Yeremia 48 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Neno la Yawe juu ya inchi ya Moabu

1Juu ya inchi ya Moabu, Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi:

Ole kwa watu wa Nebo, maana muji wao umeharibiwa!

Kiriataimu umepatishwa haya, umetekwa,

ukuta wake umebomolewa;

2utukufu wa inchi ya Moabu umetoweka.

Mupango ulifanywa huko Hesiboni juu yake:

Basi! Tuwaangamize wasikuwe tena taifa!

Nawe muji wa Madimeni utanyamazishwa,

upanga utakufuatilia.

3Sikiliza! Kilio kutoka Horonaimu:

Maangamizi na uharibifu mukubwa!

4Moabu imekwisha kuangamizwa,

kilio chake kinasikilika mpaka Zoari.

5Wale wanaopanda kwenda Luhiti

wanalia kwa sauti.

Wanapoteremuka kwenda Horonaimu,

wanasikia kilio cha uharibifu.

6Mukimbie! Mujiokoe wenyewe!

Mukimbie kama punda wa pori katika jangwa!

7Moabu, ulitumainia matendo yako na hazina zako,

lakini sasa wewe vilevile utatekwa;

mungu wako Kemosi atapelekwa katika uhamisho

pamoja na makuhani na watumishi wake.

8Mwangamizaji atapita katika kila muji,

hakuna muji utakaomwepuka;

mabonde yataangamia,

nafasi zenye kunyooka zitaharibiwa,

kama vile Yawe alivyosema.

9Muchimbie Moabu kaburi,

maana kuangamia kwake ni hakika;

miji yake itakuwa tupu,

bila mukaaji hata mumoja.

10Alaaniwe mutu anayefanya kazi ya Yawe kwa uregevu; alaaniwe anayezuia upanga wake usimwange damu!

11Moabu amestarehe tangu ujana wake,

ametulia kama divai katika mutungi.

Hajamimiliwa toka chombo kimoja katika chombo kingine,

hajapata kupelekwa katika uhamisho.

Kwa hiyo angali na onjo yake,

harufu yake nzuri haijabadilika hata kidogo.

12Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitamupelekea wamimiaji ambao wataimimia divai yake.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Wataimwanga yote kutoka vyombo vyake na kuvivunja vipandevipande.

13Halafu Wamoabu watapata haya kwa ajili ya mungu wao Kemosi, kama vile watu wa Israeli walivyopata haya kwa ajili ya kutegemea Beteli.

14Namna gani munaweza kusema: Sisi ni mashujaa,

na watu wenye nguvu nyingi za vita?

15Mwangamizaji wa Moabu na miji yake anashambulia,

vijana wake wazuri wamechinjwa.

–Ni ujumbe wa Mufalme, jina lake Yawe wa majeshi.–

16Uharibifu wa Moabu umekaribia,

maangamizi yake yanakuja haraka.

17Muomboleze juu ya Moabu, enyi wajirani zake wote,

na wote munaomujua vizuri

museme: Namna gani nguvu kama hii ilivunjwa,

uwezo ule wenye utukufu?

18Enyi wenyeji wa Diboni:

mushuke kutoka pahali penu pa utukufu,

muikae juu ya udongo usiokuwa na maji.

Maana mwangamizaji wa Moabu,

amefika kuwashambulia;

amekwisha haribu kuta zenu.

19Enyi wakaaji wa Aroeri,

musimame kandokando ya njia mupeleleze!

Mumwulize yule anayekimbia na anayetoroka:

Kumetokea nini?

20Moabu imepatishwa haya maana imevunjika.

Muomboleze na kuililia.

Mutangaze kandokando ya muto Arnoni,

kwamba Moabu imeharibika kabisa.

21Hukumu imeifikia miji ya nafasi ya uwanja: Holoni, Yahasa, Mefati,

22Diboni, Nebo, Beti-Diblataimu,

23Kiriataimu, Beti-Gamuli, Beti-Meoni,

24Kerioti na Bosira. Kweli, hukumu imeifikia miji yote ya Moabu ya mbali na ya karibu.

25Nguvu za Moabu zimevunjika na uwezo wake umevunjika. –Ni ujumbe wa Yawe.–

26Mumuleweshe Moabu kwa sababu alijitukuza juu yangu mimi Yawe. Moabu atagaagaa katika matapiko yake na watu watamuchekelea.

