Hosea 10 - Swahili Congo Revised Bible 2002

Kuharibishwa kwa vitu vya ibada vya Israeli

1Waisraeli walikuwa kama muzabibu muzuri,

muzabibu wenye kuzaa matunda.

Kadiri matunda yalivyozidi kuongezeka,

ndivyo walivyozidi kujijengea mazabahu.

Kadiri inchi yao ilivyozidi kustawi,

ndivyo walivyozidi kupamba nguzo zao za ibada.

2Mioyo yao imejaa udanganyifu.

Sasa ni lazima wabebe makosa yao.

Yawe atabomoa mazabahu zao

na kuziharibu nguzo zao.

3Wakati huo watasema:

Hatuna tena mufalme,

kwa maana hatumwogopi Yawe;

lakini, naye mufalme atatufanyia nini?

4Wanachosema ni maneno matupu;

wanaapa na kufanya mapatano ya bure;

haki imekuwa si haki tena,

inachipuka kama mimea yenye sumu katika shamba.

5Wakaaji wa Samaria watatetemeka

kwa sababu ya sanamu ya mwana-ngombe wa kule Beteli.

Watu wake watamwombolezea mwana-ngombe yule,

hata makuhani wanaomwabudu watamulilia;

maana utukufu wa mwana-ngombe yule umeondolewa.

6Sanamu hiyo itapelekwa Asuria,

kama zawadi kwa mufalme mukubwa.

Watu wa Efuraimu watafezeheka,

Waisraeli watapata haya kwa ajili ya sanamu yao.

7Mufalme wa Samaria atapelekwa,

kama kipande cha muti juu ya maji.

8Pahali pa kutambikia juu ya vilima pa Aweni,

pahali Waisraeli walipofanyia zambi, pataharibiwa.

Miiba na michongoma vitaota katika mazabahu zao.

Nao wataiambia milima: Mutufunike

na vilima: Mutuangukie!

Israeli atavuna alichopanda

9Enyi Waisraeli,

ninyi mumetenda zambi tangia kule Gibea,

na mpaka sasa munaendelea.

Hakika vita itawaangamizia kulekule Gibea.

10Nitawaendea watu hawa wapotovu na kuwaazibu;

watu wa mataifa watakusanyika kwa kuwashambulia,

watakapoazibiwa kwa ajili ya zambi zao nyingi.

11Efuraimu ni mwana-ngombe aliyefundishwa vizuri,

akapenda kupepeta ngano.

Lakini sasa shingo yake nzuri nitaifunga nira.

Yuda atalima kwa jembe yeye mwenyewe,

Yakobo atakokota jembe la kupalilia.

12Mupande haki kwa faida yenu,

nanyi mutavuna wema;

mulime mashamba yaliyoachwa,

maana wakati wa kutafuta Yawe umefika

kusudi awanyeshee haki kama mvua.

13Lakini ninyi mumepanda uovu,

ninyi mumevuna ubaya;

mumekula matunda ya uongo wenu.

Wewe Israeli ulitegemea nguvu zako mwenyewe,

na wingi wa waaskari wako.

14Kwa hiyo fujo ya vita itawafikia watu wako,

kuta zako zote zitaharibiwa.

Kama vile mufalme Salmani alivyoharibu Beti-Arbeli katika vita,

wamama wakapondwa pamoja na watoto wao.

15Ndivyo itakavyokuwa kwenu enyi watu wa Beteli,

kwa sababu ya uovu wenu mukubwa.

Kutakapopambazuka mufalme wa Israeli atauawa.

Blog
About Us
Message
Site Map

Who We AreWhat We EelieveWhat We Do

Terms of UsePrivacy Notice

2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.

Home
Gospel
Question
Blog
Help