1Munisikilize, enyi inchi za mbali,
Mutege sikio, enyi watu wa mbali!
Yawe aliniita mbele sijazaliwa,
alitaja jina langu nikiwa katika tumbo la mama yangu.
2Alifanya maneno yangu kuwa makali kama upanga mukali,
alinificha katika kivuli cha mukono wake;
aliufanya ujumbe wangu kuwa mukali kama chongo ya mushale,
akanificha kama mushale ndani ya mufuko wake.
3Aliniambia: Wewe ni mutumishi wangu;
kwa njia yako, ee Israeli, watu watanitukuza.
4Lakini mimi nikafikiri:
Nimeshugulika bure,
nimetumia nguvu zangu bure kabisa.
Hata hivyo, Yawe atanipa haki yangu;
mushahara wa kazi yangu uko kwa Mungu.
5Lakini sasa Yawe anasema.
Aliniita tangu katika tumbo la mama
kusudi nipate kuwa mutumishi wake,
nilirudishe taifa la Yakobo kwake
na kukusanya wazao wa Israeli kwake.
Yawe amenijalia heshima mbele yake.
Mungu wangu amekuwa nguvu yangu.
6Yeye anasema: Haitoshi tu wewe kuwa mutumishi wangu,
kusudi uyainue makabila ya Yakobo,
na kurudisha watu wa Israeli waliobaki.
Nitakufanya ukuwe mwangaza wa mataifa,
kusudi watu wote wapate kuokolewa katika dunia.
7Yawe, Mukombozi na Mutakatifu wa Israeli,
anamwambia hivi yule anayezarauliwa sana,
yule anayechukiwa na mataifa,
na ambaye ni mutumishi wa watawala:
Wafalme wataona nao watasimama;
wakubwa watainama na kuabudu
kwa heshima ya Yawe
ambaye anatimiza ahadi zake,
kwa heshima ya Mutakatifu wa Israeli
ambaye amekuchagua wewe.
Kujengwa upya kwa Yerusalema8Yawe anasema hivi:
Wakati uliofaa nilijibu maombi yako;
wakati wa wokovu nilikusaidia.
Nimekuweka na kukufanya
ukuwe kiungo cha agano langu na mataifa yote:
utatengeneza inchi
na kurudisha tena inchi hiyo iliyoharibika.
9Utawaambia wafungwa: Mutoke humo katika kifungo
na wale wanaokuwa katika giza: Mukuje inje kwenye mwangaza!
Kila pahali watakapokwenda watapata chakula
hata kwenye vilima vitupu watapata malisho.
10Hawatasikia tena njaa wala kuwa na kiu.
Upepo wenye kuunguza wala jua havitawachoma,
mimi niliyewahurumia nitawaongoza
na kuwapeleka kwenye chemichemi za maji.
11Milima yote nitaifanya kuwa njia,
na barabara zangu kubwa nitazitengeneza.
12Watu wangu watarudia kutoka mbali,
wengine kutoka kaskazini na magaribi,
wengine kutoka upande wa kusini.
13Muimbe kwa furaha, enyi mbingu!
Ushangilie ewe dunia,
Enyi milima, mulalamike kwa furaha,
maana Yawe amewafariji watu wake,
anawaonea huruma watu wake wanaoteseka.
14Wewe Sayuni unasema:
Yawe ameniacha.
Hakika Bwana wangu amenisahau.
15Lakini Yawe anasema:
Munafikiri kwamba mama anaweza kumusahau mutoto anayemunyonyesha,
wala kumuchukia mutoto wa tumbo lake?
Hata kama mama anaweza kumusahau mutoto wake,
mimi sitakusahau hata kidogo.
16Nimekuchora wewe katika vitanga vya mikono yangu;
kuta zako ninaziona mbele yangu siku zote.
17Watakaokujenga upya wanakuja haraka,
wale waliokuharibu wanaondoka.
18Inua macho uangalie pande zote;
watu wako wote wanakusanyika na kukufikia.
Kama vile ninavyoishi,
watu wako watakuwa kwako kama mapambo,
utawafurahia kama vile bibi arusi anavyofanya na taji lake.
–Ni ujumbe wa Yawe.
19Kweli umepatwa na uharibifu,
makao yako yamekuwa matupu,
na inchi yako imeteketezwa.
Lakini sasa itakuwa ndogo sana kwa wakaaji wake.
20Watoto wako waliozaliwa katika uhamisho,
watakulalamikia wakisema:
Inchi hii ni ndogo sana;
utupatie nafasi zaidi ya kuishi.
21Kwa hiyo utajiuliza mwenyewe:
Nani aliyenizalia watoto hawa wote?
Nilikufiwa na watoto bila kupata wengine.
Nilipelekwa katika uhamisho na kutupwa mbali;
nani basi aliyewalea watoto hawa?
Mimi niliachwa peke yangu,
sasa, hawa wametoka wapi?
22Bwana wetu Yawe anasema hivi:
Nitasimika bendera kwa kuita mataifa;
nitayaonyesha kitambulisho.
Nayo yatawarudishia wana wenu wakiwabeba kwenye kifua,
vilevile na wabinti zenu kwenye mabega.
23Wafalme watakushugulikia,
na malkia watakutengenezea chakula.
Watainama mbele yako uso mpaka chini,
na kulambula mavumbi ya miguu yako.
Halafu utatambua kwamba mimi ni Yawe;
wote wanaonitegemea hawatapata haya.
24Watu wa Yerusalema wanalalamika:
Shujaa, anaweza kunyanganywa vitu alivyoteka?
Au wafungwa wa mutu mutesaji wanaweza kuokolewa?
25Yawe anasema hivi:
Kweli! Hata mateka za shujaa zitarudishwa,
wafungwa wa mutu mutesaji wataokolewa.
Mimi mwenyewe nitawapiganisha waadui zako,
mimi mwenyewe nitawaokoa watoto wako.
26Nitawasukuma watesaji wako wakule miili yao wenyewe;
watalewa damu yao wenyewe kama divai.
Halafu wanadamu wote watatambua kwamba
mimi ni Yawe, Mwokozi wako,
Mukombozi wako, Mwenye Nguvu wa Yakobo.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.