27Ee Moabu, si ulimuchekelea Israeli! Ulimuhesabu kama mwenzake na wanyanganyi hata ukakuwa unatikisa kichwa chako kila mara uliposema juu yake.

28Enyi wenyeji wa Moabu,

mutoke katika miji, muende kukaa chini ya mawe!

Muige jinsi njiwa anavyojenga chicha chini ya jiwe.

29Tumesikia juu ya kiburi cha Moabu;

Moabu ana majivuno sana.

Tumesikia juu ya kujiona, kiburi na majivuno yake;

tumesikia jinsi anavyojisifu ndani ya moyo.

30Ninajua kiburi chake.

–Ni ujumbe wa Yawe.–

Majivuno yake ni ya bure,

na matendo yake si kitu.

31Kwa hiyo ninaomboleza juu ya Moabu,

ninalia kwa ajili ya Wamoabu wote,

ninaomboleza juu ya watu wa Kiri-Heresi.

32Ninakulilia wewe muzabibu wa Sibuma

kuliko hata watu wa Yazeri.

Matawi yako yametanda

mpaka ngambo ya bahari ya Chumvi,

yakafika hata mpaka Yazeri.

Lakini mwangamizaji ameyarukia

matunda yako ya wakati wa jua na mizabibu yako.

33Furaha na shangwe zimeondolewa

kutoka inchi ya Moabu yenye mboleo.

Nimeikomesha divai kutoka katika vikamulio.

Hakuna mutu anayekamua mizabibu kwa shangwe;

kelele zinazosikilika si za shangwe.

34Kilio cha watu wa Hesiboni kinasikilika huko Eleale mpaka Yasa; kinaenea kutoka Soari mpaka Horonaimu na kufika hata Eglati-Selisia. Hata maji ya kijito Nimurimu yamekauka.

35Nami nitamuteketeza kila mutu katika Moabu ambaye anatambikia juu ya vilima na kumufukizia mungu wake ubani.

–Ni ujumbe wa Yawe.

36Kwa hiyo, moyo wangu unaomboleza juu ya watu wa Moabu na watu wa Kiri-Heresi, kama vile filimbi; maana hata mali yote waliyojipatia imeangamia.

37Kila mutu amenyoa kichwa na ndevu zake. Wote wamejikatakata kwenye mikono na kwenye viuno wamevaa gunia.

38Juu ya nyumba za Moabu na katika viwanja vyao hakuna kinachosikilika lakini maombolezo tu. Mimi nimemuvunja Moabu kama chombo kisichotakiwa na mutu.

–Ni ujumbe wa Yawe.

39Angalia jinsi alivyovunjika! Angalia jinsi wanavyoomboleza! Ni ajabu jinsi Moabu alivyorudi nyuma juu ya haya! Moabu amekuwa kitu cha kuchekesha na kitisho kwa jirani zake wote.

40Yawe anasema hivi:

Taifa litaruka mbio juu ya Moabu,

kama tai aliyekunjua mabawa yake.

41Miji yake itatekwa,

kuta zake vilevile.

Siku hiyo mioyo ya waaskari wa Moabu

itakuwa kama vile moyo wa mwanamuke anayezaa.

42Wamoabu wataangamizwa, hata hawatakuwa tena taifa,

kwa sababu walijitukuza mbele ya Yawe.

43Kitisho, mashimo na mutego,

vinawangojea enyi watu wa Moabu.

–Ni ujumbe wa Yawe.

44Atakayetoroka kitisho

atatumbukia ndani ya shimo;

atakayetoka ndani ya shimo

atanaswa katika mutego.

Kwa maana nitaleta mambo hayo juu ya Moabu,

katika mwaka wao wa azabu.

–Ni ujumbe wa Yawe.

45Wakimbizi wanaochoka wanasimama chini ya kivuli cha Hesiboni.

Moto umewaka huko katika muji;

ulimi wa moto toka nyumba ya kifalme ya Sihoni;

umeteketeza mipaka ya Moabu,

umeunguza milima ya hao wanaopiga kelele.

46Ole kwenu watu wa Moabu!

Watu wa Kemosi sasa mumeangamizwa,

wana wenu wamekamatwa mateka,

wabinti zenu wamepelekwa katika utumwa.

47Lakini katika siku zinazokuja

nitawarudisha tena Moabu katika hali yao.

–Ni ujumbe wa Yawe.

Hii ndiyo hukumu juu ya Moabu.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help