2 Samweli 13 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Amunoni na Tamari

1Abusaloma mwana wa Daudi, alikuwa na dada yake muzuri sana aliyeitwa Tamari. Naye Amunoni, mwana mwingine wa Daudi, akamupenda sana Tamari.

2Amunoni aliteseka sana hata akajifanya mugonjwa kwa sababu ya dada yake Tamari kufuatana na vile Tamari alikuwa angali bikira, na ilionekana jambo lisilowezekana kwa Amunoni kufanya kitu chochote naye.

3Lakini Amunoni alikuwa na rafiki aliyeitwa Yonadabu, mwana wa Shama, ndugu ya Daudi. Yonadabu alikuwa mutu mwerevu sana.

4Yonadabu akamwambia Amunoni: “Wewe ni mutoto wa mufalme, kwa nini unakonda na unaonekana hauna furaha kila siku? Mbona hautaki kuniambia?”

Amunoni akamwambia: “Ninamupenda Tamari, dada ya ndugu yangu Abusaloma.”

5Yonadabu akamwambia: “Wewe ujilalishe katika kitanda na ujifanye kuwa mugonjwa. Baba yako atakapokuja kukuona, wewe umusihi ukisema: ‘Umuruhusu dada yangu, Tamari, akuje aniletee mukate nipate kula na anitayarishie chakula mbele yangu kusudi nikione naye mwenyewe anikulishe.’ ”

6Kwa hiyo, Amunoni akaendelea kulala katika kitanda, akijifanya kuwa mugonjwa. Mufalme alipokwenda kumwona, Amunoni alimwambia: “Ninakuomba, Tamari akuje hapa anitengenezee mikate michache mbele yangu. Halafu yeye mwenyewe anikulishe.”

7Halafu, Daudi alipeleka ujumbe kwa Tamari kwamba aende kwa kaka yake Amunoni, amutengenezee chakula.

8Tamari alikwenda kule, akamukuta amelala. Akatwaa unga, akauponda, na kutengeneza mikate mbele ya Amunoni.

9Mikate hiyo ilipokuwa tayari, Tamari akaiopoa kutoka kikaango. Akamupelekea Amunoni, lakini Amunoni alikataa kula, akaamuru kwamba watu wote watoke inje, na wote wakaondoka.

10Kisha, Amunoni akamwambia Tamari: “Sasa uniletee mikate ile ndani ya chumba changu, halafu unikulishe.”

Tamari alitwaa mikate aliyoitayarisha na kuipeleka ndani ya chumba cha kaka yake Amunoni.

11Hapo, alipokuwa anamupatia mikate ile, Amunoni alimukamata na kumwambia: “Kuja ulale nami.”

12Tamari akamwambia: “Sivyo, kaka yangu, usinilazimishe. Kitendo hiki hakifanyiki katika Israeli. Usifanye kitendo hiki cha kipumbafu.

13Kwa upande wangu, siwezi kuvumilia haya hiyo. Na kwa upande wako, utakuwa mumoja wa wapumbafu wa Israeli. Basi, mimi ninakusihi uzungumuze na mufalme maana hatakukataza kunioa.”

14Lakini Amunoni hakutaka kumusikiliza na kwa sababu alimushinda nguvu, akamukamata, akalala naye.

15Kisha, Amunoni akamuchukia Tamari kupita kipimo. Akamuchukia Tamari kuliko alivyomupenda zamani. Akamwambia Tamari: “Simama ondoka mara moja.”

16Tamari akamujibu: “Sivyo kaka yangu. Ukinifukuza utafanya ubaya mukubwa zaidi kuliko ule ulionitendea.”

Lakini Amunoni hakutaka kumusikiliza.

17Akamwita kijana wake aliyemutumikia, akamwambia: “Umutoshe mwanamuke huyu mbele yangu. Na ufunge mulango kwa kifungio.”

18Amunoni na yule kijana wakamutosha inje na kufunga mulango kwa kifungio. Tamari alikuwa amevaa kanzu ndefu yenye mikono mirefu maana hivi ndivyo mabikira wa mufalme walivyovaa zamani.

19Basi, Tamari alijipakaa majivu kwenye kichwa, akapasua kanzu yake, akaweka mikono yake juu ya kichwa, halafu akaondoka akiwa analia kwa sauti.

