1Nimevunjika moyo, siku zangu zimekwisha,
kaburi langu liko tayari.
2Kweli wanaonichekelea wamenizunguka,
matusi yao yananizuiza kulala.
3Ee Mungu, ujitoe mwenyewe kuwa rehani kwa ajili yangu
maana hakuna mwingine wa kujitoa kwa ajili yangu.
4Umefumba akili za warafiki zangu;
usiwaache basi wanishinde.
5Mutu anayefitini warafiki zake kwa faida,
watoto wake watakufa macho.
6Nimefanywa kuwa kichekesho kwa watu,
nimekuwa mutu wa kutemewa mate.
7Macho yangu yamefifia kwa ajili ya uchungu;
viungo vyangu vyote vimekuwa kama kivuli.
8Watu wa haki wanashangaa wanapoona hayo,
nao wasiokuwa na kosa wanachukizwa
na wasiomwogopa Mungu.
9Hata hivyo, mutu wa haki anashika njia yake,
mutu ambaye hajafanya ubaya kwa mukono wake anazidi kuwa na nguvu.
10Lakini ninyi mukuje, mukuje wote tena.
Kwenu sitamupata mwenye hekima hata mumoja.
11Siku zangu zimekwisha, mipango yangu imevunjwa,
matazamio ya moyo wangu yametoweka.
12Kwa hao watu, usiku ni muchana:
wanasema kwamba mwangaza unakaribia giza.
13Kama kuzimu kukiwa nyumba yangu,
na makao yangu yako kule katika giza,
14kama nikiita kaburi “baba yangu”
na vidudu “mama yangu” au “dada yangu”,
15basi, nimebakiliwa na tumaini gani?
Ni nani anayeweza kuona tumaini lile?
16Tazamio langu litashuka nami kuzimu!
Tutateremuka wote wawili mpaka kule katika mavumbi!
Masemi ya pili ya BildadiWho We AreWhat We EelieveWhat We Do
2025 by iamachristian.org,Inc All rights reserved.