1Mwana wangu, sikia hekima yangu,
tega sikio usikie elimu yangu.
2Kwa hiyo, utaweza kulinda akili,
na kinywa chako kitashika maarifa.
3Midomo ya mwanamuke mupotovu ni mitamu kama asali,
maneno yake ni laini kuliko mafuta;
4lakini kwa mwisho ni michungu kama nyongo,
ni mikali kama upanga wenye makali ngambo mbili.
5Miguu yake inaelekea chini kwenye kifo,
hatua zake zinaenda kuzimu.
6Yeye haijali njia ya uzima,
njia zake ni za kutangatanga, wala hajui.
7Sasa enyi wana wangu, musikilize,
wala musisahau maneno ya kinywa changu.
8Uepushe njia yako mbali naye,
wala usiukaribie mulango wa nyumba yake,
9kusudi usiwape wengine heshima yako,
na watenda mabaya miaka yako,
10wageni wasipate kushibishwa kwa mali yako,
na faida ya kazi yako kuishia katika nyumba ya mugeni.
11Kwa mwisho wa maisha yako utaomboleza,
wakati mwili wako utakapoangamizwa.
12Kwa hiyo utasema: “Kwa nini nilichukia mafundisho?
Kwa nini nilizarau ndani ya moyo wangu?
13Sikusikiliza sauti ya walimu wangu,
wala kuwategea sikio wale walionifundisha.
14Nikakuwa karibu ya kuangamia kabisa
katika kusanyiko na mukutano wa watu.”
15Kunywa maji ya birika lako mwenyewe,
maji yanayobubujika katika kisima chako mwenyewe.
16Kwa nini chemichemi zako zitawanywe mbali,
na vijito vya maji katika barabara?
17Hiyo ni yako wewe mwenyewe,
wala usiwashirikishe watu wengine.
18Chemichemi yako ibarikiwe,
umufurahie muke uliyemwoa ukiwa kijana.
19Ni muzuri kama pongo, anapendeza kama paa.
Mapenzi yake yakufurahishe kila wakati,
uvutwe siku zote na mapendo yake.
20Mwana wangu, kwa nini kutekwa na mwanamuke mwasherati?
Kwa nini kukumbatia mwanamuke mugeni katika kifua?
21Maana mwenendo wa kila mutu ni wazi mbele ya Yawe;
yeye anachunguza njia zake zote.
22Mutu mwovu ananaswa kwa uovu wake mwenyewe;
anakamatwa na vifungo vya zambi yake mwenyewe.
23Yeye anakufa kwa ajili ya ukosefu wa mafundisho,
anaangamia kwa sababu ya upumbafu wake mukubwa.
Who We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.