20Kaka yake, Abusaloma, alipomwona, alimwuliza: “Kaka yako Amunoni amelala nawe? Tulia dada yangu. Yeye ni kaka yako. Usichunge jambo hilo ndani ya moyo wako.” Halafu, Tamari aliishi katika nyumba ya Abusaloma akiwa na huzuni na mwenye kutupiliwa.

21Mufalme Daudi aliposikia jambo hilo alikasirika sana.

22Abusaloma alimuchukia Amunoni sana hata hakusema naye, kwa sababu alimukamata dada yake Tamari kwa kinguvu, akalala naye.

Abusaloma anajilipiza kisasi

23Nyuma ya miaka miwili mizima, Abusaloma alikuwa na shuguli ya kuwakata kondoo wake manyoya katika muji wa Bali-Hazori, karibu na Efuraimu. Akawaalika wana wote wa mufalme.

24Abusaloma alimwendea mufalme Daudi, akamwambia: “Angalia, mimi mutumishi wako ninawakata kondoo manyoya. Ninakuomba wewe mufalme pamoja na watumishi wako, muende pamoja nami, mutumishi wako.”

25Mufalme akamujibu: “Sivyo, mwana wangu, tusiende wote, kusudi tusikuwe muzigo kwako.”

Ingawa Abusaloma alizidi kumusihi baba yake aende, lakini mufalme alikataa, lakini alimupa baraka zake.

26Halafu, Abusaloma akamwambia: “Kama hauendi, basi, umuruhusu ndugu yangu Amunoni tuende naye.”

Mufalme akamujibu: “Lakini kwa nini aende pamoja nanyi?”

27Lakini Abusaloma alizidi kumusihi, na kwa mwisho mufalme akamuruhusu Amunoni na wana wake wengine waende kwenye karamu hiyo.

28Abusaloma akawaambia watumishi wake: “Mumwangalie Amunoni atakapokuwa amekunywa divai na kufurahi. Nitakapowaambia: ‘Mumupige Amunoni’, mumwue. Hiyo ni amri yangu kwenu. Mujipe moyo na mukuwe hodari.”

29Halafu, watumishi wa Abusaloma walimutendea Amunoni kama vile walivyoamriwa na Abusaloma, kisha wana wengine wa mufalme wakaondoka, kila mumoja akapanda juu ya nyumbu wake na kukimbia.

30Walipokuwa wangali katika njia, Daudi alipata habari kwamba Abusaloma amewaua watoto wake wote hakuna hata mumoja aliyebakia.

31Mufalme Daudi alisimama, akapasua nguo yake kwa huzuni akalala chini. Hata na watumishi wake wote waliokuwa wakisimama karibu naye walipasua nguo zao.

32Lakini Yonadabu mwana wa Simea, ndugu ya Daudi akamwambia: “Bwana wangu, usifikiri kwamba wana wako wote wameuawa. Amunoni pekee ndiye aliyeuawa. Abusaloma alikusudia kuyafanya mambo haya tangu wakati ule Amunoni alipomukamata dada yake Tamari kwa kinguvu na kulala naye.

33Kwa hiyo, bwana wangu, usifikiri ndani ya moyo wako kwamba watoto wako wote wamekufa. Ni Amunoni pekee ndiye aliyeuawa.”

34Lakini Abusaloma alikuwa amekwisha kukimbia. Naye kijana aliyekuwa na zamu ya ulinzi, akaona kundi kubwa la watu wanakuja kutokea kwenye mulima katika barabara ya kutoka Horonaimu.

35Yonadabu akamwambia Daudi: “Angalia mufalme, wana wako wanakuja kama nilivyokuambia mimi mutumishi wako.”

36Mara moja yule mutumishi alipomaliza kusema, wana wa mufalme wakaingia, wakaanza kulia kwa sauti. Mufalme na watumishi wake wote, wakalia kwa uchungu.

37Lakini Abusaloma alikimbilia kwa Talmayi mwana wa Amihudi, mufalme wa muji wa Gesuri. Mufalme Daudi akamufanyia mwana wake Amunoni kilio kwa siku nyingi.

38Abusaloma alikimbilia Gesuri, akakaa kule kwa muda wa miaka mitatu.

39Nyuma ya mufalme Daudi kutulia kutokana na kifo cha Amunoni, alianza kutamani kumwona mwana wake Abusaloma.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help