Ezekieli 36 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Mungu atabariki tena Waisraeli

1Yawe aliniambia hivi: Wewe mwanadamu! Toa unabii juu ya milima ya Israeli. Uiambie isikilize maneno yangu.

2Bwana wetu Yawe anasema hivi: Waadui zenu wamewazomea na kusema kwamba ninyi mumekuwa mali yao!

3Kwa hiyo, wewe Ezekieli, toa unabii useme kwamba Bwana wenu Yawe anasema hivi: Watu wamewafanya ninyi milima ya Waisraeli kuwa tupu na kuwashambulia kutoka kila upande hata mumekuwa mali ya mataifa mengine, mukakuwa kitu cha kusimangwa na kuchekelewa kati ya watu!

4Kwa hiyo, enyi milima ya Waisraeli, musikie neno la Bwana wenu Yawe. Anasema juu ya ninyi milima na vilima, mifereji na mabonde, jangwa tupu na miji ya matongo, na miji iliyokamatwa mateka na kuzarauliwa na mataifa yote yanayowazunguka.

5Bwana wenu Yawe anasema hivi: Wivu wangu unawaka sana. Nitayaazibu mataifa mengine na hasa watu wa inchi ya Edomu. Wao kwa furaha ndani ya moyo na mazarau walikamata hiyo inchi inayokuwa yangu ikuwe yao.

6Kwa hiyo, ewe mwanadamu, toa unabii juu ya inchi ya Waisraeli, uiambie milima na vilima, vijito na mabonde kwamba Bwana wao Yawe anasema hivi: Ninasema kutokana na upendo wangu wenye wivu juu ya ninyi, inchi yangu, kwa sababu mumetukanwa na watu wa mataifa.

7Bwana wenu Yawe anasema hivi: Ninaapa hakika kwamba watu wa mataifa yanayokuwa jirani yenu watatukanwa wao wenyewe.

8Lakini juu ya milima ya Waisraeli, miti itatoa matawi na kuzaa matunda kwa ajili ya watu wangu Waisraeli, maana wao wanakaribia kurudi katika inchi yao.

9Mimi niko upande wenu, nitahakikisha kuwa udongo wenu utalimwa na kupandwa mbegu.

10Nitawazidisha sana Waisraeli. Miji itakaliwa, na mabomoko yatajengwa upya.

11Nitawafanya watu na nyama waongezeke na kuwa wengi. Nitawafanya ninyi milima mukaliwe tena kama zamani. Nitawatendea mema mengi kuliko zamani. Nanyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe.

12Nitawafanya watu wangu Waisraeli watembee juu yenu. Nanyi mutakuwa urizi wao, wala hamutawafanya tena wakufiwe na watoto wao.

13Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa vile watu wamesema juu yenu kwamba munakula watu, na mumeliteketezea taifa lenu watoto wake,

14basi, sasa hamutakula tena watu wala kuteketezea taifa lenu watoto wake.

15Sitaruhusu tena mataifa yawatukane, wala kuwazarau tena. Hamutasababisha taifa lenu kukosa.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.

Maisha mapya ya Waisraeli

16Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi:

17Wewe mwanadamu! Waisraeli walipoishi katika inchi yao waliichafua kwa mienendo na matendo yao. Niliyaona matendo yao kuwa sawa na mwanamuke anayekuwa muchafu wakati wa ugonjwa wake wa mwezi.

18Niliwamwangia kasirani yangu kwa sababu ya damu waliyomwanga katika inchi na kwa sababu ya miungu ambayo kwa ajili yao waliichafua inchi.

19Niliwasambaza kati ya mataifa, wakasambazwa katika inchi nyingine. Niliwaazibu kadiri ya tabia yao na matendo yao.

20Hata walipokuwa kati ya mataifa walilikufuru jina langu takatifu, hata watu wakasema hivi juu yao: Hawa ndio wale watu wa Yawe, lakini wamelazimishwa kuondoka katika inchi yake!

21Hiyo ilinifanya kuhangaika juu ya jina langu takatifu ambalo Waisraeli walilikufuru kati ya mataifa walikokwenda.

22Basi, uwaambie Waisraeli kwamba:

Bwana wetu Yawe anasema hivi: Ninachotaka kufanya si kwa faida yenu ninyi watu wa inchi ya Israeli, lakini ni kwa heshima ya jina langu takatifu mulilolikufuru kati ya mataifa mulikokwenda.

23Nitalitakasa jina langu kubwa mulilokufuru kati ya mataifa. Na kwa hiyo mataifa yatatambua kwamba mimi ni Yawe.

–Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.–

Nitawatumia ninyi kuonyesha utakatifu wangu mbele yao.

24Nitawaondoa ninyi katika kila taifa na kuwakusanya kutoka inchi zote za kigeni; nitawarudisha katika inchi yenu wenyewe.

25Nitawanyunyizia maji safi, nanyi mutakuwa safi. Nitawatakasa toka uchafu wenu wote na toka uchafu wa sanamu za miungu yenu yote.

26Nitawapa moyo mupya na kuweka roho mupya ndani yenu. Nitauondoa kwenu moyo mugumu kama jiwe na kuwapa moyo musikilivu. Ang. Eze 11.19-20

27Nitatia roho yangu ndani yenu; nitawafanya mufuate masharti yangu na kushika maagizo yangu.

28Mutakaa katika inchi niliyopatia wazee wenu. Mutakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu.

29Nitawaokoa kutoka uchafu wenu wote. Nitaiamuru ngano iongezeke, wala sitawaletea njaa tena.

30Nitayazidisha matunda ya miti na mazao ya mashamba kusudi musizarauliwe tena kwa ajili ya njaa kati ya mataifa.

31Kisha mutakapokumbuka mienendo yenu miovu na matendo yenu mabaya, mutajichukia wenyewe kwa sababu ya maovu yenu na machukizo muliyofanya.

32Lakini mujue kwamba sitafanya hivyo kwa ajili yenu. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe.– Lakini mupate haya na kufazaika kwa sababu ya matendo yenu, enyi Waisraeli!

33Bwana wetu Yawe anasema hivi: Siku ile nitakapowasafisha ninyi toka maovu yenu yote, nitaifanya miji yenu ikaliwe, nayo mabomoko yajengwe upya.

34Inchi iliyokuwa jangwa italimwa tena, hata atakayepita huko hataiona kuwa jangwa.

35Nao watu watasema: Inchi hii iliyokuwa jangwa, sasa imekuwa kama bustani ya Edeni, nayo miji iliyokuwa ukiwa, matongo na mabomoko, sasa inakaliwa na watu, tena inazungukwa na kuta!

36Hapo mataifa yaliyobaki kandokando yenu, yatatambua kwamba ni mimi Yawe niliyejenga upya yaliyoharibiwa na kupanda mbegu katika inchi iliyokuwa jangwa. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo, na nitafanya hayo.

37Bwana wetu Yawe anasema hivi: Waisraeli wataniomba niwafanye kuwa wengi kama kundi la kondoo, nami nitawafanya hivyo.

38Wataniomba wakuwe wengi kama kundi la kondoo wa kutolewa sadaka, kama kundi la kondoo katika Yerusalema wakati wa sikukuu zake. Hivi ndivyo miji yenu iliyokuwa ukiwa itakavyojaa makundi ya watu. Kwa hiyo watatambua kwamba mimi ni Yawe.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help