, kutakuwa mazabahu kwa ajili ya Yawe katikati ya inchi ya Misri, na nguzo iliyotakaswa kwa ajili ya Mungu kwenye mpaka wa Misri.
20Mazabahu hayo yatakuwa kitambulisho na ushuhuda kwa Yawe wa majeshi katika inchi ya Misri. Watu wakimulilia Yawe humo kwa sababu ya kugandamizwa, yeye atawapelekea mukombozi atakayewatetea na kuwakomboa.
21Yawe atajijulisha kwa Wamisri na hapo ndipo Wamisri watakapomwitikia na kumwabudu kwa kumutolea matoleo na sadaka za kuteketezwa. Vilevile watafanyia Yawe viapo ambavyo watavitimiza.
22Yawe atawaazibu Wamisri na kuwaponya. Nao watamurudilia, naye atayasikiliza maombi yao na kuwaponya.
23Wakati huo, kutakuwa barabara kubwa kutoka inchi ya Misri mpaka katika inchi ya Asuria. Waasuria watawatembelea Wamisri, na Wamisri watawatembelea Waasuria; nao wote watamwabudu Mungu pamoja.
24Wakati huo, Israeli itahesabiwa pamoja na Misri na Asuria; mataifa haya matatu yatakuwa baraka kwa dunia yote.
25Yawe wa majeshi atawabariki na kusema: Wabarikiwe Wamisri watu wangu, vilevile na Waasuria ambao ni kitambulisho cha kazi yangu na Waisraeli wanaokuwa urizi wangu.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.