Waroma 2 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Hukumu ya Mungu

1Wewe unayemuhukumu mwingine hauna namna yoyote ya kujitetea, haizuru wewe ni nani. Kwa maana wakati unapohukumu mwingine, unajikatia hukumu wewe mwenyewe, kwa sababu wewe unayehukumu unatenda mambo yale yale.

2Tunajua kwamba Mungu anahukumu kwa haki watu wanaofanya mambo ya namna hiyo.

3Basi wewe unawahukumu wale wanaofanya mambo yale, lakini wewe mwenyewe unayafanya! Unafikiri kwamba utaponyoka hukumu ya Mungu?

4Au haujali na uwingi wa wema, utulivu na uvumilivu wa Mungu? Haujui kwamba wema wake ungeweza kukuongoza hata upate kugeuka toka zambi?

5Lakini wewe ni mugumu na mwenye moyo usiotaka kugeuka. Kwa hiyo unajiwekea azabu kubwa siku Mungu atakapoonyesha kasirani yake na hukumu yake ya haki.

6Kwa maana Mungu atamulipa kila mutu kwa kadiri ya matendo yake.

7Wale wanaofanya matendo mema bila kuchoka na kutafuta toka kwa Mungu utukufu, heshima na uzima usiokuwa na mwisho, Mungu atawapa uzima wa milele.

8Lakini wapingaji na wale wanaokataa kufuata ukweli, wakifuata uovu, wataangukiwa na kasirani na hasira ya Mungu.

9Mateso na taabu zitamupata kila mutu anayefanya mabaya: kwanza Wayuda, kisha watu wa mataifa mengine vilevile.

10Lakini kila mutu anayefanya mema atapata utukufu, heshima na amani; kwanza Wayuda, kisha watu wa mataifa mengine vilevile.

11Kwa maana Mungu hana upendeleo.

12Wote wanaofanya zambi pasipo kujua Sheria ya Musa watapotea pasipo kuhukumiwa na Sheria ile. Lakini wote wanaofanya zambi wakijua Sheria watahukumiwa kufuatana na Sheria.

13Ni vile kwa sababu si wale wanaosikia Sheria ndio wanaohesabiwa haki mbele ya Mungu, lakini ni wale wanaotii Sheria.

14Watu wa mataifa hawana Sheria ya Musa. Lakini wanapofanya sawa inavyoamuriwa na Sheria ile kutokana na zamiri yao, wao ni Sheria kwa ajili yao wenyewe, ijapokuwa hawana Sheria ile.

15Kwa maana wanaonyesha kwamba maagizo ya Sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao. Zamiri yao vilevile inawahukumu, na mawazo yao yenyewe yanawashitaki au yanawatetea.

16Hiyo ndiyo itakayotokea siku ile Mungu atakapohukumu mambo ya siri ya watu kwa njia ya Yesu Kristo, kama vile Habari Njema yangu inavyosema.

Wayuda walivunja Sheria

17Sasa wewe unaitwa Muyuda, unategemea Sheria na kujivunia Mungu.

18Unajidai kwamba unajua mapenzi yake na kutambua mambo yanayofaa zaidi kwa sababu umefundishwa na Sheria.

19Unajiaminia kwamba wewe ni mwongozi wa vipofu na mwangaza kwa wale wanaokuwa katika giza,

20mufundisha wajinga na mwalimu wa watoto, kwa sababu kutokana na Sheria unajua uhakika juu ya mambo ya elimu na ya kweli.

21Basi wewe unayewafundisha watu wengine, kwa sababu gani haujifundishi wewe mwenyewe? Wewe unayehubiri kwamba haifai kuiba, kwa nini unaiba?

22Wewe unayesema kwamba haifai kuzini, kwa nini unazini? Wewe unayechukia sanamu za miungu, kwa nini unaiba vitu ndani ya hekalu zao?

23Unajisifu kwamba unajua Sheria, lakini unamuzarau Mungu kwa kuvunja Sheria!

24Kwa maana kama ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Kwa sababu yenu, jina la Mungu linatukaniwa katikati ya watu wa mataifa mengine.”

25Kutahiriwa kuna mafaa kama ukitii Sheria. Lakini usipotii Sheria, wewe unahesabiwa kama mutu asiyetahiriwa.

26Na kama mutu asiyetahiriwa akitii maagizo ya Sheria, Mungu hatamuhesabu kuwa ametahiriwa?

27Mutu asiyetahiriwa kimwili, lakini anatii Sheria, atakuhukumu wewe unayevunja Sheria ijapokuwa unajua maandiko ya Sheria na umetahiriwa.

28Kwa maana kuonekana kwa inje kwa Muyuda si kuwa Muyuda wa kweli, wala kutahiriwa kimwili tu si kutahiriwa kwa kweli.

29Lakini Muyuda wa kweli ni yule anayekuwa Muyuda kwa ndani, nako kutahiriwa kwa kweli ni kule Roho Mutakatifu anakofanya ndani ya moyo wa mutu, wala si kule kunakofanyika kwa njia ya maandiko ya Sheria. Mutu wa namna hii hapati sifa kutoka kwa watu lakini kutoka kwa Mungu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help