2 Samweli 16 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Siba na mufalme Daudi

1Daudi alipokuwa ametambuka kidogo tu kichwa cha mulima, Siba mutumishi wa Mefiboseti akakuja kumupokea Daudi akiwa na punda wawili ambao walikuwa wametandikwa nao wakibeba mikate mia mbili, vishada mia moja vya zabibu yenye kukauka, matunda mia moja ya wakati wa jua na mufuko wa ngozi unaojaa divai.

2Mufalme akamwuliza Siba: “Kwa nini umeleta vitu hivi?”

Siba akamujibu: “Punda ni kwa ajili ya kubeba watu wa jamaa yako, mikate na matunda ni kwa ajili ya vijana wote, nayo divai ni kwa ajili ya wale watakaochoka katika jangwa.”

3Mufalme akamwuliza: “Mwana wa bwana wako yuko wapi?”

Siba akamwambia mufalme: “Yeye amebaki Yerusalema kwa sababu anazani kwamba watu wa Israeli watamurudishia ufalme wa Saulo babu yake.”

4Mufalme akamwambia Siba: “Basi, yale yaliyokuwa mali ya Mefiboseti sasa ni mali yako.”

Siba akamwambia: “Ninashukuru, bwana wangu mufalme, nami ninaomba nipate kukubaliwa mbele yako siku zote.”

Simei anamulaani mufalme Daudi

5Wakati Daudi alipofika kule Bahurimu, kulitokea mutu mumoja wa ukoo wa Saulo, jina lake Simei mwana wa Gera, akaanza kumulaani Daudi kwa mufululizo.

6Akakuwa anamutupia mufalme Daudi pamoja na watumishi wake mawe ingawa watu wengine wote na mashujaa walikuwa wakimuzunguka Daudi upande wa kuume na wa kushoto.

7Simei alimulaani Daudi akisema: “Kwenda! Kwenda, wewe mwuaji, mutu wa ovyoovyo!

8Yawe amekulipiza kisasi kutokana na kumwanga damu ya watu wote wa jamaa ya Saulo, ambaye sasa wewe umenyanganya ufalme kwa pahali pake. Sasa, Yawe amemupa mwana wako Abusaloma ufalme. Maangamizi yamekupata kwa sababu wewe ni mwuaji.”

9Kwa hiyo, Abisayi mwana wa Zeruya akamwambia mufalme: “Kwa nini huyu anayekuwa sawa imbwa mufu akulaani wewe bwana wangu mufalme? Uniruhusu nimwendee, nami nitakikata kichwa chake.”

10Lakini mufalme akamwambia: “Kuna maneno gani kati yangu na ninyi wana wa Zeruya? Ikiwa Yawe amemwambia: ‘Umulaani Daudi’, nani sasa anaweza kuuliza: ‘Kwa nini umefanya hivyo?’ ”

11Tena mufalme Daudi akamwambia Abisayi na hata watumishi wake wote: “Ikiwa mutoto wangu mwenyewe anayawinda maisha yangu, si ni zaidi kwa mutu wa kabila la Benjamina? Ninyi muache anilaani maana Yawe amemwagiza anilaani.

12Labda Yawe ataangalia mateso yangu, naye atanilipa wema kwa laana hii ninayopata leo.”

13Kwa hiyo, mufalme Daudi na watu wake wakaendelea na safari, naye Simei akiwa anamufuata akimutupia mawe na kurusha mavumbi juu ya mufalme Daudi. Simei alikuwa akitembea kwenye kilele cha mulima, akielekea mufalme Daudi.

14Kisha mufalme pamoja na watu wote waliokuwa pamoja naye, wakafika kwenye muto wakiwa wamechoka. Basi wakapumzika.

Abusaloma katika muji Yerusalema

15Wakati ule, Abusaloma na watu wote wa Israeli wakaenda Yerusalema na Ahitofeli akiwa pamoja nao.

16Husayi wa inchi ya Arki, rafiki ya Daudi, akamwendea Abusaloma, akamwambia: “Uishi milele, ee mufalme! Uishi milele, ee mufalme!”

17Abusaloma akamwuliza Husayi: “Huu ndio uaminifu wako kwa rafiki yako Daudi? Mbona haukuenda pamoja na rafiki yako?”

18Husayi akamujibu: “Hapana! Maana yule ambaye amechaguliwa na Yawe, watu hawa na watu wote wa Israeli, mimi nitakuwa wake, na nitabaki naye.

19Zaidi ya hayo, nitamutumikia nani? Si mwana wa rafiki yangu? Basi, kama nilivyomutumikia baba yako ndivyo nitakavyokutumikia wewe.”

20Halafu Abusaloma alimwambia Ahitofeli: “Unipatie shauri; tufanye nini?”

21Ahitofeli akamwambia Abusaloma: “Ulale na wale wahabara za baba yako ambao aliwaacha kuangalia nyumba yake. Kisha watu wote wa Israeli watakaposikia kwamba umechukizwa na baba yako, hapo watu wote wanaokuwa pamoja nawe watapata nguvu.”

22Kwa hiyo, watu wakamupigia Abusaloma hema kwenye paa, naye akalala na wahabara za baba yake, watu wote wa Israeli wakiwa wanaona.

23Siku hizo, shauri lolote Ahitofeli alilotoa lilikuwa kama limetolewa na Mungu. Na shauri la Ahitofeli liliheshimiwa na Daudi na Abusaloma.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help